Home » » WAZIRI WA JK ATEMA CHECHE

WAZIRI WA JK ATEMA CHECHE

WAZIRI katika Serikali ya Rais Jakaya Kikwete, ametaka viongozi wote walionufaika na fedha za kutoka akaunti ya Tegeta Escrow, washtakiwe, wafungwe na kufilisiwa mali zao, kwani kuwafuta kazi au kujiuzulu hakusaidii Watanzania.

“Kitendo cha kufukuzwa kazi viongozi walionufaika na fedha za akaunti ya Escrow hakutoshi... kuwafanya hivyo, ni sawa na kuwafanyia watu send off na kuwapeleka fungate kwa pesa ya wananchi.”

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, wakati alipofanya ziara katika Hospitali ya Mwananyamala ili kuwajulia hali wajawazito na watoto ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa.

Alisema endapo watafilisiwa na kufungwa jela itakuwa ni kujenga Taifa lenye kuogopa fedha za umma zinazohitajika kutumika sehemu nyingi kwa ajili ya manufaa ya nchi yetu.

“Watu wanaokula pesa za wananchi ni lazima wafukuzwe, kufungwa na hata kufilisiwa pesa hizo ni kodi ya wananchi ambayo ingetumika sehemu nyingine kama hospitali...kitendo cha wajawazito kulala watu wawili ni aibu kwa nchi yetu, hivyo inatakiwa ukusanywaji wa kodi ufanywe kwa kina ili kuondoa changamoto zilizopo hospitalini,”alisema Nchemba.

Aliongeza kuwa tayari watumishi saba wamesimamishwa kazi ni wale ambao walioiachia kodi katika sakata la escrow. “

Hivyo wanatakiwa kuhojiwa na katika mahojiano hayo wakisema kuwa walikuwa hawajui kama pesa hizo zilikuwa zinatakiwa kukatiwa kodi itajulikana kuwa walikuwa si watumishi wa TRA au BoT na wakisema kuwa walikuwa wanajua ni lazima hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.

Nchemba aliwashangaa viongozi wenzake wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuacha kufanya majukumu waliyonayo na kuanza kusimulia habari za uchukuaji wa fomu za urais.

“Hii inachekesha mno badala ya sisi viongozi kufanya majukumu yetu tuliyoagizwa tunawaza namna ya kuchukua fomu ya urais wakati muda bado haujafika, wana- CCM wenzangu muda ukifika kila mtu atawajibika kuchukua fomu,”alisema Nchemba.

Naye, Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mwananyamala Dkt. Sophinias Ngonyani, alisema anashukuru kwa msaada alioutoa Waziri katika hospitali hiyo kwa kuwa utawaletea tija.

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa