KAGERA WAHIMIZWA KUJIUNGA NSSF
WANANCHI mkoani Kagera, wametakiwa kujiunga na Shirika la Taifa la
Hifadhi ya Jamii (NSSF), ili waweze kupata mafao bora ikiwemo bima ya
afya bure kwa familia.
Wito huo ulitolewa mjini hapa jana na Meneja wa Mafao ya Matibabu wa
NSSF, Dk. Ally Mtulia, alipokuwa akisoma taarifa ya utakelezaji mkoani
hapa katika siku ya zoezi la upimaji wa afya bure kwa Kanda ya Ziwa.
Dk. Mtula alisema shirika hilo litaendelea kuwahimiza wananchi
kujiunga nalo, kwani kuna mafao mengi wanaweza kunufaika nayo na pia
wanaweza kujipatia mikopo hasa wajasiriamali wadogo, ushirika wa
bodaboda, wakulima kupitia vyama vya akiba na mikopo.
Alisema mbali na kujiunga na NSSF, amewaomba wananchi hao
kujijengea tabia ya kupima afya zao, ili kujiwekea mfumo bora wa maisha
ikiwa ni pamoja na kuepuka magonjwa sugu.
Zoezi la kila mwananchi kupima afya lilianzia mkoani Mara, Shinyanga, Geita ambako watu wengi walijitokeza kupima afya zao.
Chanzo:Tanzania Daima
WAVUVI WALALAMIKIA POLISI
WAVUVI wa Kisiwani Mazinga, Kata ya Mazinga wilayani Muleba,
Kagera, wamelilamikia Jeshi la Polisi kwa kutoweka ulinzi wa kutosha
katika Ziwa Victoria hali inayosababisha wavuvi hao kufanyiwa vitendo
vya uhalifu na kuuawa.
Walisema hayo jana walipozungumza na waandishi wa habari baada
ya kuona jeshi hilo halichukui hatua kuhusu taarifa za kunyang’anywa
zana zao za uvuvi, zikiwemo injini za boti katika tukio la hivi
karibuni.
Mvuvi Misana Ramadhani mkazi wa mwalo wa Kimoyomoyo, Kijiji cha
Mazinga, alisema hivi sasa wamechoshwa na vitendo vya uhalifu
wanavyofanyiwa kila mara.
Thomas Josia ambaye ni mmiiki wa mitumbwi, alisema serikali wakati wa
kutoza kodi mbalimbali inakuwa ya kwanza kufika visiwani na wavuvi
wanakuwa mstari wa mbele kulipa kodi, lakini suala la usalama wao
haijali.
“Rais Kikwete wakati wa ahadi zake alisema atapambana na uhalifu
katika sekta ya uvuvi, lakini tunashangaa hakuna kinachoendelea hadi
sasa badala yake tunazidi kuporwa mali zetu… tutaishije wakati ulinzi
unapelekwa nchi nyingine wazawa tunateseka?” alihoji Josiah.
Diwani wa Mazinga, Alex Bakenjela, alisema baada ya Jeshi la Polisi
kuona kilio cha wavuvi hao, limekubali na kushauri kuwepo kwa polisi
jamii watakaobaini chanzo cha tatizo.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, George Mayunga, alisema hajapata
taarifa hiyo kutoka wilayani, huku akiahidi kufuatilia suala hilo.
Chanzo;Tanzania Daima
'PAMBANENI NA UVUVI HARMU'
WANANCHI wa Wilaya ya Muleba, mkoani Kagera, wametakiwa kutumia
elimu wanayopewa na maofisa uvuvi kupambana na kutokomeza uvuvi haramu,
ili kuokoa kuangamia kwa Ziwa Victoria.
Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Ofisa Uvuvi Wilaya ya Muleba, Siymphorian Ngaiza, alipozungumza na Tanzania Daima ofisini kwake, kutokana na kuongezeka kwa vitendo vya uvuvi haramu katika ziwa hilo.
“Jamii ina wajibu mkubwa wa kudhibiti vitendo vya uvuvi haramu kwa
vile wao ndio wanaoishi na wavuvi wenye tabia kama hizo,” alisema.
Alisema kuwa aina ya uvuvi haramu ulioshamiri katika Wilaya hiyo ni
ule wa kutumia nyavu zisizoruhusiwa ambazo ziko chini ya kiwango na
zinazonasa samaki wadogo.
Aliwataka wavuvi kuzingatia sheria zilizopo ikiwa ni pamoja na
kulipia ushuru wa usafirishaji wa samaki ili kuepuka usumbufu
unaojitokeza wa kukamatwa.
Pia aliwashauri wakazi wa visiwani humo kuanzisha ulinzi shirikishi,
ili kuwabaini wageni wanaojihusisha na vitendo vya wizi wa injini na
zana nyingine za uvuvi na kuwafikisha katika kituo cha polisi.
Chanzo:Tanzania Daima
WATAHADHARISHWA KUEPUKA MAGONJWA
WAKAZI wa Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, wametakiwa kuchukua
tahadhari dhidi ya ugonjwa wa malaria ili kupunguza idadi ya vifo vya
watoto na wajawazito.
Kauli hiyo imetolewa jana na Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya, Leontine
Rwamulaza wakati akihojiwa na Tanzania Daima ofisini kwake
kuhusiana na mlipuko wa magonjwa wilayani kwake.
Rwamulaza alisema wilaya hiyo inaongoza kwa ugonjwa huo katika Mkoa
wa Kagera, na hivyo akawataka wananchi kuzingatia sheria na masharti
ambayo wanakuwa wanapewa na wataalamu wanazunguka katika vijiji.
Alisema wamechukua hatua za kupambana na ugonjwa huo kwa kuanzisha
utaratibu wa kutembelea vijiji kupima kila mtu na ambae anabainika kuwa
na ugonjwa huo hupewa dawa ikiwa ni pamoja na kutakiwa kuweka
mazingira safi ili kuondoa mazalia ya mbu.
“Wilaya yetu ni kati ya wilaya tisa hapa nchini zinazoongoza kwa
ugonjwa huu, na hii inatokana na kuwa na mito inayoaminika kuwa na mbu
wengi na ambayo pia wananchi wanaishi karibu nayo,” alisema.
Chanzo:Tanzania Daima
CUF YAHIMIZA WANACHAMA KUWANIA UONGOZI
CHAMA cha Wananchi (CUF) Wilaya Bukoba Mjini, mkoani Kagera,
kimewataka wanachama na wakereketwa wa chama hicho kuhamasishana kukipa
nguvu chama pamoja na kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi
katika uchaguzi wa serikali za mitaa baadaye mwaka huu.
Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa la
CUF, Saverina Mwijage, alipokuwa akitoa salamu kwa wajumbe wa mkutano
mkuu wa wilaya uliofanyika katika Manispaa ya Bukoba.
Mwijage ambaye pia aliwahi kuwa Mbunge wa Viti Maalumu, aliwataka
wananchi wilayani Bukoba kutokata tamaa na badala yake wakitetee chama
mbele ya Watanzania.
“Kwa kuwa uchaguzi wa serikali za mitaa unakaribia, nawaomba wapenzi,
wakereketwa na wananchi wote kwa ujumla kuanza kujiandaa kwa kuwabaini
wanachama ambao wanaweza kujitokeza kuwania nafasi za uongozi, kwani
msingi wa chama cha siasa kuwa na nguvu ni kuanzia kuchukua madaraka
katika serikali za mitaa,” alisema.
Alisema kwa kipindi ambacho amekuwa nje ya Bunge, kuna mambo mengi
amejifunza yanayohusu maendeleo ya wananchi wa Bukoba na
yanayomshawishi kuanza kuhamasisha wananchi wa Bukoba kupigania chama,
ili kiweze kuwainua kiuchumi wananchi.
“Bukoba imegubikwa na migogoro kila siku, wananchi hawapati kile
kilichotarajiwa. Migogoro haimsaidii mwananchi, mimi nimeazimia
kusaidiana na chama changu kutatua kero hizo,” alisisitiza Mwijage.
Katibu wa CUF Wilaya ya Bukoba Mjini, Ramadhan Bahati, aliwataka
vijana, wanawake na wapenzi wa CUF wilayani humo kuanza kurudisha nguvu
ya chama hicho kuanzia ngazi za kata.
Alisema dhamira ya chama hicho ni kurudisha nguvu kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Chanzo:Tanzania Daima



























































