Home » » WAVUVI WAANDAMANA KUPINGA UVAMIZI

WAVUVI WAANDAMANA KUPINGA UVAMIZI

ZAIDI ya wavuvi 30 wa Kisiwa cha Mazinga, Kata ya Mazinga wilayani Muleba, wameandamana hadi kituo cha polisi cha wilaya, kulalamikia kutokuwepo ulinzi katika Ziwa Victoria, kiasi cha kutoa mwanya kwa majambazi kuwavamia na kuwapora zana za uvuvi.
Wakizungumza na Tanzania Daima mbele ya kituo cha polisi, wavuvi hao walisema wameamua kuandamana kutokana na kuongezeka kwa uvamizi huo, huku Jeshi la Polisi likionekana kutochukua hatua madhubuti za kuimarisha ulinzi.
Walisema mwishoni mwa wiki iliyopita kundi la majambazi liliwavamia wavuvi watano na kuwashambulia kwa mapanga, kisha kuwapora zana zao za uvuvi zenye thamani zaidi ya sh milioni 60.
Katika shambulizi hilo, majambazi hao waliwajeruhi Nicolaus Cleophas (33), Amidu Hussein (32 ), Mussa Antony (28) Medson Muhanika (30) na Juma Said (40 ) wote wakazi wa Mulumo Mazinga.
Walidai pia kuwa hivi karibuni kundi la majambazi wenye silaha za moto lilivamia kisiwa hicho na kupora zana za uvuvi mbalimbali, zikiwemo injini za mitumbwi sita zenye thamani ya sh milioni 18 pamoja na kuwajeruhi kwa mapanga wavuvi sita.
Imedaiwa kwa majambazi hao wamekuwa wakifanya uporaji kila wanapojisikia kwa kuwa wanajua Jeshi la Polisi wilayani humo haliwezi kufanya chochote.
Thomas Josia, mmoja wa wamiliki wa mitumbwi, alisema wakati wa kutoza kodi mbalimbali serikali inakuwa ya kwanza kufika visiwani humo huku wavuvi wakiwa mstari wa mbele kulipa, lakini serikali inakwama kuchukua hatua za haraka kuwalinda.
Diwani wa Kata hiyo, Alex  Bakenjela, alisema  wamezungumza na Jeshi la Polisi ambapo wamekubaliana kushirikiana ili kubaini chanzo cha ujambazi huo na njia za kukabiliana nao.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, George Mayunga, alisema hana taarifa za kuvamiwa kwa wavuvi hao, lakini akaahidi kulifuatilia suala hilo ili walipatie ufumbuzi kwa lengo la wananchi wafanye kazi zao bila hofu.
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa