Home » » Ndege wa ajabu waanza kuteketezwa Bukoba

Ndege wa ajabu waanza kuteketezwa Bukoba

Wananchi katika Kisiwa cha Musira mkoani Kagera wameanza kuteketeza ndege waliodaiwa kutoa kinyesi chenye sumu, huku Wizara ya Afya na Ustawi wa jamii ikiendelea kukalia majibu ya utafiti kuhusu ukweli wa madai hayo.
Wizara iliahidi ingetoa majibu ya utafiti huo mapema.
Gazeti hili lilishuhudia idadi kubwa ya viota vilivyokuwa na vifaranga na mayai ya ndege hao waliodaiwa kuwa wa ajabu vikiwa vimeharibiwa.
Awali ilielezwa kinyesi chao kilidaiwa kuwa na sumu kali iliyohusishwa na vifo vya mifugo.
Mmoja wa wananchi katika kisiwa hicho Jackson Robert ambaye alikutwa akikata matawi yenye viota ili kuharibu mazalia ya ndege hao alisema wananchi walikubaliana kuwaangamiza ndege hao ili kuepuka madhara yaliyojitokeza.
“Hawa ni viumbe wa ajabu sana, kinyesi chao kina sumu kali kwani kikianguka kwenye bati zinatoboka baada ya muda mfupi, lakini pia wanyama wakila kinyesi hicho hufa,” alisema mkazi huyo.
Awali, Mkuu wa Mkoa huo Kanali Mstaafu Fabian Massawe alithibitisha ndege hao kuvamia kisiwa hicho na baadaye Wizara ya Afya kutuma watafiti kuchunguza ukweli wa madai ya ndege hao kutoa kinyesi chenye sumu.
Ilidaiwa ndege hao pamoja na kinyesi chao kutoboa mabati pia kuku 516 na mbuzi 12 walikufa katika mazingira yaliyohusishwa na ukali wa kinyesi chenye sumu kilichosababishwa na ndege hao.
Hata hivyo gazeti hili lilipomtafuta Dk. Munda Elias ambaye aliongoza utafiti huo kutoka Wizara ya Afya kutaka kupata majibu ya utafiti huo, mtaalamu huyo alikata simu na kuendelea kufanya hivyo kila alipotafutwa.
Hata baada ya kutumiwa ujumbe mfupi wa maandishi kwa njia ya simu kuhusu nia ya kufahamu matokeo ya utafiti huo, hakuna jibu lolote lililotolewa pamoja na kuwa ndiye aliyefika katika kisiwa hicho na kuchukua sampuli za ndege hao kwa ajili ya chunguzi zaidi wa kimaabara.
Pia mtafiti huyo wa wanyama na ndege baada ya kufika katika kisiwa hicho wiki chache zilizopita aliwaeleza wananchi kuwa wamefika kuangalia ukubwa wa tatizo na kuwataka watoe ushirikiano ili kupata ufumbuzi wa madai yao.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa