Home » » Operesheni Kimbunga yatumika kutapeli

Operesheni Kimbunga yatumika kutapeli

WANANCHI wa maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Bukoba vijijini mkoani Kagera wamekumbwa na taharuki kubwa baada ya askari mgambo kujifanya maofisa wa Operesheni Kimbunga awamu ya tatu, huku wakijitambulisha kama maofisa Usalama wa Taifa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Kwa mujibu wa taarifa zilizolifikia gazeti hili, mgambo hao walifika katika maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Rubale wakiwa wamevalia sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Akizungumza na Tanzania Daima, Shaban Buruan ambaye ni mmiliki wa duka la bidhaa mbalimbali, alisema akiwa dukani kwake lilifika kundi la watu, wengine wakiwa wamevalia sare za JWT na wengine kiraia, wakamueleza kuwa ni maofisa wa Operesheni Kimbunga awamu ya tatu, wakiongozana na mtendaji wa Kijiji cha Kihumulo, Gidius Alfred.
Buruan alisema baada ya kujitambulisha, walimuomba leseni ya biashara huku wale waliokuwa wamevalia kiraia wakijitambulisha kama maofisa wa TRA.
Alisema kuwa hakuwapa leseni hiyo kwa vile hakuwa nayo mahala hapo, na hivyo wakamtaka awape fedha sh laki moja, jambo ambalo hakuliafiki badala yake akaomba muda awaletee, lakini waliondoka.
Naye Clementina Kakooza ambaye ni raia wa Rwanda aliyeolewa Tanzania, alisema mgambo hao walifika kwake wakiwa na sare za JWTZ wakiongozana na mtendaji wa kijiji na kumtaka awaonyeshe vibali vyake vya kuishi nchini la sivyo watamfikisha polisi.
“Waliponitishia hivyo niliwaeleza kuwa nimebaki kutokana na agizo la serikali kuwa watu tulioolewa na Watanzania tubaki wakati tukifanya utaratibu wa kupata vibali, walikataa na kusema kuwa niwapatie kiasi cha sh 500,000 ambacho sikuwa nacho.
“Nikataka niwape ng’ombe wawili na mbuzi mmoja wakagoma na kulazimisha niwapatie fedha, hapo ndipo tuliposhituka na kupiga simu polisi Rubale,” alisema. 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Philip Kalangi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo Oktoba 26 mwaka huu, katika Kijiji cha Kihumulo, Tarafa ya Rubale, Halmashauri ya Bukoba.
Alisema kuwa baada ya Operesheni Kimbunga awamu ya pili kitaifa kumalizika, walikabidhi majukumu yote kwa kamati ya ulinzi na usalama za vitongoji, kata, wilaya na mkoa kuendelea na taratibu za kubaini wahalifu wa makosa mbalimbali.
Kalangi alisema wakiwa katika maeneo mbalimbali ya kutekeleza majukumu ya kikazi, walipata taarifa kuwa kuna mgambo walionekana wakifanya kazi ya kukamata watu na kuwahoji, hususani wahamiaji haramu. Walifika eneo la tukio na kufanikiwa kuwakamata mgambo watatu.
Aliwataja waliowakamatwa kuwa ni Amran Sadick, Abeid Amada na Mathias Sospeter ambao ni mgambo wa Manispaa ya Bukoba na Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Kihumulo, Gidius Alfred.
Alisema mtendaji huyo alikamatwa kwa kosa la kushirikiana na mgambo hao kufanya kazi bila kushirikiana na uongozi wa kata na wilaya.
Kwa mujibu wa Kalangi, walipofikishwa polisi na kuhojiwa hawakuwa na la kujitetea zaidi ya kuomba msamaha.
Alisema watuhumiwa wote wamefikishwa mahakamani kwa kosa la kudai fedha kwa njia ya vitisho na uchunguzi unaendelea ili kuendelea kubaini makosa yao mengine kwa ajili ya kuwasilisha ushahidi mahakamani.
Hata hivyo, alifafanua kuwa wakati watuhumiwa hao wanakamatwa, hawakuwa na sare za jeshi lolote na kwamba uchunguzi bado unaendelea.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa