NAIBU WAZIRI NDUNGULILE ACHANGISHA ZAIDI YA MILIONI 17 KUJENGA NYUMBA ZA WATUMISHI KITUO CHA WAZEE KIILIMA MKOANI KAGERA

 Dk. Faustine Ndungulile Kulia Akiongea na Mzee Mmojawapo Anaishi Katika Kituo cha Wazee Kiilima
 Naibu Waziri wa Afya  Dk. Faustine Ndungulile Akionesha Mfano wa Kufyatua Tofali Ili Nyumba za Watumishi Zijengwe Katika Kituo cha Wazee Kiilima
 Mkuu wa Mkoa Kagera Mhe. Kijuu (Kulia) Akipokea Ahadi ya Vifaa Vilivyohaidiwa na Redcross Wakati wa Harambee Mabati 20, Blanketi 20 na Vyandarua
 Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Kijuu Aliyesimama Kulia Akitoa Taarifa kwa Naibu Waziri wa Afya Dk. Ndungulile
 Naibu Waziri wa Afya  Dk. Faustine Ndungulile Akionesha Mfano wa Kufyatua Tofali Ili Nyumba za Watumishi Zijengwe Katika Kituo cha Wazee Kiilima
Nyumba za Watumishi (Kulia) Zinazotakiwa Kujengwa Upya Kwasababu ya Uchakavu Katika Kituo cha Wazee Kiilima Zikikaguliwa na Waziri Ummy Mwalimu
Na: Sylvester Raphael
Naibu Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia  Wazee na Watoto Dk. Faustine Ndungulile afanikisha  kupatikana kwa zaidi ya  shilingi milioni 17 kwenye harambee ya kuchangia ujenzi wa  Nyumba ya Watumishi katika Kituo cha Wazee Kiilima Kata ya Nyakato Wilayani Bukoba Mkoani Kagera.

Katika Harambee hiyo iliyofanyika Februari 22, 2018 katika Kituo cha Wazee Kiilima Dk. Ndungulile akiwa  Mgeni Rasmi alichangisha fedha taslimu milioni 7,000,000/= na kiasi cha shilingi milioni 11 zikiwa ahadi kutoka kwa wadau mbalimbali pamoja ahadi za vifaa kama magodoro, saruji,  baiskeli za wazee na mabati.

Katika hotuba yake kwa wananchi na wadau mbalimbali waliohudhuria harambee hiyo Naibu Waziri Dk. Ndungulile aliwasisitiza wananchi kuwa na moyo wa kujitolea kuchangia kituo hicho ili watumishi wanaowatunza wazee wapate mazingira mazuri ya kuishi baada ya kufanya kazi yao ya kuwahudumia wazee hao.

“Serikali itaendelea kuwaunga  mkono wananchi kwa kuleta fedha katika kituo hiki ili kikamilike ujenzi wake na Wazee wetu  waweze kuhudumiwa na watumishi  ambao watawaza ni wapi pa kuishi au kukaa salama mara baada ya kufanya kazi yao ya kuwahudumia Wazee wetu,” Alisisitiza Dk. Ndungulile.
Kituo cha Kutunza Wazee Kiilima ni kituo cha Serikali kilichopo chini ya Wizara ya  Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia  Wazee na Watoto.  Kituo Hicho kilijengwa upya na Serikali baada ya kuathiriwa na Tetemeko la Ardhi lililotokea Septemba 10, 2016 Mkoani Kagera.

Majengo yaliyojengwa upya na Serikali ni pamoja na Mabweni mawili ya Wanaume na Wanawake, Jiko, stoo ya kutunzia chakula, Sehemu ya kulia chakula, sehemu ya kupumzikia wazee,  vyoo viwili vya wanawake na wanaume. Changamoto iliyokuwa imebaki ni nyumba za watumishi ambazo kwa sasa zina hali mbaya ya uchakavu na hazistahili tena kuishi watu.

Fedha zilizopatikana zinatarajiwa kujenga nyumba mbili za watumishi (Two in One) ili kutatua changamoto ya watumishi wanaoishi na kufanya kazi ya kuwahudumia wazee ili wapate mahali salama pa kuishi na kutimiza wajibu wao kikamilifu bila kuwa na changamoto za sehemu za kuishi.
Katika Hatua nyingine Naibu Waziri Dk. Ndungulile alimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu Salum M. Kijuu kwa juhudi zake za kuipatia Bohari ya Dawa (MSD)  kiwanja cha kujenga Bohari ya dawa katika Manispaa ya Bukoba na Mkoani Kagera ili kurahisisha upatikanaji wa dawa zote hapa Kagera.

Pia Dk. Ndungulile alimuomba Mkuu wa Mkoa kuhamasisha wananchi kuitikia wito wa kuwapeleka watoto wa kike miaka 4 hadi 9 kwenda kwenye vituo vitakavyokuwa vimepangwa kupata chanjo ya kansa ya shingo na uzazi kwani imeonekana kuwa kuna ongezeko kubwa la Kansa ya Shingo na uzazi katika mkoa wa Kagera.

Akimshukuru Naibu Waziri kwa kuamua kufanya ziara ya kukagua shughuli za afya Mkoani Kagera Mkuu wa Mkoa Kijuu aliomba Wizara ya Afya kuangalia upya tatizo la ugonjwa wa Malaria katika Mkoa wa Kagera kwani pamoja na juhudi zote zinazofanyika laikini kiwango cha ugonjwa huo kinazidi kupanda ambapo Naibu Waziri Dk. Ndungulile alisema tayari Wizara imeliona hilo na linafanyiwa kazi.

Naibu Waziri Dk. Ndungulile akiwa Mkoani hapa katika ziara yake ya siku mbili alivitembelea pia vituo vya Afya Kabyaile Wilayani Missenyi, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera, Kituo cha Afya Kaigara na Kituo cha Afya Kimeya Wilayani Muleba ili kukagua huduma za Afya zinavyotolewa kwa wananchi na kuongea na watumishi katika maeneo hayo.

MAAFISA HABARI NA TEHAMA WANOLEWA KUZIBORESHA TOVUTI ZA MIKOA NA HALMASAHURI ILI KUWA KITOVU CHA HABARI KWA WANANCHI



Maafisa Habari na Tehama wakiwa katika mafunzo juu ya namna bora ya uandishi wa habari za Tovuti.

Na: Sylvester Raphael
Serikali kupitia Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa kushirikiana na Mradi wa kuboresha Mifumo ya Serikali PS3 waendesha mafunzo ya siku nne juu ya namna bora ya uandishi wa habari za Tovuti za Serikali kwa Maafisa Habari na Maafisa Tehama wa Mikoa na Halmashauri zote Tanzania Bara.

Kutokana na umuhimu wa Tovuti za Serikali hasa katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa nchini kuwa chanzo kikuu cha habari kwa wananchi Serikali kwa kushirikiana na Mradi wa Maboresho ya Mifumo ya Serikali PS3 waliona kuna umuhimu wa kuendesha mafunzo juu ya uandishi bora wa habari katika Tovuti za Mikoa na Halmashauri  ili wananchi wapate habari muhimu na zenye uhakika juu ya maendeleo yao.

Kwakuwa siyo Mikoa yote na Halmashauri zote nchini zina Maafisa Habari na kazi za Habari zinafanywa na baadhi ya watu kama Maafisa Tehama, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Mradi wa kuboresha Mifumo ya Serikali PS3 wameona kuna umuhimu wa Maafisa hao kupitishwa katika mafunzo ya namna bora ya uandishi wa habari za Tovuti kwa wananchi ili kuwa na uelewa wa pamoja na aina moja ya uandishi (House Style)

Katika Mafunzo hayo mada mbalimbali zihusuzo Uandishi wa Habari zinawasilishwa na wataalamu waliobobea katika mambo ya habari na uandishi wa habari pia ambapo mada hizo ni pamoja na Malengo ya Mwongoz wa  Tovuti, Sheria na Maadili ya Habari, Upigaji wa Picha za Kidijitali, Mbinu za Mahojiano, Uandishi wa Aya, Habari katika mfumo wa 5Ws + H (Piramidi iliyogeuka).

Mafunzo ya namna bora ya uandishi wa habari za Tovuti za Serikali yanaendeshwa katika makundi ya mikoa mbalimbali ambapo mikoa ya Geita, Tabora Kigoma na Kagera mafunzo hayo yanafanyika katika Mkoa wa Kagera Bukoba Hotel Manispaa ya Bukoba aidha, mafunzo hayo yalianza Februari 19 na yanatarajia kukamilika Februari 22, 2018.

Matarajio ya Serikali baada ya mafunzo hayo ni kuona Tovuti za Serikali zinakuwa kitovu cha habari kwa wananchi na si ilimradi habari tu bali habari zenye weledi, ukweli, uhakika na kuisemea Serikali inafanya nini katika kuwaletea wananchi maendeleo. Pia katika Tovuti hizo kuwa na taarifa muhimu mbalimbali zinazohusu taasisi husika mfano Mkoa au Halmashauri husika.
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa