Home » » MTAMBO MPYA WA KUFUA UMEME WAFUNGWA KAGERA

MTAMBO MPYA WA KUFUA UMEME WAFUNGWA KAGERA

 

WANANCHI mkoani Kagera wataondokana na tatizo la kukatika kwa umeme baada ya kufungwa mtambo mpya wa kufua Umeme (Transfoma) katika eneo la Kibeta kwa ajili ya kusambaza huduma ya umeme kwa wakazi wa mkoa huo.

Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco ) mkoani Kagera mhandisi Martine Madulu alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari, waliotembelea eneo ilipofungwa transfoma hiyo.

Mhandisi Madulu alisema kuwa serikali imeamua kuleta transfoma hiyo mpya, iliyogharimu zaidi ya sh.Bilioni 1.3 kutokana na kuongezeka kwa wateja na kusababisha transfoma iliyokuwepo kushindwa kukidhi mahitaji ya wateja.

“Transfoma hii ina uwezo wa kuzalisha megawati 12 za umeme tofauti na iliyokuwa ikitumika, ambayo ilikuwa na uwezo wa kuzalisha megawati nne… mahitaji ya wateja wote ambao ni zaidi ya 22,000 katika manispaa hiyo yaliishafikia megawati sita” alisema Meneja huyo.

Alisema kuwa transfoma hiyo itakuwa na uwezo wa kuhudumia wateja zaidi ya 22,000 tofauti na iliyokuwepo awali ambapo ilikuwa na uwezo wa kuhudumia wateja 15,000.

Aidha Mhandisi Madulu aliwataka wananchi mkoani Kagera kuendelea kushirikiana na Tanesco katika kutoa taarifa kwa wanaohujumu miundombinu ya shirika hilo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Wakati huo huo, alisema kuwa wameanza awamu ya pili ya Mradi wa Umeme Vijijini (REA), ambapo hadi kufikia mwezi Juni mwakani vijiji 400 mkoani Kagera vinatarajiwa kuwa vimenufaika kupitia mradi huo.

Kwa mujibu wa meneja huyo ifikapo mwakani wateja wanaohudumiwa na shirika hilo watakuwa wameongezeka kutoka idadi ya sasa hadi kufikia 36,000.

Kwa upande wake mhandisi wa Tanesco kutoka makao makuu,anayesimamia ufungaji wa transfoma hiyo, Amon Gamba alisema kuwa kufungwa kwa transfoma hiyo kutawezesha kuongezeka kwa idadi ya wateja na hivyo kuondoa malalamiko yaliyokuwepo ya umeme mdogo.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa