Home » » RC: Tengeni maeneo ya vijana, wanawake

RC: Tengeni maeneo ya vijana, wanawake

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Salim Kijuu
VIONGOZI wa mitaa, vijiji na kata na wataalamu wa Serikali, wametakiwa kutenga maeneo ya vikundi vya uzalishaji vya vijana na wanawake ili wajikwamue katika umasikini wa kipato.
Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Salim Kijuu wilayani Karagwe hivi karibuni alipofika kujitambulisha.
Alisema watendaji, wananchi, wadau wakiwamo viongozi wa dini, watoe ushauri na maoni kujua changamoto zinazowakabili ili Serikali izifanyie kazi kwa haraka.
“Katika suala zima la ajira kwa vijana na uwezeshaji kiuchumi, naagiza mamlaka husika ambao ni madiwani, serikali za vijiji na mitaa, wataalamu na wananchi katika ngazi za vijijini, mitaa na kata kutenga maeneo. Maeneo hayo ni kwa ajili ya vikundi vya wanawake na vijana ili waweze kuanzisha miradi ya kilimo, ufugaji, viwanda vidogo na biashara, hii itasaidia waweze kuzalisha na kuondokana na umasikini wa kipato,” alisema Kijuu.
Alisema hiyo ni hatua za awali katika maandalizi ya mpango wa Serikali wa kutoa fedha za kuwezesha wanachi kiuchumi na kuwekeza katika miradi ya kuzalisha mali.
“Vijana washauriwe, wajengwe katika misingi ya kujitegemea na kuwatengenezea mbinu zitakazowawezesha kuibua miradi kama vile kilimo cha mboga ambapo watavuna kwa muda mfupi pia watafutiwe masoko, kuanzisha viwanda vidogo ambapo wakikusanyika kwa pamoja na kila mtu akaleta wazo lake na ujuzi wake wakaungana wanaweza kutengeneza kitu kizuri na kutokea hapo wakajikuta wanaingia katika viwanda vikubwa," alisema Kijuu.
Chanzo Gazeti la Habari Leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa