Home » » Wahamiaji warudi kwa kasi Kagera

Wahamiaji warudi kwa kasi Kagera

Katika hali isiyo ya kawaida, wahamiaji haramu waliorejeshwa nchini mwao na serikali katika ‘Operesheni Kimbunga’ wameanza kurejea kwa wingi katika Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera wakijiita M23 na kupora mali za wananchi kwa nguvu.
Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhandisi Benedict Kitenga, aliyasema hayo jana wakati akitoa taarifa kwa Mkuu wa Mkoa huo Kanali mstaafu, Fabian Massawe ambaye alitembelea wilaya hiyo kukagua shughuli za maendeleo na ujenzi wa maabara katika shule za sekondari za kata.
Alisema wahamiaji hao wamejazana katika Kijiji na Kata ya Kibingo wakiwatisha wananchi ambao hivi sasa wanahofia usalama wa maisha yao na mali zao.
Aliongeza kuwa, baada ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya kupata taarifa hizo, ilikwenda eneo la tukio na kufanya operesheni kubwa na kufanikiwa kukamata wahamiaji haramu zaidi ya 20 na baadhi ya Watanzaia waliokuwa wakiwahifadhi.
Mhandisi Kitenga alisema baada ya kukamatwa, wahamiaji hao walirudishwa katika nchi zao bila kutaja uraia wao na Watanzania waliohusika kuwahifadhi wamechukuliwa hatua za kisheria.
“Kutokana na hali ilivyo, wananchi wanapaswa kutoa taarifa wawaonapo wahamiaji haramu katika maeneo yao,” alisema.
Kwa upande wake, Bw. Massawe alisema, katika “Operesheni Kimbunga”, wahamiaji haramu walirudishwa katika nchi zao, lakini operesheni hiyo inaendelea ili kuhakikisha waliobaki wanakamatwa na kurudishwa nchini mwao.
“Chini ya Kaulimbiu ya Hakuna wa Kubaki na Hakuna wa Kurudi, tutahakikisha kila mhamiaji haramu anaondoka na Watanzania ambao watabainika kushirikiana nao pia watachukuliwa hatua za kisheria.
“Naiagiza Kamati za Ulinzi na Usalama kuendelea na operesheni hadi wahamiaji haramu wamalizike,” alisisitiza Bw. Massawe na kuwataka wananchi watoe taarifa kwa viongozi wanapowaona na kutoa namba zake za simu.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi waliohojiwa walisema tatizo la wahamiaji haramu linachangiwa na baadhi ya watendaji wa Serikali ngazi za chini ambao wanachukua hongo na kuwarudisha.
Walisema inavyoonekana, viongozi wa chini kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji hadi kata, wamepewa mamlaka makubwa pia wamekuwa wakikaa muda mrefu bila kubadilishwa vituo vya kazi na hivyo kujenga mazoea na wahamiaji hao.
“Serikali kuanzia ngazi ya Wilaya, iwe na utamaduni wa kuwatembelea viongozi wa vitongoji na kata kwa kushtukiza ili kukomesha tabia hii ambayo wamejijengea na kuonekana miungu watu katika maeneo yetu,” alisema mkazi wa eneo hilo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini.
Hivi karibuni Serikali ilifanya “Operesheni Kimbunga” na kushirikisha vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama baada ya Rais Jakaya Kikwete kutoa wiki mbili kwa wahamiaji haramu wawe wameondoka nchini kwa hiari yao.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa