Home » » MGANGA MKUU ASAFISHWA KASHFA YA FEDHA BUKOBA.

MGANGA MKUU ASAFISHWA KASHFA YA FEDHA BUKOBA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongela (wa pili kutoka kushoto) akishuhudia mgao wa fedha kwa kaya masikini mkoani humo.
MWENYEKITI wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba, Murshid Ngeze amesema aliyekuwa Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya hiyo (DMO), Dk Hamza Mgula hahusiki na tuhuma za kubadili matumizi ya fedha za Halmashauri hiyo zilizosababisha watumishi saba kusimamishwa kazi.
Januari 28, mwaka huu, Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba lilipendekeza kusimamishwa kwa watumishi saba kwa lengo la kupisha uchunguzi kutokana na kubadili matumizi ya fedha Sh milioni 851 za miradi ya maendeleo na ukosefu wa baadhi ya nyaraka za uhamisho wa fedha hizo.
Awali, Mwenyekiti huyo alilieleza gazeti hili kwa simu kuwa Dk Mgula ambaye sasa yuko Manispaa ya Bukoba ni miongoni mwa watumishi hao ambao wamesimamishwa kazi, lakini baadaye alieleza kuwa DMO huyo hahusiki, kwani Baraza hilo liliamua kuwasimamisha watumishi hao saba.
“Katika taarifa zilizotolewa mwanzo na kuandikwa katika vyombo mbalimbali zilimhusisha aliyekuwa DMO wa Halmashauri hiyo kwa kipindi cha nyuma ambaye sasa ni Mganga wa Manispaa ya Bukoba Dk Hamza Mgula, mtumishi huyo hahusiki na tuhuma hizo na si mtumishi wa Halmashauri hii,” alieleza Mwenyekiti Ngeze katika barua ambayo aliviandikia vyombo vya habari kufafanua suala hilo.
Kwa mujibu wa Ngeze, waliosimamishwa ni Mweka Hazina wa Wilaya, Jonathan Katunzi, Kaimu Mweka Hazina wa Wilaya, Selialis Mutalemwa, Mhandisi wa Wilaya, Robert Massoro na Fundi Sanifu Mkuu wa Wilaya, Desu Bizibu. Aliwataja wengine kuwa ni Ofisa Elimu Sekondari Wilaya, Lucas Mzungu, Ofisa Mipango wa Wilaya, Mustapha Sabuni na Mganga wa Mifugo wa Wilaya, Dk Kisanga Makigo.
Aidha, Mwenyekiti huyo alisema Mkurugenzi Mtendaji (DED) aliyekuwepo Gladys Ndyamvunye ambaye amehamishiwa mkoani Pwani akitakiwa kurudishwa kujibu tuhuma zinazomkabili.
Alisema baraza hilo limewasimamisha kazi watumishi saba wa Idara mbalimbali kutokana na mapendekezo ya timu iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella ili kufanya uchunguzi juu ya tuhuma za ubadhirifu wa zaidi ya Sh milioni 851 zilizokuwa zimepangwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Pamoja na kuchukua hatua za kinidhamu kwa watumishi hao, Baraza hilo la madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba limemtaka Katibu Mkuu Tamisemi kumchukulia hatua za kinidhamu Ndyamvunye kwa kosa la kutosimamia ipasavyo fedha hizo.
Kwa mujibu wa taarifa ya uchunguzi chini ya uenyekiti wa Mhandisi Wambura Sabora, fedha zinazodaiwa kufujwa ama kubadilisha matumizi ni Sh milioni 168 za Mfuko wa Jimbo, Sh milioni 200 kama ombi maalum la ujenzi wa Daraja la Kyamabale, Sh milioni 176 za Mfuko wa Barabara na Sh milioni 307 zilizotolewa na wafadhili katika Mfuko wa Afya.
CHANZO : HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa