Home » » CUF YAHIMIZA WANACHAMA KUWANIA UONGOZI

CUF YAHIMIZA WANACHAMA KUWANIA UONGOZI

CHAMA cha Wananchi (CUF) Wilaya Bukoba Mjini, mkoani Kagera, kimewataka wanachama na wakereketwa wa chama hicho kuhamasishana kukipa nguvu chama pamoja na kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi wa serikali za mitaa  baadaye mwaka huu.
Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa la CUF, Saverina Mwijage, alipokuwa akitoa salamu kwa wajumbe wa mkutano mkuu wa wilaya uliofanyika katika Manispaa ya Bukoba.
Mwijage ambaye pia aliwahi kuwa Mbunge wa Viti Maalumu, aliwataka wananchi wilayani Bukoba kutokata tamaa na badala yake wakitetee chama mbele ya Watanzania.
“Kwa kuwa uchaguzi wa serikali za mitaa unakaribia, nawaomba wapenzi, wakereketwa na wananchi wote kwa ujumla kuanza kujiandaa kwa kuwabaini wanachama ambao wanaweza kujitokeza kuwania nafasi za uongozi, kwani msingi wa chama cha siasa kuwa na nguvu ni kuanzia kuchukua madaraka katika serikali za mitaa,” alisema.
Alisema kwa kipindi ambacho amekuwa nje ya Bunge, kuna mambo mengi amejifunza yanayohusu maendeleo ya wananchi wa Bukoba na yanayomshawishi kuanza kuhamasisha wananchi wa Bukoba kupigania chama, ili kiweze kuwainua kiuchumi wananchi.
“Bukoba imegubikwa na migogoro kila siku, wananchi hawapati kile kilichotarajiwa. Migogoro haimsaidii mwananchi, mimi nimeazimia kusaidiana na chama changu kutatua kero hizo,” alisisitiza Mwijage.
Katibu wa CUF Wilaya ya Bukoba Mjini, Ramadhan Bahati, aliwataka vijana, wanawake na wapenzi wa CUF wilayani humo kuanza kurudisha nguvu ya chama hicho kuanzia ngazi za kata.
Alisema dhamira ya chama hicho ni kurudisha nguvu kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa