Home » » Rweikiza Cup kutimua vumbi Machi 25

Rweikiza Cup kutimua vumbi Machi 25

KITIMUTIMU cha kumtafuta bingwa wa Kombe la Rweikiza kinatarajiwa kuanza kutimua vumbi Machi 25, mwaka huu na kushirikisha vijiji 92 vya Jimbo la Bukoba Vijijini, mkoani Kagera.
Kombe hilo litaanza kwa mchujo kuanzia ngazi za vijiji na hatimaye kata na kumpata mshindi wa kwanza, ambako zawadi kwa washindi zinatarajiwa kutajwa hivi karibuni na waandaaji wa mashindano hayo.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara kwenye Kijiji cha Kishogo juzi, Katibu wa Michezo wa Jimbo hilo, Cajethanus Charles, alisema tayari mchakato umekamilika na kwamba, Machi 25 michuano itaanza katika vijiji mbalimbali na hatimaye kumpata mshindi wa kombe hilo maarufu kwa jina la Rweikiza Cup.
Hata hivyo, aliwataka viongozi walioteuliwa katika maandalizi hayo kuanza kuwaandaa vijana vema ili michuano iwe na mvuto zaidi kwa kupata pia mashabiki wengi wa kuiangalia.
Naye Mbunge wa Jimbo hilo ambaye ndiye muandaaji wa mashindano hayo, Jasson Rweikiza, alisema tayari amenunua mipira zaidi ya 1,000 na jezi za kugawa kwa timu zote katika vijiji husika, sambamba na mabasi mawili ambayo yatatumika kubeba wachezaji pamoja na dawa mbalimbali, hivyo wachezaji wanatakiwa kukaa mkao wa kula tayari kwa mashindano hayo.
Alibainisha kuwa amekuwa akifanya hivyo mara kwa mara lengo likiwa ni kujenga umoja baina ya vijana waliopo kijijini humo na hata kuwafanya wawe katika hali ya kuwaza michezo na si kuwaza kujiingiza katika mambo mabaya ambayo katika jamii hayana nafasi.
Pia alisema Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kwa sasa lipo katika mchakato wa kusaka vipaji katika wilaya mbalimbali, hivyo ingekuwa vema wakafika katika ligi hiyo ambayo anaamini vijana wake wana vipaji ili waweze kutangazika.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa