Home » » AMANI AGEUZIWA KIBAO BUKOBA

AMANI AGEUZIWA KIBAO BUKOBA

Anatory Amani BAADHI ya madiwani na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera, wamelaani kitendo cha aliyekuwa Meya wa manispaa hiyo, Anatory Amani cha kuweka pingamizi mahakamani ili kuzuia kikao cha dharula cha madiwani.
Waakizungumza baada ya kumalizika kwa kikao hicho juzi, baadhi ya madiwani hao akiwemo mbunge wa Viti Maaalum, Conchestaer Rwamulaza (CHADEMA), walisema inasikitisha kuona malumbano yaliyokuwepo wakati wa nyuma yakijitokeza tena kupitia kwa mtu mwenye maslahi binafsi.
Rwamlaza ambaye pia ni Katibu wa CHADEMA mkoa wa Kagera, alisema kuwa hatua ya Amani kuweka pingamizi mahakamani ni kukwamisha maendeleo ya wananchi bila sababu.
“Sikufurahishwa na maamuzi haya aliyochukua Amani kwenda mahakamani kupinga vikao visiendelee. Tulikuwa na kesi baadhi ya madiwani wameondolewa nyadhifa zao wakituhumiwa kukwamisha maendeleo ya Bukoba lakini bado yeye kwa maslahi yake binafsi anaweka pingamizi tena,”alisema.
Naye Diwani wa Kata ya Bakoba, Felician Bigambo (CCM), alisema kuwa japokuwa hawana mamlaka ya kuingilia uhuru wa mahakama lakini wamesikitishwa na hatua hiyo ya ubinafsi wa Amani ambaye pia ni diwani kata ya Kagondo.
“Tunaomba Serikali kuingilia kati hata kama mahakama haingiliwi, jamani angalia mtu mmoja anaamua kukwamisha na kuzuia vikao visiendelelee kwa maslahi yake.
Haingii akilini maana wenzetu walivuliwa nyadhifa wakidaiwa kukwamisha maendeleo, sasa wananchi wapime nani anawakwamisha,”alisema.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bukoba, Yusuph Ngaiza alisema kuwa Amani hapendi maendeleo ya Bukoba kwa sababu kila kinachofanyika yeye anaweka pingamizi mahakamani.
Wakili wa Amani, Alon Kabunga alisema kuwa kwa mujibu wa taratibu kikao kilichoitishwa na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo pamoja na Naibu meya, Alexander Ngalinda juzi hakikuwa halali kwani sheria, Amani bado inatambulika kuwa Meya Bukoba.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa