Home » » WASSIRA: SERIKALI HAINA AJIRA ZA KUTOSHA KWA VIJANA

WASSIRA: SERIKALI HAINA AJIRA ZA KUTOSHA KWA VIJANA




Vijana kote nchini wametakiwa kubuni mbinu mbadala ya kujiajiri wenyewe ili waweze kujikwamua katika umaskini, badala ya kutegemea ajira za serikali pekee ambazo hazitoshelezi mahitaji yaliyopo.

Rai hiyo imetolewa na waziri ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira wakati akikagua miradi ya mfuko wa maendeleo ya jamii nchini (TASAF) katika wilaya ya Ngara.

Waziri Wassira alisema kuwa serikali haina uwezo wa kuajiri vijana wote hapa nchini,  inachokifanya ni kubuni namna wananchi watakavyotumia fursa zilizopo kujiajiri kupitia sekta mbalimbali hasa ya kilimo.

Miongozi mwa miradi ya Tasaf aliyoitembelea ni pamoja na mradi wa kikundi cha vijana 25 walioibua mradi wa kufuga mbuzi  katika kijiji cha Ibuga kata Kabanga, ambao wamejiinua kiuchumi kupitia mradi huo.

Akisoma risala katibu wa kikundi hicho Bahati Philmon, amesema kuwa  baada ya kuona kupata ajira za serikali kumeshindikana, wao kama vijana walijiunga katika kikundi na kupatiwa fedha kutoka Tasaf kwa ajili ya kuanzisha mradi huo wa ufugaji wa mbuzi, ulioibuliwa katika mkutano wa hadhara mwaka 2009.

Philmon amesema kuwa  walipata shilingi milioni 11 kutoka Tasaf, na kununua mbuzi 105, ambapo  kila mmoja wao alipata mbuzi wanne, na kuwa sasa wana jumla ya  mbuzi 200, na kila mmoja amekwishafikisha mbuzi kumi.

Amesema kuwa jumla ya gharama ya mradi huo ni zaidi ya shilingi milioni 12.5 na kuwa mbali na fedha zilizotolewa na Tasaf, wananchi walichangia nguvu zao zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 1.5.

Amesema kuwa kutokana na ufugaji huo vijana  kumi miongoni mwao wameweza kuanzisha kilimo cha mazao mbalimbali katika shamba lenye ukubwa wa ekari nane, ikiwamo mashamba ya migomba ya kisasa, kahawa na magimbi.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa