Home » » SHULE YA MUGEZA MSETO HAINA VYOO

SHULE YA MUGEZA MSETO HAINA VYOO

SHULE ya Msingi Mugeza Mseto inakabiliwa na ukosefu wa vyoo na bafu kwa wanafunzi wenye ulemavu wa viungo.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Philemon Coelestine, alibainisha hayo juzi alipokuwa akitoa taarifa ya shule kwa Balozi wa China nchini aliyetembelea shule hiyo na kutoa vitabu vyenye thamani ya sh milioni tano.
Coelestine alisema mabweni yanayotumiwa na wanafunzi ambao ni walemavu hayakidhi mahitaji ya wahitaji.
Alisema changamoto nyingine ni uhaba wa nyumba za watumishi, usafiri kwa wanafunzi na uchakavu wa miundombinu ya majengo, umeme na viwanja vya michezo.
Alisema shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 650 kati yao walemavu wasioona 40, walemavu wa ngozi ni 40 na walemavu wa viungo ni 52.
Hata hivyo alisema pamoja na changamoto hizo shule hiyo imekuwa ikiendelea kufanya vizuri katika matokeo ya kumaliza elimu ya msingi kwa miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka 2010/13.
Alisema mwaka 2013 wanafunzi waliofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi walikuwa 66, kati yao wanafunzi 40 ambayo ni asilimia 61 walichaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza.
Balozi wa China Tanzania, Dk. Lu Youging, alisema wanafunzi wenye ulemavu wanao uwezo wa kujitegemea na kutoa mchango wao kwa maendeleo ya taifa.
Aliwashauri wanafunzi hao kusoma kwa bidii ili waweze kufanya vizuri katika masomo yao.
Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Bukoba, Ado Mapunda, alisema atasimamia msaada huo uliotolewa na Ubalozi wa China ili utumike kwa malengo yaliyokusudiwa.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa