Home » » KAUSTA WAOMBA KUUNGWA MKONO SHULE ZA KATA

KAUSTA WAOMBA KUUNGWA MKONO SHULE ZA KATA

UMOJA wa wanafunzi wa vyuo vikuu Tanzania kutoka mkoani Kagera (Kausta), umewaomba wadau wa sekta mbalimbali kujitokeza kuwaunga mkono ili waweze kwenda kujitolea katika shule za kata.
Ombi hilo lilitolewa hivi karibuni na Mwenyekiti wa Kausta Mkoa wa Kagera, David Willbard, wakati alipokuwa akisoma taarifa katika kikao kilichowahusisha viongozi wa kada mbalimbali kwenye Ukumbi wa Mkuu wa Mkoa mjini Bukoba.
Willbard alisema kuwa wameamua kuwaita viongozi hao ili waweze kujadili kwa pamoja ufundishaji na namna bora ya kuanzisha mfuko shirikishi kusaidia wanafunzi wa umoja huo watakaokwenda kujitolea katika shule hizo pamoja na kutafuta suluhu ya kudumu juu ya suala la taaluma katika Mkoa wa Kagera ambao unaonekana kuwa na changamoto kubwa kwa kizazi hiki.
Alisema vyuo vikuu husaidiana baina ya wanafunzi wenyewe katika kutatua changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wakiwa vyuoni na kuangalia namna bora ya kuinua maendeleo ya Mkoa wa Kagera katika nyanja mbalimbali za kitamaduni, kijamii, kiuchumi na hata kisiasa.
Hata hivyo, alisema kuwa wameamua kwenda kujitolea katika shule za kata, kutokana na kuziona zimekuwa zikifanya vibaya katika mitihani ya kidato cha nne, hivyo kutokana na utafiti uliofanywa na Kausta mwaka 2012, waliona kiwango cha elimu katika mkoa huo ni tofauti na miaka ya70 na 80.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali mstaafu Fabiani Massawe, alisema kuwa uongozi wa mkoa umepokea suala hilo na watawaunga mkono ili kuona kama ufaulu katika shule za kata utaongezeka.
Pia, amewataka wanafunzi wanaohitimu vyuo vikuu kuachana na tabia ya kukaa nyumbani wakisubiri matokeo, badala yake wajitolee katika shule kama hizo ili kujijengea uelewa zaidi.
Chanzo;Tanzania Daima

1 comments:

Unknown said...

Ndibalema Twinomukama. ilo ni wazo zuri na la kuunga mkono ili liwe endelevu. wadogo zetu wanashindwa kufanya vizuri kimasomo kutokana na upungufu wa walimu. kwa njia yoyote ile nawa support KAUSTA na kwa mchango zaidi 0715 983089 mwenyekiti au kiongozi yoyote katika chama nitafuteni kwa namba iyo.

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa