Home » » BENKI YASUASUA MALIPO YA KAYA MASIKINI.

BENKI YASUASUA MALIPO YA KAYA MASIKINI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WALENGWA wa Mpango wa Uhawilishaji wa fedha za ruzuku kwa kaya masikini unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) III wa kunusuru kaya masikini wilayani Kyerwa, wamelalamikia ucheleweshwaji wa fedha kutoka benki wakati wa malipo ambao umeonekana kuwa kero na kuwakatisha tamaa wahusika hao.
Walitoa malalamiko hayo kwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella aliyefanya ziara ya siku moja kwa lengo la kupata maelezo juu ya maendeleo ya mpango na mafanikio yaliyofikiwa na kutafuta ufumbuzi juu ya changamoto zinazokabili mpango huo ili malengo ya Serikali ya kupunguza umasikini yafikiwe kwa asilimia 100.
Mkazi wa kijiji cha Mulongo, Adelina Danstan alisema mwanzoni wakati wanaingizwa katika mpango huo walielezwa kuwa dirisha la malipo linafunguliwa na kufungwa ndani ya siku nne, lakini kwa Wilaya ya Kyerwa ni tofauti ambapo hufunguliwa siku nne lakini malipo hufanyika siku mbili au moja usiku na mchana.
“Wenzetu wakianza kupata malipo sisi hushinda vituoni siku mbili jua kali au mvua ikiwa halali yetu tukisubiri malipo ambapo tunalazimika kuwauliza wahusika wa Tasaf ambao tunaelezwa kuwa benki ndiyo inayokwamisha na kusababisha hali hiyo hata wao hawapendi hali hiyo itokee,” alieleza Dastan.
Mkazi wa kijiji cha Rwabikagati, Catherine Binomutonzi alisema kutokana na adha hiyo inayoelezwa kuwa inasababishwa na benki kutotoa kipaumbele kwa wilaya hiyo husababisha walengwa kuhudhuria vituoni siku mbili na kutoka patupu; na siku ya tatu jioni ndipo fedha zinapoletwa na kuanza kugawiwa mpaka usiku.
“Hali hii inakatisha tamaa na kuona kama tunadharauliwa kwa kuwa ni masikini, kwa hiyo tunakuomba Mkuu wa Mkoa kuingilia kati na kuona ni sababu zipi zinakwamisha. Kumbuka ucheleweshwaji huo unasababisha msongamano, wazee hapa wanashindwa kubaki mpaka usiku wakihofia maisha yao kuwa hatarini kwani wanaweza kukabwa na vibaka usiku kwa hiyo wanalazimika kuondoka na kuiacha fedha,” alisema Binomutonzi.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa