Home » » WAVUVI WALALAMIKIA POLISI

WAVUVI WALALAMIKIA POLISI

WAVUVI wa Kisiwani Mazinga, Kata ya Mazinga wilayani Muleba, Kagera, wamelilamikia Jeshi la Polisi kwa kutoweka ulinzi wa kutosha katika Ziwa Victoria hali inayosababisha wavuvi hao kufanyiwa vitendo vya uhalifu na kuuawa.
Walisema hayo jana walipozungumza na waandishi wa habari baada ya kuona jeshi hilo halichukui hatua kuhusu taarifa za kunyang’anywa zana zao za uvuvi, zikiwemo injini za boti katika tukio la hivi karibuni.
Mvuvi Misana Ramadhani mkazi wa mwalo wa Kimoyomoyo, Kijiji cha Mazinga, alisema hivi sasa wamechoshwa na vitendo vya uhalifu wanavyofanyiwa kila mara.
Thomas Josia ambaye ni mmiiki wa mitumbwi, alisema serikali wakati wa kutoza kodi mbalimbali inakuwa ya kwanza kufika visiwani na wavuvi wanakuwa mstari wa mbele kulipa kodi, lakini suala la usalama wao haijali.
“Rais Kikwete wakati wa ahadi zake alisema atapambana na uhalifu katika sekta ya uvuvi, lakini tunashangaa hakuna kinachoendelea hadi sasa badala yake tunazidi kuporwa mali zetu… tutaishije wakati ulinzi unapelekwa nchi nyingine wazawa tunateseka?” alihoji Josiah.
Diwani wa Mazinga, Alex Bakenjela, alisema baada ya Jeshi la Polisi kuona kilio cha wavuvi hao, limekubali na kushauri kuwepo kwa polisi jamii watakaobaini chanzo cha tatizo.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, George Mayunga, alisema hajapata taarifa hiyo kutoka wilayani, huku akiahidi kufuatilia suala hilo.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa