Home » » Wafugaji wauawa kinyama

Wafugaji wauawa kinyama



 WAFUGAJI wawili wameuawa kinyama kwa kukatwa mapanga na kuchomwa mikuki na wananchi, huku ng'ombe wapatao 12 nao wakiuawa katika Kijiji cha Kasulo wilayani Ngara, Mkoa wa Kagera.
Chanzo cha mauaji hayo kinadaiwa kuwa ni uhasama wa muda mrefu kati ya wananchi na wafugaji hao wanaodaiwa kuingiza mifugo kijijini humo bila ridhaa ya serikali ya kijiji.
Tukio hilo lilitokea Septemba 19 mwaka huu, saa 11:00 jioni na kwamba ng'ombe waliouawa kwa kuchomwa mikuki na kukatwa mapanga, nyama zake zilichukuliwa na wanawake kwa ajili ya kitoweo.
Akithibitisha tukio hilo, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ngoma 'B' yalipotokea mauaji hayo, Simeon Nzakaya alilaani kitendo cha wananchi kujichukulia sheria mkononi na kuwataja waliouawa kuwa ni Ngabo Godfrey (24) na mwingine ambaye bado hajatambulika jina lake.
Alisema kuwa miili ya marehemu hao ilipatikana Septemba 20, na watu wanane wanashikiliwa na vyombo vya usalama kwa mahojiano zaidi kuhusiana na mauaji hayo.
Hata hivyo, taarifa zinadai kwamba baadhi ya mamlaka zinazolalamikiwa ni pamoja ni Idara ya Uhamiaji Wilaya, Mifugo na Halmashauri ya Wilaya kupitia kitengo cha sheria kwa kushindwa kuchukua hatua mara baada ya kuombwa kuingilia kati mambo ya uvamizi wa wafugaji.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kasulo, Yusufu Katula alithibitisha kuwepo kwa mauaji hayo pamoja na kulaani kitendo hicho.
"Mgogoro huo unafukuta kutokana na idara husika kutochukua hatua mapema. Hii inachangia kutokea mauaji kama haya, na hatua za haraka zisipochukuliwa yanaweza kutokea mapigano makali kati ya wanakijiji na wafugaji wanaoingia kinyemela,"alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Costantine Kanyasu alionya kuwa matukio kama hayo hayaruhusiwi kutokea katika jamii, na aliahidi ofisi yake kuyafanyia kazi malalamiko yote yanayotolewa kwa baadhi ya mamlaka.
"Ni kweli baadhi ya mamlaka za serikali zinalalamikiwa sana na wananchi. Na sasa nitakachokifanya ni kuchukua hatua za haraka kuhakikisha tukio kama hilo halitokei tena," alisema.
Chanzo: Tanzania Daima



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa