Home » » HARAMBEE YABUGADEA YAKUSANYA MIL.8/-

HARAMBEE YABUGADEA YAKUSANYA MIL.8/-

SHILINGI milioni 8.8 zimekusanywa katika harambee ya kuchangia ujenzi wa Kituo cha Afya cha Buganguzi, wilayani Muleba iliyoratibiwa na Umoja wa Maendeleo ya Buganguzi (Bugadea).
Akizungumza katika harambee hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki, Mwenyekiti wa umoja huo ulioasisiwa na wakazi wa Kata ya Buganguzi waishio Dar es Salaam, Rodrick Lutembeka, alisema kiasi hicho kilitokana na michango ya wananchi, pia ofisi  ya mkuu wa mkoa imechangia  sh milioni 1.8 na ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muleba imeahidi kuchangia sh milioni 30.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Fabian Massawe, aliyekuwa mgeni rasmi kwenye harambee hiyo iliyofanyika kwenye makao makuu ya kata hiyo, amehimiza wakazi mkoani humo kuepuka tabia ya kusubiri misaada na badala yake  wachangie miradi ya maendeleo katika maeneo yao.
Alisema juhudi za wananchi lazima zionekane kwanza katika miradi yao kabla ya kuomba misaada.
Alisema ni aibu kuomba misaada kwenye utekelezaji wa miradi mbalimbali hata kwa vitu ambavyo viko ndani ya uwezo wa wananchi.
Massawe alisema miradi mingi ya maendeleo katika Wilaya  ya Muleba ukiwemo ujenzi wa vyumba vya madarasa, haikutekelezwa kwa kasi ya kuridhisha kwa kile alichodai ni wananchi kurubuniwa na kushindwa kuchangia nguvu zao.
Katika kuhamasisha ujenzi wa Kituo cha Afya Buganguzi kinachokadiriwa kugharimu zaidi ya sh milioni 600,  Mkuu wa Mkoa ameshauri kila kaya kuchangia sh 20,000 au vitu vyenye thamani hiyo, ili kufikia lengo la kata hiyo kuwa na huduma hiyo.
Alipongeza wakazi wa Buganguzi walioko nje ya mkoa  chini ya mwavuli wa Bugadea kwa kuwa na wazo la kukumbuka nyumbani na kushiriki kuchangia maendeleo. Kata ya Buganguzi iliyo katika Tarafa ya Nshamba, ina vijiji vya Buhanga, Bushemba, Katare na Kashozi.
Mwenyekiti wa Bugadea, Lutembeka, alihimiza wakazi wa kata hiyo kuunganisha nguvu katika ujenzi wa kituo hicho na miradi mingine ya maendeleo.
Alisema hakuna sababu  ya kushindwa kufanya hivyo kwa kuwa fursa zilizopo,  ikiwemo ardhi na rasilimali  vinatosheleza kutekeleza ujenzi huo.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Rembris Kipuyo, alisema serikali itaendelea kushirikiana na wananchi wa kata hiyo hadi kukamilika kwa kituo hicho.
Diwani wa Buganguzi, Onesmo Yegira alipongeza uamuzi wa Bugadea kuandaa tamasha hilo la maendeleo lililopambwa na burudani pamoja na michezo mbalimbali ikiwa ni njia ya kukutanisha wakazi kuchangia maendeleo. 
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa