CAG AMBWAGA AMANI

Aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatory AmaniMAHAKAMA Kuu kanda ya Bukoba, imetupilia mbali kesi namba moja ya mwaka 2014, iliyofunguliwa na aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatory Amani dhidi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Amani alifungua kesi hiyo, akipinga ripoti ya ukaguzi uliyofanywa na CAG katika halmashauri hiyo Desemba mwaka jana, kuhusu utekelezwaji wa miradi ya maendeleo akidai kwamba alionewa.
Ripoti hiyo, iliyosomwa na aliyekuwa CAG, Ludovick Uttouh mbele ya Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri ilimtia hatiani Amani na aliyekuwa Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Hamis Kaputa kwamba waliendesha miradi hiyo kwa kukiuka utaratibu wa kutoshirikisha Baraza la Madiwani na wizara husika.
Katika hukumu yake juzi, Jaji G. J. Mjemmas, alisema kumshtaki CAG ni jambo linalowezekana lakini kwa suala hilo la kuhusu ripoti ya ukaguzi haiwezekani CAG kushtakiwa kwasababu alitumwa na Serikali kufanya kazi yake na imekamilika.
Jaji Mjemmas, aliagiza vyombo vingine vinavyohusika katika suala hilo, kuchukua hatua za haraka kutekeleza mapendekezo ya ripoti ya CAG na kusisitiza kwamba kesi hiyo haitaweza kuwepo kabisa huku Amani akitakiwa kulipa gharama zote za kesi.
Hii si mara ya kwanza kwa Amani kufungua kesi ya kujaribu kupigania umeya wake, ambao aliupoteza alipotangaza kujiuzulu muda mfupi baada ya CAG kuwasilisha ripoti yake, lakini baadaye akaibuka na kukana kujiuzulu.
Kwa sasa, Amani amefungua kesi katika Mahakama ya Wilaya ya Bukoba dhidi ya Mkurugenzi wa manispaa hiyo, akimtaka amruhusu aingie katika vikao vya Baraza la Madiwani akiwa mamlaka yake ya umeya na kurejeshewa haki zake zote za usafiri na mahitaji mengine.
Suala hilo, lilikataliwa na mkurugenzi akisema kuwa hamtambui kwa sababu kwa mujibu wa maelezo ya barua aliyopewa na serikali ili ampatie ina maana kwamba yeye si meya tena na hasa kwa kuzingatia tamko lake la kujiuzulu baada ya CAG kusoma ripoti yake.
Msimamo wa mkurugenzi huyo, ndio ulimlazimu Amani kupitia kwa mwanasheria wake kufungua shauri katika mahakama hiyo, ambayo juzi iliahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 2 mwaka huu.

RC: FAINI ZA MAKOSA BARABARANI ZIONGEZWE

MKUU wa Mkoa wa Kagera, Fabian Massawe ametaka sheria za usalama barabarani, ziangaliwe upya kwa lengo la kuongeza adhabu na faini kwa wanaosababisha ajali.
Akihutubia jana katika ufunguzi wa Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani mkoani Kagera, alisema sheria ya sasa imepitwa na wakati kutokana na kutoa adhabu ndogo jambo alilosema linawapa jeuri watu wanaosababisha ajali barabarani.
“Maana mtu akifanya kosa la kusababisha ajali, tena ameua mtu eti faini Shilingi elfu 20. Hii inawapa jeuri ya kuendelea kutenda makosa hayo,” alisema.
Alisema madereva hawajali kwa kuwa huchukulia kwamba watalipa faini hiyo ambayo ni ndogo. Alitoa mfano wa Australia, kwamba mtu akitenda kosa kama hilo katika nchi hiyo, hunyang’anywa leseni na haruhusiwi kuendesha gari milele.
Alisema haitoshi kwa polisi kila wakati kuorodhesha ajali zinazoendelea kutokea, ambazo sababu zake ziko ndani ya uwezo wao.
Alihimiza polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani, kufuata kanuni na maadili ya kazi yao. Alisema jambo la muhimu ni kutekeleza kwa vitendo majukumu yao na mikakati madhubuti, waliojiwekea kukabili ajali zinazogharimu uhai wa watu.
Katika risala yake, Kaimu Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabara Mkoa wa Kagera, Peter Magayane , alisema ajali nyingi zinatokana na makosa ya kibinadamu, ambayo ni mwendo mkali, ulevi, uchovu na usingizi.
Alisema makosa mengine ni ya kimazingira, kama vile mteremko mkali uliopo eneo la K 9 wilayani Ngara mkoani Kagera
Chanzo;Habari leo

‘USHIRIKA MULEBA WAPINDISHA SHERIA YA UCHAGUZI’

 
BAADHI ya wakulima wa chama cha ushirika cha Kamachumu kilichopo Wilayani Muleba Mkoani Kagera wamedai kuwa uchaguzi wa kuwachagua wajumbe wa bodi na mwenyekiti wa chama hicho uliofanyika wiki iliyopita ulikuwa batili kutokana na sheria namba sita ya ushirika kukiukwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mkutano kabla ya kufanyika kwa uchaguzi huo mbele ya Afisa ushirika wilayani Missenyi Humphery Kachelele, aliyekuwa msimamizi wa uchaguzi huo walisema sheria hiyo inakataza mwanachama ambaye ni kiongozi wa siasa kugombea nafasi yoyote katika ushirika hadi atakapojiuzuru wadhifa wake.
Diocles Rutabana alisema sheria hiyo inakataza wanasiasa kugombea nafasi za uongozi katika ushirika lakini cha ajabu waliochukuwa fomu ya kugombea nyadhifa hizo (majina yanahifadhiwa) ni viongozi wa chama cha siasa kikongwe nchini.
Alisema kutokana na hayo inaonyesha wazi kuwa uchaguzi huo ni batili kutokana na makao makuu kushindwa kusimamia vyema sheria hiyo na hata katika suala la ugawaji fomu.
Rutabana alidai kuwa mwenyekiti wao Superi Karugaba aliamua kuficha fomu hizo ili kumuwezesha kurudi katika nafasi yake pamoja na bodi yake huku ikiwanyima fursa wanachama waliokuwa na nia ya kuwania nyadhifa hizo.
“Viongozi wote waliokuwa madarakani walichukuwa fomu pamoja na mtu mmoja huku kiongozi wa juu wa ushirika akizificha fomu hizo ili wengine wasipate nafasi ya kugombea,” alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo wagombea waliochukua fomu walipita bila kupingwa kutokuwa na kukosa upinzani.
Akizungumza katika kikao hicho, Kachelele alisema yeye ndiye mtafsiriwa sheria hivyo hakuna mtu yeyote anayeweza kumshinikiza katika hilo.
Hata hivyo aliwauliza wagombea hao iwapo ni wanasiasa ambapo walikana madai hayo na kusema kuwa walishajiuzuru.
Alikwenda mbali zaidi na kutoa onyo kwa wanachama hao ya kuwa iwapo watasusia uchaguzi huo, atalazimika kuendelea na uchaguzi hata wakibaki wawili.
Naye mtendaji wa kijiji cha Kamachumu Lenard Anseremy, alisema kuwa ni mgombea mmoja aliyejiuzulu wadhifa wake lakini waliobaki walikidanganya kikao hicho kwani hadi sasa bado wanaendelea na shughuli zao.
Akizungumzia tuhuma za kuficha fomu Karugaba, alisema kuwa madai hayo hayana ukweli wowote kwa kuwa matangazo yalitolewa ya ugawaji wa fomu na hakuna wanachama waliofika kuchukua.
Kuhusu kuwania nafasi hiyo kwa miaka 30 pamoja na bodi yake wakiwa ni walewale, mwenyekiti huyo alisema kuwa suala hilo linapaswa kujibiwa na msimamizi wa uchaguzi huo
Chanzo:Tanzani Daima 

MWANAFUNZI AJIUA KWA SHUKA HOSPITALINI

 
KATIKA hali isiyotarajiwa, mwanafunzi wa Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Wavulana Ihungo Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera, Ezra Gerald (19), amejinyonga hadi kufa kwa kutumia shuka ya hospitali, alikokuwa amelazwa kwa kile kinachoeleza alikuwa anasumbuliwa na homa ya matumbo.
Hata hivyo, ujumbe ulioachwa na marehemu huyo unaonesha alichukua uamuzi huo, kutokana na kuchukizwa na uamuzi wa daktari aliyemhudumia wa kumlaza ili atibiwe ugonjwa ambao hakuwa anaumwa.
Aidha, katika ujumbe huo imeelezwa alichukizwa na kitendo cha kupotezewa muda hospitalini wakati wenzake wakiendelea na masomo.
Tukio hilo limethibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Gilles Muroto aliyesema mwanafunzi huo alijinyonga Septemba 16 mwaka huu saa moja asubuhi.
Alisema mwili wake uligundulika ukining’inia kwenye mti uliopo maeneo ya hospitali hiyo na alipopekuliwa katika mifuko ya suruali yake, zilionekana karatasi mbili, moja ikiwa na ujumbe uliosomeka;
“Haiwezekani binadamu kuhudumiwa kama mbwa, yaani nafika hospitali najieleza hali yangu halafu daktari ananiandikia kulazwa bila kupima, sasa sijui wanatibu nini?
“Kwa kweli siwezi kuvumilia wenzangu wanasoma halafu mimi nimekalishwa tu hapa hospitali bila kujua wananitibu nini, inaniuma sana mpaka nafikia hatua hii ya kujiondoa duniani kwa sababu naona watu wanachezea ndoto zangu, mimi siwezi kuona ndoto yangu inazimwa wakati natakiwa niwepo shuleni nikamilishe ndoto zangu “mjitahidi tukutane mbinguni “Respect My Family and Brother Henry.”
Kamanda Muroto amesema hakuna aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo, lakini polisi wanaendelea na uchunguzi.
Inaelezwa mwanafunzi huyo aliyetajwa kuwa ni mwenyeji wa mkoa wa Tabora, alilazwa hospitalini hapo tangu Septemba 11 mwaka huu.
Kwa mujibu wa Katibu wa Hospitali ya Mkoa wa Kagera, Benges Justus, tukio hilo lilitokea Septemba 16, mwaka huu, siku moja baada ya mgonjwa huyo kulazwa.
Alisema baada ya mwanafunzi huyo kupokelewa hospitalini hapo, alifanyiwa vipimo vyote vya kitabibu na kugundulika anasumbuliwa na malaria, ndipo akaanzishiwa tiba ya ugonjwa huo.
Chanzo;Habari Leo

RADI YAUA BABA, MAMA NA MTOTO

Kamanda wa Polisi mkoani Kagera,Henry Mwaibambe.
Watu watatu wa familia moja wamefariki dunia papo hapo baada ya kupigwa na radi wakiwa ndani ya nyumba yao katika kijiji cha Byeju Wilaya ya Missenyi mkoani Kagera.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Henry Mwaibambe, alisema tukio hilo lilitokea Agosti 24, mwaka huu majira ya usiku kufuatia mvua kubwa iliyonyesha usiku kucha.

Kamanda Mwaibambe aliwataja waliokufa katika tukio hilo la kusikitisha kuwa Daud Muonge (35) na mkewe, Fatuma Daud (24) pamoja na mtoto wao, Zaituni Daud, mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu.

Alisema katika tukio hilo, mtu mwingine, Sadam Daud (22), aliyekuwa mgeni wa familia hiyo, alijeruhiwa.

Wakati huo huo, Jeshi la Polisi mkoani Kagera, limekamata zana haramu za uvuvi ukiwamo mitumbwi inayofanya uvuvi kinyume cha taratibu, injini za boti na watuhumiwa 25 kutokana na msako mkali unaoendelea.

Kamanda Mwaibambe alisema msako uliowawezesha kukamatwa kwa zana hizo ulianza Mei, mwaka huu na unaendelea katika maeneo mbalimbali.

Alitaja zana zilizokamatwa ni injini za boti 10 zinazohofiwa zilipatikana isivyo halali kutokana na namba zake kufutwa, makokoro 38, mbao 1,378,  nyavu saba za kuvulia dagaa, nyavu zenye matundu chini ya sentimita sita 780    na   boti   16   zisizo   na usajili.

Alisema tayari nyavu haramu zilizokamatwa zimeteketezwa kwa moto na watuhumiwa wote waliokamatwa watafikishwa mahakamani wakati wowote baada ya  upelelezi kukamilika.
CHANZO: NIPASHE

NGARA KATIKA KASHFA YA UBADHIRIFU WA FEDHA

 
HALMASHAURI ya Wilaya ya Ngara inadaiwa kukumbwa na kashfa ya ubadhirifu wa fedha za umma katika miradi mitatu kwenye maeneo tofauti hali ambayo Kamati ya Utekelezaji ya Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Kagera imeamuru irudiwe na kukamilishwa.
Ubadhirifu huo uligundulika baada ya kamati hiyo kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo juzi kwa lengo la kutathmini na kujiridhisha utekelezaji wa Ilani ya chama ya mwaka 2010.
Pia ililenga kujiridhisha kama fedha inayotolewa na serikali ya chama hicho inafanya shughuli zilizokusudiwa na kwa viwango.
Ikiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kagera Costansia Buhiye, ilibaini nyumba ya walimu katika Shule ya Msingi Ngoma iliyoko Kata ya Kasulo iliyojengwa kwa gharama ya Sh milioni 45 kuwa chini ya kiwango.
Kamati hiyo iliagiza ndani ya siku saba Halmashauri imtafute mkandarasi aliyejenga nyumba hiyo, aondoe milango, vigae na nyavu za madirisha na kuweka vingine kutokana na vilivyowekwa kuwa chini ya kiwango ikilinganishwa na fedha zilizotumika. Ubadhirifu mwingine umebainika katika Mradi wa Maji katika Kijiji cha Nterungwe Kata ya Nyamihaga.
Ilibainika mradi huo uliojengwa tangu mwaka 2004, maji hayajawahi kutoka licha ya Halmashauri ya Wilaya ya Ngara kutenga zaidi ya Sh milioni moja kila mwaka kwa ajili ya kufanya ukarabati wa mradi huo ‘hewa’.
Kamati ilimwagiza Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kuhakikisha mradi huo unakamilika haraka iwezekanavyo ili kuondoa kero kwa wananchi wa eneo hilo ambao hutembea umbali wa kilometa 10 kufuata maji.
Mradi mwingine ni wa upanuzi na ukarabati wa miundombinu ya maji Ngara mjini ambao Sh milioni 150 zilitolewa na Rais Jakaya Kikwete. Pia ilibainika katika fedha hizo, zaidi ya Sh milioni 32 zimetumika tofauti na utaratibu.
Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Fabian Massawe aliiambia kamati hiyo kuwa baada ya kugundua ubadhirifu huo, Meneja wa Mamlaka ya Maji Ngara Edward Magai (60) amefikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo.
Chanzo;Habari Leo 
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa