Home » » PINDA:SERIKALI HAIMTAMBUIMEYA BUKOBA

PINDA:SERIKALI HAIMTAMBUIMEYA BUKOBA

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
 
Serikali haimtambui Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatoli Amani, kwa kuwa alijiuzulu mbele ya Baraza la Madiwani.
Hata hivyo kiongozi huyo alikana maamuzi yake na kuendelea kufanya shughuli za umeya ambazo serikali iliagiza zifanywe na Naibu Meya.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alitoa kauli hiyo jana bungeni wakati akijibu hoja mbalimbali za wabunge waliochangia  bajeti ya ofisi yake  na Mbunge wa Bukoba Mjini (CCM), Balozi Khamis Kagasheki, kumtupia lawama Pinda  kushindwa kutatua mgogoro huo kwa miaka mwili.

"Nasisitiza Amani  si Meya tangu siku alipojiuzulu, alitoa tamko hili kutokana na ushauri uliokuwa umetolewa,”  alisema.

Alieleza kuwa  alichukua hatua mbalimbali ikiwa ni  kuunda kamati ya mkuu wa mkoa na  kuihusisha ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) aliyefanya ukaguzi na kuandaa ripoti ambayo iliionyesha kasoro nyingi  na kuagiza kuwa kwa mazingira hayo Meya ajiuzulu pamoja na wataalamu waliohusika.

"Barua niliyoletewa na Naibu Waziri Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, aliyehudhuria kikao kile, Meya alikubali kujiuzulu mbele ya Baraza la Madiwani, lilikuwa jambo la wazi katamka amekubali na kuandika barua ya  kuthibitisha, lakini muda kidogo pakatokea zogo ambalo sijui chanzo chake," alisema.

Pia alisema  madiwani walifungua kesi kuitaka mahakama iagize madiwani wa Manispaa ya Bukoba wasikutane  mpaka suala hilo litakapomalizika na kwamba kama kiongozi walipokea uamuzi huo na kuomba wanasheria kupinga uamuzi huo ili kazi za manispaa ziendelee.

Alisema shughuli za maendeleo zimesimama na kwamba madiwani hawawezi kuendelea kukutana kwa kuwa watakuwa wanakwenda kinyume na uamuzi wa mahakama.

Aidha, alimwagiza Mkuu wa mkoa wa Kagera, Kanali Mstaafu Fabian Massawe, kuzungumza na madiwani kuwa wananchi ndiyo wanaumia katika zoezi hilo na ni heri kuondoa kesi mahakamani.

"...kuliko kujifunga baraza lisikutane wana miradi ya mabilioni ya fedha, hakuna chochote kinachoweza kufanyika Bukoba, hili si jambo la busara kwa kiongozi unajua suala hili haliwasaidii wananchi wako lakini unasema potembelea mbalo, hili linanisumbua kidogo," alifafanua.

Hata hivyo,  hadi sasa Meya huyo hajaandika kwa maandishi kujiuzulu kwake na kubaki kwa maandishi kama alivyosema kwenye kikao huku kukiwa na mgawanyiko mkubwa kwa madiwani hao.

Mgogoro huo kati ya viongozi hao unahusishwa na utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa soko kuu la Bukoba na upimaji wa viwanja 5,000, miradi ambayo Kagasheki anadai ni ya kifisadi kwa madai kwamba mikataba yake haiko wazi na mmojawapo haujafanyiwa upembuzi yakinifu.

Baada ya mvutano mkali wa ndani CCM  mkoa wa Kagera chama hicho kiliwasimamisha madiwani tisa, lakini siku chache baadaye CCM Taifa iliwarejeshea nafasi zao.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa