Home » » JPM: SINA UTANI MATUMIZI YA EFDS

JPM: SINA UTANI MATUMIZI YA EFDS

Imeandikwa na Mwandishi Wetu, Biharamulo
Rais John Magufuli akiondoa kitambaa kwenye jiwe la msingi, kuashiria ufunguzi wa Barabara ya Biharamulo-Kagoma-Lusaunga ya kiwango cha lami yenye urefu wa Kilometa 154 wilayani Biharamulo, mkoa wa Kagera wakati akiwa kwenye ziara ya siku mbili mkoani humo jana. (Picha na Ikulu).
RAIS John Magufuli ametoa siku 14 kwa wamiliki wa vituo vya mafuta nchini, kuhakikisha kwamba wanafunga mashine za kielektroniki za kutolea risiti (EFDs) na kuonya watakaoshindwa kufanya hivyo watahatarisha biashara zao.
Ametoa agizo hilo jana alipohutubia mkutano wa hadhara mjini Biharamulo mkoani Kagera wakati wa kuzindua barabara ya Kagoma – Biharamulo – Lusahunga yenye urefu wa kilometa 154, ambayo itasaidia kuifungua Tanzania na nchi za jirani katika ukanda huo wa Magharibi.
Katika maagizo yake, pia amewataka wakuu wa mikoa na wilaya kulisimamia jambo hilo kwa karibu. “Kwa muda mrefu baadhi ya wafanyabiashara wanaoendesha vituo vya mafuta, wamekuwa wakikwepa kodi.
Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata huduma muhimu ikiwemo afya na elimu,” alisema Rais Magufuli. Aliongeza, “Hatuwezi kufanikiwa katika hayo kama baadhi ya wafanyabiashara wanakwepa kulipa kodi na kuacha mzigo mkubwa kwa watumishi wa umma na wakulima kwa miaka yote.”
Dk Magufuli ameiagiza Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, kuhakikisha vituo vyote vya mafuta nchini vinatumia mashine hizo. Alisisitiza kuwa wamiliki watakaokiuka agizo hilo, vituo vyao vifungwe na kufutiwa leseni.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) tangu wiki iliyopita, imeendesha kampeni ya kufungia vituo vya mafuta visivyotumia EFDs baada ya kuwapo makubaliano na wafanyabiashara hao tangu Oktoba mwaka jana kufunga mashine hizo.
Juzi, TRA ilieleza kuwa vituo 710 vya mafuta vilifungwa nchi nzima tangu ianze kazi ya kuvikagua vituo hivyo kuona kama vinatumia EFDS. Aidha, vituo 469 kati ya hivyo vimefunguliwa baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa na TRA na vituo vingine 241 havijafunguliwa kutokana na kushindwa kukidhi masharti ya TRA.
Kwa mujibu wa Rais Magufuli, serikali imeongeza bajeti ya kununulia dawa muhimu kutoka Sh bilioni 31 hadi Sh bilioni 250 na kuongeza kuwa lengo ni kuwafanya Watanzania wengi kupata huduma ya afya kwa gharama nafuu.
Alifafanua kwamba serikali imejenga barabara ya Kagoma-Biharamulo- Lusahunga kwa gharama ya Sh bilioni 190, ambazo zote zimelipwa kutokana na mapato ya ndani na kusema hayo ni mafanikio makubwa.
Alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi tano za Afrika, zilizomudu kujenga barabara kwa kutumia mapato yao wenyewe. Akasisitiza kwamba ni muhimu miundombinu hiyo ikatunzwa. Rais aliwakumbusha Watanzania kuendelea kutunza amani na utulivu uliopo.
Aliwataka wananchi kujifunza kutoka kwa baadhi ya nchi jirani, ambako maelfu ya watu waliuawa kwenye migogoro ya wenyewe kwa wenyewe na hivyo wasiruhusu mambo kama hayo kutokea nchini.
Alieleza kuwa serikali imeondoa kodi na ushuru kwenye mazao ili kuwawezesha watu wa kipato cha chini kuwa huru. Alisema kwamba kodi hizo ndizo zilizowashawishi watu kujiingiza kwenye biashara ya magendo na nchi jirani ya mazao ikiwemo kahawa.
“Mkulima mwenye tani 20 za mazao ya chakula asikodi lori la tani 20 badala yake akodi tu lori la tani moja na hatatozwa kodi,” alisema Rais Magufuli. Aidha, aliwahakikishia wakazi wa Biharamulo kwamba tatizo la maji wanalokabiliana nalo, litatatuliwa hivi karibuni na kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Maji Bukoba Mjini na Mamlaka ya Usafi (BUWASA), Allen Marwa kuhakikisha mkandarasi aliyepewa kazi kufunga kuunganisha mabomba kabla ya Julai 30, mwaka huu.
Aliwaagiza pia Mkuu wa Mkoa, Salum Kijuu na mkuu wa wilaya ya Biharamulo, kuhakikisha mifugo inayozurura kwenye hifadhi za misitu ukiwemo Burigi wanakamatwa. Rais Magufuli aliwataka Watanzania kuwa na idadi ndogo ya mifugo, ambayo itawaingizia fedha na kuongeza kuwa Tanzania bado haijanufaika vya kutosha kutoka sekta ya mifugo.
Pia aliwahakikishia wachimbaji wadogo wa Biharamulo kwamba serikali itawapatia maeneo ya kuchimba dhahabu, inayopatikana katika eneo hilo. Rais Magufuli yuko kwenye ziara ya siku mbili mkoani Kagera na leo atakuwa wilayani Ngara, ambako pia atahutubia mkutano wa hadhara.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa