8 WASIMAMISHWA KAZI BUKOBA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Bukoba, limewasimamisha watumishi wanane kutokana na ufisadi wa Sh milioni 851 zilizotolewa na Serikali pamoja na wafadhili kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella ameagiza kuchukuliwa hatua za kijinai kwa watendaji wote waliohusika. Mongella alishtushwa na taarifa ya tume iliyoundwa na uongozi wa mkoa huo kuchunguza matumizi ya fedha hizo kwa ajili ya maendeleo ya halmashauri hiyo.
Kutokana na hali hiyo, Baraza la Madiwani la halmashauri hiyo limekaa kikao cha dharura na kuwasimamisha watumishi hao ili kupisha uchunguzi. Waliosimamishwa ni aliyekuwa Mganga Mkuu (DMO), Hamza Mgula kabla ya kuhamishiwa Manispaa ya Bukoba, Idara ya Fedha ni Mweka Hazina, Jonathan Katunzi na Selialisi Mtalemwa, Kitengo cha Ujenzi; Robert Massoro na Deus Bizibu, Ofisa Mipango na Ofisa Elimu Sekondari, Lucas Mzungu, Idara ya Mipango, Mustapha Sabuni na Idara ya Mifugo, Dk Kisanga Makigo.
Hali hiyo ilikuja wakati Mwenyekiti wa Tume ya watu sita, Wambura Sabora kutoa taarifa katika kikao maalumu cha madiwani, watumishi wa halmashauri hiyo, wakuu wa idara kutoka mkoani na mkuu huyo wa mkoa juu ya waliyobaini ndani ya siku nne walizofanya ukaguzi na uchunguzi ambapo walidai kubaini madudu.
“Katika uchunguzi tulibaini kuwa fedha kutoka Basket Fund milioni 307 zilizotolewa na Serikali 2011/2012 kwa ajili ya kununulia dawa katika hospitali na vituo vya afya zilihamishwa na kutumika tofauti na malengo bila kufuata taratibu zinazostahili huku milioni 200 za Mfuko wa Barabara zilizotolewa 2014 kwa ombi maalumu ambazo zilizotolea kwa mfumo wa kibajeti hazikutumika kama ilivyokusudiwa na badala yake zilihamishiwa sehemu nyingine ikiwemo matumzi ya ofisi,” Wambura alisema.
Alitaja fedha nyingine kuwa ni Sh milioni 168 za Mfuko wa Jimbo ambazo pia zimetumika katika shughuli nyingine, bila idhini ya kikao chochote wala nyaraka inayoonesha kuhamishwa kwa fedha hiyo jambo ambalo ni kosa kisheria kwani ni matumizi yanayotia shaka.
Baada ya Mkuu wa Mkoa kupata taarifa hiyo, aliwataka Mweka Hazina, John Katunzi kutoa maelezo, na akakiri kuwepo kwa upungufu huo huku akibainisha walibadilisha matumizi ya fedha hiyo baada ya kukaa na Mkurugenzi wakati huo Glades Ndyamvunye.
Inaelezwa kuwa walipanga kurudisha fedha hizo lakini hadi sasa hazijarudishwa. Pamoja na hayo, alimwagiza Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) Mkoa, Joseph Mwaiswelo na Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo kuwachukulia hatua zaidi watuhumiwa kwa yale yatakayobainika kuwa ya kijinai.
CHANZO ; HABARI LEO.

FLAVIANA MATATA FOUNDATION YATOA MSAADA SHULE YA MSINGI

fmf msinune Flaviana Matata akikabidhi mabegi ya shule kwa watoto wa shule ya Msingi ya Msinune ambapo ameteuliwa kama mlezi wa shule hiyo kwa mwaka wa tatu sasa.

Mkuu wa shule Bukoba avuliwa cheo kwa kutoza michango

Mkuu wa shule Bukoba avuliwa cheo kwa kutoza michango
Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Nassoro Mnambila
MKUU wa Shule ya Sekondari ya Bilele ya Mjini Bukoba, mkoani Kagera, Siasa Phocus amevuliwa madaraka kwa madai ya kuendelea na msimamo wa kutaka wazazi wenye watoto shuleni hapo, waendelee kutoa michango kinyume na agizo la serikali.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Nassoro Mnambila aliliambia gazeti hili jana mjini hapa kwamba mwalimu huyo alishapewa utaratibu wa kuzingatia sera ya utoaji elimu msingi bure, lakini alikaidi.

“Kwa mamlaka niliyonayo, nachukua hatua hii kwa kumvua mamlaka mkuu wa shule Bilele kutokana na kushindwa kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na serikali…,” alisema Mnambila.

Alisema mwalimu huyo aliendelea na msimamo wa kuwaambia baadhi ya wazazi waliofika kuuliza utaratibu wa michango, kwamba hana taarifa na miongozo ya serikali, akiwasisitiza kila mzazi kutimiza mahitaji yaliyopo kwenye fomu ya mwanafunzi.

“Mwalimu huyo aliendelea kutoa fomu kwa kila mwanafunzi iliyoainisha kila mahitaji kama ilivyokuwa hapo awali (miaka ya nyuma) huku akitaka michango ya madawati, karatasi za kuchapia mitihani na mlolongo wa gharama nyingine nyingi,”alisema Katibu Tawala.

Michango mingine ambayo wanafunzi wa sekondari wamekuwa wakitozwa kila mwaka ni ya fyekeo, ndoo, jembe, uji, chakula cha mchana na uzio.

Katibu tawala alionya walimu wakuu na wakuu wa shule, kuzingatia na kutekeleza sera ya utoaji wa elimu msingi bure, kama ilivyo kwenye taratibu za miongozo iliyotolewa kwao katika idara ya elimu.

Fedha zafika mikoani

Wakati huo huo, mikoa mbalimbali imethibitisha kupokea fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mpango wa elimu bure. Jumla ya Sh bilioni 18.77 zimetolewa na serikali kwa ajili ya shule zote za umma nchini.

Miongoni mwa mikoa iliyothibitisha kwa waandishi wa habari kupokea fedha zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kutekeleza elimu msingi bila malipo ni pamoja na Kagera, Morogo, Rukwa na Mwanza.

Ofisa Elimu wa Mkoa wa Kagera, Aloyce Kamamba alisema wamepatiwa jumla ya Sh 810,157,000 ambazo zimeshaelekezwa kwenye akaunti za shule zilizoko mkoani humo, ambapo za msingi ni 888 na sekondari 190. Kati ya hizo, 17 ni sekondari za bweni. Kiasi hicho kimetolewa na serikali kwa ajili ya kugharimia huduma mbalimbali ikiwemo chakula.

Mkoani Rukwa, Mkuu wa Mkoa, Magalula Said Magalula alisema wamepokea Sh milioni 336 ambapo Sh 143,859,000 zimepelekwa kwenye shule za msingi 360 na kiasi kilichobaki, kimepelekwa shule 105 za sekondari. Kwa mujibu wa Magalula, fedha hizo ni kwa ajili ya mwezi huu kwani kila mwezi serikali itakuwa ikitoa fedha kwa ajili ya mpango huo.

Mkuu wa Shule ya Sekondari Kalangasa Manispaa ya Sumbawanga, Gabriel Hokororo, alikiri shule yake kupokea Sh milioni 1.4 kwa ajili ya Januari mwaka huu. Katika Mkoa wa Morogoro, Katibu Tawala Msaidizi wa mkoa huo anayeshughulikia elimu, Wariambora Nkya, alithibitisha kupokea Sh milioni 724.7 kwa ajili ya shule 846 za msingi na 179 za sekondari za bweni na kutwa.

Mkoa mwingine uliothibitisha kupokea fedha hizo ni Mwanza wenye shule za sekondari 197, ambazo zimepewa Sh 642,648,000 kwa ajili ya fidia ya ada za kutwa na bweni na chakula kwa shule za bweni. Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo alisema upande wa Shule za Msingi, zipo 850 ambazo zimepokea Sh milioni 356,728,000.

Alisema hadi Desemba 30 mwaka jana, shule zote zilishawekewa fedha kwenye akaunti zake.

Wahadharishwa matumizi

Walimu wakuu, wakuu wa shule, bodi wamesisitizwa juu ya matumizi sahihi ya fedha hizo na wakati huo huo kuzingatia maelekezo ya serikali ya kuhakikisha elimu msingi inatolewa bure.

Licha ya wakuu wa mikoa na idara ya elimu kuhadharisha juu ya hilo, pia Wizara ya Fedha na Mipango hivi karibuni, ilionya wakuu wa shule za msingi na Sekondari watakaotumia ovyo fedha hizo zilizotolewa na serikali kutoa elimu bure, ikisema atakayebainika kuzitumia isivyo, atashughulikiwa.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango iliwataka walimu katika kuhakikisha fedha hizo zinatumika ipasavyo, waweke wazi fedha walizopokea kutoka serikalini wananchi wafahamu alichopewa na matumizi yake.

Bodi za shule zimepewa kazi ya kuhakikisha zinasimamia matumizi na kutoa taarifa. Pia wakuu wa wilaya, mikoa na wakurugenzi wamepewa wajibu wa kusimamia fedha hizo Sh bilioni 14.7, ambazo kati yake, Sh bilioni tatu zimepelekwa katika vyombo vya usimamizi wa mitihani.


HABARI LEO

SERIKALI YATOA TAMKO KUHUSU MISAADA ILIYOKATALIWA‏ -NI PAMOJA NA ULE ALIOTOA MH. RWAKATALE (MB)

Na Magreth Kinabo –Maelezo


Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Mpoki Ulisubisya amesema misaada inayotolewa na watu mbalimbali kwa ajili ya kusaidia jamii ni lazima iwe imekidhi viwango vya ubora, hivyo haitakiwi kuangaliwa kwa vigezo vya dini, itikadi wala siasa.
 Kauli hiyo imetolewa leo na Katibu huyo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake baada kituo kimojwapo nchini kukataa misaada iliyotolewa na Mbunge wa Bukoba Mjini (Chadema), Wilfred Lwakatare wa Chama cha Wananchi(CUF), hivi karibuni.
 Dkt. Ulisubisya  alisema hivi karibuni gazeti moja la kila siku la hapa nchini liliripoti kwamba misaada iliyotolewa na Mbunge huyo, katika baadhi vituo afya Zahanati  kwa ajili ya wajawazito  kukataliwa.
“Serikali ina sera ya kusaidia jamii hususan misaada inayotolewa  kwenye huduma za afya, ambayo inakidhi viwango vya ubora kulingana Sheria , kanuni na taratibu za Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA),” alisema Katibu Mkuu huyo.  
Kwa mujibu wa chanzo kimoja cha habari kiliripoti kwamba baadhi ya wakuu wa vituo vya afya na zahanati katika Manispaa ya Bukoba, wamegoma kupokea misaada kwa ajili ya wajawazito uliotolewa na kwa madai ya kupewa maelekezo na Serikali.
Dkt. Ulisubisya aliwataka watendaji wa afya wa vituo hivyo kuwa wasiangalie misaada hiyo kwa misingi ya dini, itikadi na kisiasa.
Hata hivyo Katibu Mkuu huyo aliwataka watu mbalimbali wenye lengo la kutoa misaada katika vituo vya afya kuhakikisha kwamba imekidhi viwango viliyowekwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).
 Katika hatua nyingine aliyekuwa Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dkt. Donan Mmbando alikabidhi ofisi hiyo kwa Katibu Mkuu huyo mpya.

    

MISAADA YA MBUNGE LWAKATARE (CHADEMA ) YAKATALIWA HOSPITALINI


Baadhi ya wakuu wa vituo vya afya na zahanati katika Manispaa ya Bukoba, wamegoma kupokea misaada kwa ajili ya wajawazito uliotolewa na Mbunge wa Bukoba Mjini (Chadema), Wilfred Lwakatare kwa madai ya kupewa maelekezo na Serikali.
Mbunge huyo mwishoni mwa wiki alikuwa akisambaza vifaa tiba katika vituo vya afya na zahanati, lakini wasimamizi walikataa kuvipokea, huku wengine wakikimbia wakidai walipewa maelekezo na viongozi wao kutovipokea.
Katika hali ya kushangaza Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba, Richard Mihayo ambaye alikuwa katika msafara wa mbunge huyo alitoweka ghafla baada ya kufika Kituo cha Afya cha Zamzam, huku Kaimu mganga, Samwel Chaba akigoma kupokea vifaa hivyo.
Baada ya mkurugenzi kutoweka, mbunge huyo alilazimika kutelekeza vifaa hivyo kituoni hapo na kwenda Zahanati ya Kashai ambako Kaimu Msimamizi wa zahanati hiyo, Emmanel Luviga alikubali kuvipokea.
Katika Kituo cha Afya Rwamishenye vifaa hivyo vilipokewa na wauguzi waliogoma kuzungumza suala lolote.
Baada ya kufika Zahanati ya Kagemu, Msimamizi wake Glory Sailo aligoma kupokea vifaa kwa ajili ya mama wajawazito kwa madai ni maelekezo ya viongozi.
Hatua ya viongozi kuweka vikwazo kwenye upokeaji wa vifaa hivyo vyenye thamani ya zaidi ya Sh3 milioni ililalamikiwa na Lwakatare aliyedai aliandika barua manispaa na kutoa nakala hadi ngazi ya mkoa, lakini Mganga Mkuu wa manispaa hiyo, Dk Hamza Mgula alisema hajui lolote kuhusu suala hilo.
Akizungumzia suala hilo, Mihayo alisema kwa kawaida vifaa vya tiba ni lazima vikaguliwe na mganga mkuu wa manispaa ili kuthibitisha ubora, hivyo haviwezi kupelekwa bila kuthibitishwa.

CHANZO: MWANANCHI

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa