Home » » ‘USHIRIKA MULEBA WAPINDISHA SHERIA YA UCHAGUZI’

‘USHIRIKA MULEBA WAPINDISHA SHERIA YA UCHAGUZI’

 
BAADHI ya wakulima wa chama cha ushirika cha Kamachumu kilichopo Wilayani Muleba Mkoani Kagera wamedai kuwa uchaguzi wa kuwachagua wajumbe wa bodi na mwenyekiti wa chama hicho uliofanyika wiki iliyopita ulikuwa batili kutokana na sheria namba sita ya ushirika kukiukwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mkutano kabla ya kufanyika kwa uchaguzi huo mbele ya Afisa ushirika wilayani Missenyi Humphery Kachelele, aliyekuwa msimamizi wa uchaguzi huo walisema sheria hiyo inakataza mwanachama ambaye ni kiongozi wa siasa kugombea nafasi yoyote katika ushirika hadi atakapojiuzuru wadhifa wake.
Diocles Rutabana alisema sheria hiyo inakataza wanasiasa kugombea nafasi za uongozi katika ushirika lakini cha ajabu waliochukuwa fomu ya kugombea nyadhifa hizo (majina yanahifadhiwa) ni viongozi wa chama cha siasa kikongwe nchini.
Alisema kutokana na hayo inaonyesha wazi kuwa uchaguzi huo ni batili kutokana na makao makuu kushindwa kusimamia vyema sheria hiyo na hata katika suala la ugawaji fomu.
Rutabana alidai kuwa mwenyekiti wao Superi Karugaba aliamua kuficha fomu hizo ili kumuwezesha kurudi katika nafasi yake pamoja na bodi yake huku ikiwanyima fursa wanachama waliokuwa na nia ya kuwania nyadhifa hizo.
“Viongozi wote waliokuwa madarakani walichukuwa fomu pamoja na mtu mmoja huku kiongozi wa juu wa ushirika akizificha fomu hizo ili wengine wasipate nafasi ya kugombea,” alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo wagombea waliochukua fomu walipita bila kupingwa kutokuwa na kukosa upinzani.
Akizungumza katika kikao hicho, Kachelele alisema yeye ndiye mtafsiriwa sheria hivyo hakuna mtu yeyote anayeweza kumshinikiza katika hilo.
Hata hivyo aliwauliza wagombea hao iwapo ni wanasiasa ambapo walikana madai hayo na kusema kuwa walishajiuzuru.
Alikwenda mbali zaidi na kutoa onyo kwa wanachama hao ya kuwa iwapo watasusia uchaguzi huo, atalazimika kuendelea na uchaguzi hata wakibaki wawili.
Naye mtendaji wa kijiji cha Kamachumu Lenard Anseremy, alisema kuwa ni mgombea mmoja aliyejiuzulu wadhifa wake lakini waliobaki walikidanganya kikao hicho kwani hadi sasa bado wanaendelea na shughuli zao.
Akizungumzia tuhuma za kuficha fomu Karugaba, alisema kuwa madai hayo hayana ukweli wowote kwa kuwa matangazo yalitolewa ya ugawaji wa fomu na hakuna wanachama waliofika kuchukua.
Kuhusu kuwania nafasi hiyo kwa miaka 30 pamoja na bodi yake wakiwa ni walewale, mwenyekiti huyo alisema kuwa suala hilo linapaswa kujibiwa na msimamizi wa uchaguzi huo
Chanzo:Tanzani Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa