Home » » Wanasiasa wamchefua January Makamba

Wanasiasa wamchefua January Makamba

image

Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Bw.January Makamba, amekemea tabia ya baadhi ya wanasiasa nchini kutumia mkondo wa dini kisiasa kwani hilo ni kosa
kubwa kwa mustakabali wa amani ya nchi.

Bw. Makamba aliyasema hayo juzi Mjini Bokoba, mkoani Kagera, wakati akizungumza kwenye Tamasha la Amani ambalo liliandaliwa na Nazareth Singers kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Alisema wanasiasa wenye tabia hiyo wanaamini kuwa waumini wa dini yake watamuunga mkono katika uchaguzi jambo ambalo ni hatari kwa sababu anapogombea uongozi, wananchi ndio wanaopiga kura bila kujali dini zao.

Aliongeza kuwa, viongozi wa dini wamefanya kazi kubwa ya kulinusuru Taifa kutokana na chokochoko za kidini kupitia mahubiri yao kwani bila wao, hali ingekuwa mbaya zaidi.

Aliwaomba viongozi wa madhehebu ya dini nchini, kuendelea kuhubiri amani, upendo na mshikamano miongoni mwa Watanzania ili kudumisha amani iliyoasisiwa na Hayati Julius Nyerere.

"Baada ya kuibuka kwa chochoko za kidini nchini, viongozi wa dini wamefanya kazi kubwa ya kuhubiri amani, upendo na mshikamano miongoni mwa wananchi...mahubiri yao
yamesaidia kupunguza chokochoko hizo," alisema.

Bw. Makamba alisema madhara ya Taifa kukosa amani ni makubwa na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuheshimu imani za watu wengine.

Alikemea tatizo la ukosefu wa haki na usawa katika jamii juu ya upatikanaji wa huduma mbalimbali za msingi ikiwemo elimu na afya miongoni mwa Watanzania.

"Unapoona katika jamii hakuna haki na usawa hilo ni tatizo,kwa mfano, ukiona kuna watu wanapata elimu au huduma tofauti na wanayopata wengine, uhakika wa amani
unakuwa hatarini," alisema.

Aliwapongeza waandaaji wa tamasha hilo ambalo liliwakutanisha waumini wa dini mbalimbali mkoani humo na kusisitiza kuwa, ujumbe uliotolewa usambazwe nchi nzima.

Aliahidi kusaidiana na waandaaji hao kuhakikisha ujumbe huo wa amani unafika maeneo mbalimbali nchini.

Awali Mkuu wa Mkoa huo, Kanali mstaafu Fabian Massawe,alisema amani ya Tanzania ipo mashakani kutokana sababu mbalimbali kama malumbano ya kidini, kisiasa, matumizi ya dawa za kulevya kwa unyanyasaji wa kijinsia.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa