Home » » Watu 7 kortini kwa uchomaji makanisa

Watu 7 kortini kwa uchomaji makanisa

Imeandikwa na Angela Sebastian, Bukoba
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi
POLISI mkoani Kagera imekamata watu saba na kuwafikisha mahakamani wakihusishwa na uchomaji moto makanisa kikiwemo Kigango cha Nyarwele Parokia ya Kimiza, Jimbo Katoliki la Kayanga wilayani Karagwe.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Augustine Ollomi alibainisha hayo jana ofisini kwake mjini Bukoba wakati akizungumza na gazeti hili ambalo lililenga kutaka kujua chanzo cha uchomaji wa makanisa, pia kama kuna waliokamatwa na wamechukuliwa hatua gani mpaka sasa.

Alisema tangu mwaka jana, zaidi ya makanisa 10 yamechomwa katika mkoa huo na Polisi waliunda kikosi kazi cha kusaka wanaojihusisha na vitendo, hivyo mpaka sasa watu saba wamefikishwa mahakamani huku jeshi hilo likiendelea kuwasaka wahusika wengine.

“Tumewakamata watu saba na kuwafikisha mahakamani. Uchunguzi wa kina unaendelea ili tuweze kubaini chanzo ni nini na wanatumwa na nani kuchoma nyumba za ibada na baada ya kupata chanzo ndipo tutatoa taarifa kamili. Tunaendelea na uchunguzi wetu,” alisema Kamanda Ollomi.

Alisema katika matukio ya hivi karibuni, makanisa mawili yalichomwa moto Januari mwaka huu katika kata ya Kihanga wilayani Karagwe yamechomwa ingawa kanisa moja ndilo liliathirika sana.

Alitaja makanisa hayo kuwa ni Tanzania Assemblies of God (TAG) na Pentekoste Assemblies of God (PAG) pia kuamkia Mei 2, mwaka huu watu wasiojulikana walichoma kigango cha Kanisa Katoliki wilayani humo na kusababisha hasara ya zaidi ya Sh milioni 52.1.

Chanzo Gazeti la Habari leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa