Home » » Zana haramu 9,000 zateketezwa

Zana haramu 9,000 zateketezwa

SERIKALI kupitia Idara ya Uvuvi mkoani Kagera, imekamata na kuteketeza kwa moto zana haramu 9,809 zilizokuwa zikitumika kwenye uvuvi ndani ya Ziwa Victoria.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Bukoba, Ofisa Mfawidhi wa Uvuvi na Doria Mkoani Kagera, Apolinary Kyojo alisema zana hizo zilikamatwa kutokana na msako maalumu wa kushitukizwa ndani ya Ziwa Victoria.
Alisema msako huo wenye lengo la kupambana na uvuvi haramu ndani ya ziwa hilo ulifanyika kati ya Juni na Agosti mwaka huu.
"Serikali inaendelea kupambana na watu wanaoshiriki uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria. Kati ya Juni na Agosti mwaka huu, tulikamata zana haramu 9,809. kwenye msako wa kushtukiza,” alisema.
Alizitaja zana zilizokamatwa kuwa ni nyavu zenye matundu madogo zipatazo 7,000, nyavu aina ya timba 2,700, makokoro yenye urefu wa zaidi  ya mita 110,000, vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh 750,000.
Kwa mujibu wa Kyojo katika kutekeleza misako ya namna hiyo, idara yake inakabiliwa na changamoto ya kukosa ushirikiano kutoka kwa baadhi ya viongozi wa vijiji, kata na hata wasimamizi wa rasiliamali za Ziwa Victoria (BMU).
Chanzo: Tanzania Daima


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa