Home » » SERIKALI HAINA FEDHA ZA KULIPA FIDIA-MUHONGO

SERIKALI HAINA FEDHA ZA KULIPA FIDIA-MUHONGO

WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, amesema Serikali haina fedha za kulipa fidia kwa wananchi wa maeneo ambayo Mradi wa Umeme Vijijini (REA) unatekelezwa mkoani Kagera.

Profesa Muhongo, alitoa kauli hiyo wiki iliyopita, baada ya kutembelea na kukagua mradi wa usambazaji umeme katika kijiji cha Katoke, wilayani Biharamulo, Kagera.

Alisema Serikali haina fedha za kuwalipa wananchi fidia katika maeneo ya mradi wa REA ingawa ni haki yao, kwa sababu hiyo italazimika kuhamisha mradi na kuupeleka ambako wananchi hawahitaji fidia bali nishati ya umeme.

Alisema kuwa, fidia ni utapeli na hakuna mahali ambapo fidia imetolewa (imelipwa ) kwa wananchi kesi zikaisha, hivyo wananchi waelezwe ukweli kuwa hakuna fedha za fidia. "Fidia ni haki yao, lakini hatuna fedha za kuwalipa.Sasa wafanye uamuzi, wanahitaji umeme au fidia.

"Kama ni fidia wasubiri baada ya miaka 20.Na kwa sababu hiyo tutahamisha mradi tuupeleke maeneo wasikohitaji kulipwa fidia," alisema Profesa Muhongo.

Alisema dhamira ya serikali ni kufuta umaskini na kuleta ajira mpya kwa kuwaunganishia wananchi umeme ambao utasaidia kukuza na kuboresha biashara zao, kilimo cha kisasa, kuboresha huduma za afya na elimu.

Aidha alisema tatizo ni wananchi kukataa kulipa fedha za kuunganishiwa umeme ambazo ni sh 27,000 tu,na kufafanua kuwa taasisi za umma (ofisi za watendaji, shule na zahanati) na taasisi za kidini (makanisa na misikiti) zitaunganishiwa bure nishati hiyo.

Profesa Muhongo, aliwataka Wahandisi nchini kuanzisha kampuni zao wafanye kazi za miradi mbalimbali ya ujenzi wa nishati ya umeme, badala ya kulalamika kuwa kazi nyingi wanapewa wageni badala ya wazawa.

Aidha Mratibu wa mradi huo mkoani Kagera, Mhandisi Julius Kateti wa kampuni ya Urban and Rural Engineering Service Ltd, alisema mradi huo utagharimu sh. 98 bilioni na utakamilika Januari mwakani.

Alisema zinahitajika nguzo 55,000 ili kukamilisha mradi huo na kampuni hiyo imeagiza nguzo nyingine kutoka nchini Uganda na Afrika Kusini

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa