OPERESHENI KIMBUNGA AWAMU YA PILI SASA KUHAMIA MIKOA YA KAGERA, KIGOMA NA GEITA


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Awamu ya Pili ya Operesheni Kimbunga imeweza kukamata majambazi ya kutumia silaha 67 na wahamiaji haramu 134  katika kipindi cha wiki moja tangu  kuanza kwake Septemba 21hadi Septemba 27 mwaka huu katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita.
Silaha zilizokamatwa ni pamoja na bunduki aina ya SMG Moja, Pistol Moja na Magobole 17 pamoja na risasi 115 zikiwemo za bunduki aina ya SMG 102 na Risasi za Pistol 13. Aidha, Magazine mbili zilikamatwa pamoja na Sare za Jeshi la Burundi.
Wahamiaji haramu waliokamatwa wengi wao ni kutoka nchi za Burundi ambapo raia wake 114 walikamatwa wakiishi nchini kinyume na sheria wakati raia wa Rwanda 20 walikamatwa katika kipindi hicho.
Aidha, watu Watatu walikamatwa kwa tuhuma za kuhifadhi wahamiaji haramu nchini huku Lita 271 za gongo , ngozi ya Mbwea, Bangi kilo Tatu na Makokoro 12 vilikamatwa wakati wa operesheni Kimbunga awamu ya Pili ikiwa katika wiki yake ya kwanza.  
Wakati huo huo, Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera imejipanga kukabiliana na tatizo la wahamiaji haramu ili kuhakikisha kuwa tatizo hilo linafikia mwisho wake na kuwapa nafasi wananchi kufanya shughuli zao za kijamii na kimaendeleo bila ya hofu ya kufanyiwa uhalifu na wahamiaji haramu.
Mkuu wa Wilaya ya Karagwe Bi Dari Rwegasira amewaambia          Maafisa Tarafa na Watendaji wa Kata aliokutana nao katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe, mwishoni mwa wiki iiliyopita kuwa kuanzia sasa kila kiongozi, kuanzia ngazi ya Kiijiji/Mtaa, Kata, Tarafa na Wilaya, atawajibika kwa jinsi anavyoshughulikia kumaliza tatizo la wahamiaji haramu katika eneo lake.
Wilaya ya Karagwe ni moja ya wilaya zenye tatizo sugu la wahamiaji haramu ambao wanatuhumiwa kuwanyanyasa wananchi katika baadhi ya maeneo ya Wilaya hiyo, kwa kuendesha vitendo vya wizi wa mifugo, kuvamia maeneo ya kilimo, na pia kuchochea uhalifu wa unyang’anyi wa kutumia silaha na kusababisha mauaji.
Wahamiaji hao haramu wanashutumiwa kufanya baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Karagwe yasipitike kwa urahisi, mojawapo ikiwa ni eneo la msitu wa Kimisi, ambapo eneo hili limekuwa na matukio mengi ya ujambazi wa kutumia silaha na wananchi kuvamiwa na kuibiwa mali zao na hata wengine wakipoteza maisha katika matukio hayo.
Maazimio kadhaa yalitolewa katika kikao hicho kati ya Mkuu wa Wilaya ya Karagwe na Watendaji Wakuu wa Wilaya hiyo, ikiwa ni pamoja na kuwa:
·         Viongozi kuanzia ngazi ya Kijiji/Kitongoji, Kata hadi Tarafa kutia saini mkataba wa kushughulikia wahamiaji haramu, majambazi wa kutumia silaha na wafadhili wao, mifugo haramu inayoingia nchini kutoka nchi jirani pamoja na vitendo vyote vya uhalifu katika maeneo wanayoyaongoza.
·         Kiongozi yoyote wa Kijiji, Kata au Tarafa atakayeshindwa kushughulikia wahamiaji haramu walioko katika eneo lake atawajibishwa.
·         Wahamiaji wote haramu ambao bado wapo katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo wasakwe na kurejeshwa kwao mara moja.
·         Msako uanzishwe mara moja kuwasaka wahamiaji haramu wote ambao wamejificha katika maeneo ya misitu na ranchi za mifugo zilizoko katika wilaya hiyo kwa kuvishirikisha vyombo vyote vya Utawala na vya Ulinzi na Usalama vilivyoko katika Wilaya hiyo.
·         Kila kijiji kiwe na takwimu sahihi za wageni waliopo katika maeneo yao.
·         Wahamiaji haramu wote wanaorejeshwa kwao wasipewe nafasi ya kurudi tena nchini na mwananchi yoyote atakayebainika kuwapokea au kuwasaidia kurejea  atolewe taarifa haraka ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake.
·         Vibali vyote vya Ukazi vilivyotolewa kwa wageni mbalimbali sasa vitakaguliwa upya ili kuhakiki uhalali wake.

Imeandaliwa na: 
Timu ya Habari ya Operesheni Kimbunga

Septemba30,2013

Madereva wakorofi waonywa

MKUU wa Mkoa wa Kagera, Kanali Mstaafu, Fabian Massawe, amewaonya madereva wa vyombo vya moto mkoani hapa kujiepusha na uvunjaji wa sheria za barabarani.
Amesema madereva lazima watii sheria za barabarani bila shuruti, na kwamba serikali haitasita kuwakamata wanaovunja sheria.
Kanali Massawe alitoa onyo hilo juzi wakati wa sherehe za maadhimisho ya wiki ya usalama barabarani, ambayo kimkoa ilifanyika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Massawe ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo, ambayo kitaifa yalifanyika jijijni Mwanza, alisema lengo la kuwepo maadhimisho hayo ni kuielimisha jamii juu ya matumizi ya barabara na sheria za nchi.
“Ajali za barabarani zinaathiri sana maisha ya wananchi wetu. Kwa hiyo natoa onyo kwa madereva wote kuzingatia sheria,” alisema.
Alisema jamii kutojua vizuri sheria zikiwemo za barabarani, kimekuwa chanzo kikubwa cha ukiukwaji wa sheria na kutokea ajali ambazo nyingi husababisha vifo.
Aliwaomba watembea kwa miguu na waendesha vyombo vya moto kuwa makini na kuzingatia sheria za barabarani, kani itasaidia kupunguza ajali.
Chanzo: Tanzania Daima

CAG KUKAGUA OFISI YA MEYA BUKOBA

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Bw. Ludovick Utouh, amesema ofisi yake ipo mbioni kwenda mjini Bukoba, mkoani Kagera, ili kufanya ukaguzi wa mahesabu katika Ofisi ya Meya na kutoa ripoti yenye uhakika.

  Bw. Utouh aliyasema hayo Dar es Salaam jana katika mafunzo yaliyoshirikisha Wahariri na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari ili kuwajengea uwezo wa kuripoti taarifa za ofisi hiyo.
  Alisema ukaguzi wanaokwenda kuufanya mjini Bukoba, hautokani na matakwa ya Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Nape Nnauye; bali ni ombi maalumu lililotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu. 

  Aliongeza kuwa, kumekuwa na taarifa za upotoshaji ambazo zimekuwa zikifanywa na baadhi ya makundi ambayo hayana nia njema na ofisi hiyo, hivyo ni vyema ikaeleweka kuwa, ukaguzi huo umezingatia agizo la Waziri Mkuu. 

 "Ofisi yangu inafanya kazi kikatiba si kwa matakwa ya chama chochote cha siasa, ukaguzi maalumu ambao utafanyika mjini Bukoba, utaanza wiki ijayo...ni jukumu la vyombo vya habari kuwa waangalifu wanaporipoti taarifa hizi.
"Wananchi wa Bukoba wasiwe na wasiwasi, tunakwenda huko lakini hatutaki chai ya mtu labda usafiri ambao upo kisheria kwa ajili ya ukaguzi wa miradi yenye utata iweze kufikiwa na kupatikana taarifa sahihi," alisema. 

  Bw. Utouh alisema uwajibikaji na uwazi ni mambo yasiyoweza kupatikana katika mfumo wa kuficha taarifa za utekelezaji wa mipango mbalimbali ya Serikali. 

  Alisema mahali ambapo habari inafichwa, lazima patatokea mvutano, kutoaminiana na hatimaye wananchi kuona Serikali yao ndiyo chanzo cha matatizo hivyo ni muhimu haki ya kikatiba kwa wananchi kupashwa habari ikazingatiwa. 

  Alitumia fursa hiyo kuvitaka vyombo vya habari nchini k u p u n g u z a u p o t o s h a j i n a kuelimisha jamii ipasavyo ili kusaidia makundi mbalimbali kuzielewa vizuri ripoti za CAG ili kuzuia machafuko yasiyo na lazima nchini. 

 "Madhara ya kuripoti taarifa za upotoshaji na mipaka ambayo inahitajika ni makubwa kwa jamii ...tunahitaji kufikiria masuala mazito yanayokwamisha kufikia malengo yetu, hivyo ni muhimu kuacha kutoa taarifa zisizo sahihi," alisema 

Chanzo: Majira



Zana haramu 9,000 zateketezwa

SERIKALI kupitia Idara ya Uvuvi mkoani Kagera, imekamata na kuteketeza kwa moto zana haramu 9,809 zilizokuwa zikitumika kwenye uvuvi ndani ya Ziwa Victoria.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Bukoba, Ofisa Mfawidhi wa Uvuvi na Doria Mkoani Kagera, Apolinary Kyojo alisema zana hizo zilikamatwa kutokana na msako maalumu wa kushitukizwa ndani ya Ziwa Victoria.
Alisema msako huo wenye lengo la kupambana na uvuvi haramu ndani ya ziwa hilo ulifanyika kati ya Juni na Agosti mwaka huu.
"Serikali inaendelea kupambana na watu wanaoshiriki uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria. Kati ya Juni na Agosti mwaka huu, tulikamata zana haramu 9,809. kwenye msako wa kushtukiza,” alisema.
Alizitaja zana zilizokamatwa kuwa ni nyavu zenye matundu madogo zipatazo 7,000, nyavu aina ya timba 2,700, makokoro yenye urefu wa zaidi  ya mita 110,000, vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh 750,000.
Kwa mujibu wa Kyojo katika kutekeleza misako ya namna hiyo, idara yake inakabiliwa na changamoto ya kukosa ushirikiano kutoka kwa baadhi ya viongozi wa vijiji, kata na hata wasimamizi wa rasiliamali za Ziwa Victoria (BMU).
Chanzo: Tanzania Daima


Wafugaji wauawa kinyama



 WAFUGAJI wawili wameuawa kinyama kwa kukatwa mapanga na kuchomwa mikuki na wananchi, huku ng'ombe wapatao 12 nao wakiuawa katika Kijiji cha Kasulo wilayani Ngara, Mkoa wa Kagera.
Chanzo cha mauaji hayo kinadaiwa kuwa ni uhasama wa muda mrefu kati ya wananchi na wafugaji hao wanaodaiwa kuingiza mifugo kijijini humo bila ridhaa ya serikali ya kijiji.
Tukio hilo lilitokea Septemba 19 mwaka huu, saa 11:00 jioni na kwamba ng'ombe waliouawa kwa kuchomwa mikuki na kukatwa mapanga, nyama zake zilichukuliwa na wanawake kwa ajili ya kitoweo.
Akithibitisha tukio hilo, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ngoma 'B' yalipotokea mauaji hayo, Simeon Nzakaya alilaani kitendo cha wananchi kujichukulia sheria mkononi na kuwataja waliouawa kuwa ni Ngabo Godfrey (24) na mwingine ambaye bado hajatambulika jina lake.
Alisema kuwa miili ya marehemu hao ilipatikana Septemba 20, na watu wanane wanashikiliwa na vyombo vya usalama kwa mahojiano zaidi kuhusiana na mauaji hayo.
Hata hivyo, taarifa zinadai kwamba baadhi ya mamlaka zinazolalamikiwa ni pamoja ni Idara ya Uhamiaji Wilaya, Mifugo na Halmashauri ya Wilaya kupitia kitengo cha sheria kwa kushindwa kuchukua hatua mara baada ya kuombwa kuingilia kati mambo ya uvamizi wa wafugaji.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kasulo, Yusufu Katula alithibitisha kuwepo kwa mauaji hayo pamoja na kulaani kitendo hicho.
"Mgogoro huo unafukuta kutokana na idara husika kutochukua hatua mapema. Hii inachangia kutokea mauaji kama haya, na hatua za haraka zisipochukuliwa yanaweza kutokea mapigano makali kati ya wanakijiji na wafugaji wanaoingia kinyemela,"alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Costantine Kanyasu alionya kuwa matukio kama hayo hayaruhusiwi kutokea katika jamii, na aliahidi ofisi yake kuyafanyia kazi malalamiko yote yanayotolewa kwa baadhi ya mamlaka.
"Ni kweli baadhi ya mamlaka za serikali zinalalamikiwa sana na wananchi. Na sasa nitakachokifanya ni kuchukua hatua za haraka kuhakikisha tukio kama hilo halitokei tena," alisema.
Chanzo: Tanzania Daima



ABELA KIBIRA: BINTI WA KIHAYA ANAYETIKISA AMERICA KIMUZIKI

Mkoa wa Kagera umebarikiwa kuwa na uwakilishi mzuri katika tasnia mbalimbali ndani na nje ya nchi, akina Rweyemamu wanazidi kupasua anga! mfano mzuri ni Mwanamuziki wa kike Abela ambaye ni mzaliwa wa Bukoba Mkoani Kagera anayepeperusha vyema bendera ya Tanzania kimziki huko Amerika anakoishi na kufanya kazi zake za muziki.

Abela Kibira alizaliwa Septemba 22 mwaka 1989 akiwa mtoto wa kwanza katika familia ya Mtanzania Josiah Kibira mzaliwa wa Bukoba Kagera, Tanzania na Mmarekani, Mrs Josiah Kibira.

Mchanganyiko huo wa tamaduni mbili kwa binti huyo ambaye ana kipaji cha utunzi na uimbaji, umemfanya kujimarisha na kujijengea jina katika muziki kutokana na aina ya muziki na manjonjo anayoyafanya katika mzuiki wake kupendwa.

Abela ni mzaliwa wa Bukoba, Tanzania lakini kwa sasa anaishi Minneapolis, Marekani. Binti huyu anasauti nzuri, ya kipekee na ya kuvutia jambo ambalo nyimbo zake nyingi zimekuwa zikipendwa sana

Onyesho lake la kwanza Binti huyu alilifanya kanisani na ndipo kipaji chache kilipojifunua machoni mwa watu wengi na hivyo kuendelea kuimba katika matamasha mbalimbali shuleni na matamasha maalumu.

Abela amekulia katika mji wa Wayzata, Minnesota na alipendwa kutokana na kuwa na uwezo wa ajabu katika kuimba kwaya na matamasha ya pamoja wakati akiwa katika masomo yake ya sekondari na chuo.

Mwaka 2003 baba yake mzazi Mr. Josiah Kibira alimshirikisha katika filamu yake aliyoiita Bongoland, ambapo Abela alitunga wimbo wa kusindikiza filamu hiyo (soundtrack) jambo lililomuongezea uwezo na umaarufu kwa mashabiki Amerika, Afrika na maeneo mengi ulimwenguni.

Abela ambaye bado binti kigoli anayejitambua amekuwa akiiimba na kujifua utumiaji wa sauti takriban maisha yake yote lakini kwa sasa amejikita zaidi katika utunzi na utengenezaji wa nyimbo za Hip Hop, Reggae na ni mzuri katika aina tofauti tofauti za muziki.

Abela hana shida juu ya kufanya collabo na wasanii wa Kitanzania na Africa kwa ujumla kwa hiyo kama unapenda kumshirikisha kazi ni kwako! Kwa sasa anatamba na video ya wimbo wake alioutoa mwishoni mwa mwaka jana unaoitwa Ball & Chain.

Kabla ya hapo ametamba na nyimbo nyingi zikiwemo Rolling Stone, Someone like you na Hey Ya.
Imeandaliwa na Dotto Kahindi

Operesheni Kimbunga yanasa wahamiaji haramu 1,851


HATIMAYE operesheni ya kuwasaka wahamiaji haramu nchini, iliyopewa jina la Kimbunga, imeanza juzi huku watu 1,851 wakikamatwa. Hatua hiyo, imetokana na agizo la Rais Jakaya Kikwete la kuwataka watu wanaomiliki silaha na kuishi nchini kinyume cha sheria, kuondoka wenyewe kwa hiari yao kabla vyombo vya dola havijaanza kazi ya kuwasaka.

Operesheni hiyo inayovishirikisha vyombo vyote vya dola, imeanza katika Mikoa ya Geita, Kagera na Kigoma.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali mstaafu, Fabian Massawe, alisema hadi jana wahamiaji haramu 1,851 wamekamatwa wakati 11,601 wameondoka kwa hiari yao.

Alisema operesheni hiyo haitamuacha mhamiaji haramu ndani ya mikoa hiyo.

Alisema licha ya wahamiaji 11,601 kuondoka wenyewe, Serikali imelenga wahamiaji 52,053 ambao bado wapo katika mikoa hiyo.

Alisema tangu Rais Jakaya Kikwete alipotoa agizo la wahamiaji haramu kuondoka kwa hiari, bunduki 65 zikiwamo Sub Machine Gun (SMG) tatu, ShortGun 10 na magobole 52 zilisalimishwa.

Naye, Mkuu wa Operesheni Msaidizi wa Jeshi la Polisi, Simon Sirro, alisema vyombo vyote vya dola vinaendelea na kazi ya kuwasaka wahamiaji.

Aliwatahadharisha wananchi mkoani Kagera kujihadhari na kuuziwa mali yoyote kutoka kwa mtu yeyote anayehamishwa bila maandishi kwa ajili ya kuepuka kukamatwa na kuhusishwa kushirikiana na wahamiaji hao.

Alisema walikamata ng’ombe 1,765, sare na vifaa mbalimbali vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). 


 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa