Home » » MWIJAGE: WAWEKEZAJI WASIKATISHWE TAMAA

MWIJAGE: WAWEKEZAJI WASIKATISHWE TAMAA

Imeandikwa na Regina Mpogolo
Waziri wa Viwanda na Biashara, Charles Mwijage.
WAZIRI wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amesema Tanzania ni changa katika sekta ya viwanda hivyo faini za mara kwa mara kwa wawekezaji wa sekta hiyo wakidaiwa kuharibu mazingira zitawakatisha tamaa.
Baraza la Taifa la Uhifadhi Mazingira (NEMC) imekuwa ikifanya ziara mara kwa mara kukagua viwanda hasa vile ambavyo vinalalamikiwa kufanya uchafuzi wa mazingira na kuvifungia kwa muda ili vifanye marekebisho, kutoza faini au vyote viwili.
Katika mahojiano na kituo kimoja cha redio nchini jana, siku ambayo huadhimishwa Siku ya Viwanda Afrika, Mwijage alisisitiza kuwa faini za mara kwa mara kwa wawekezaji haiwajengi, bali kuwakatisha tamaa.
Mwijage alisema ni kazi ya wizara yake pamoja na taasisi nyingine kuhakikisha wawekezaji wanaelimishwa badala ya kutozwa faini kwani nchi bado ni changa katika sekta ya viwanda na pia faini hazifundishi.
“Hawa watu walikuwa na shughuli zao, lakini tumefanya kazi kubwa kuwashawishi kuingia katika sekta ya viwanda, leo hii unataka wajue elimu yote kwenye viwanda walisomea wapi?” alihoji Mwijage.
Alisema wizara yake mwaka huu inaanzisha Kitengo cha Mazingira kwa lengo la ulezi na pia kuwafundisha wenye viwanda utunzaji wa mazingira katika viwanda. Akizungumzia viwanda, Mwijage alisema nia ni kuwa na viwanda vingi vyenye ushindani na kila mwananchi ashiriki katika uchumi huo na kujenga viwanda ambavyo vinatumia malighafi za ndani.
“Asilimia 70 mpaka 80 ya Watanzania wanajihusisha katika kilimo sasa tujenge viwanda ambavyo vinapokea haya mazao, pili tuzalishe ajira za kutosha kwa vijana na kuzalisha bidhaa ambazo zinatumiwa sana na watu,” alisema na kuongeza kuwa nia ya serikali pia ni kuhakikisha viwanda vyote vinafufuliwa ambapo alifafanua kuwa kuna viwanda 156 hapa nchini, vinavyofanya vizuri ni 62 na 56 vilikua na matatizo.
Mwijage alisema kati ya hivyo, viwanda 56 vyenye matatizo sasa vimepata wawekezaji na vingine wenyewe wanavifufua
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa