Home » » Kamanda CHADEMA auawa

Kamanda CHADEMA auawa

KATIBU wa Baraza la Wanawake wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAWACHA) Kata ya Runazi, Wilaya ya Biharamulo, mkoani Kagera, Oliva Evodius, ameuawa kwa kukatwa mapanga na watu wasiojulikana.
Kifo hicho ambacho kimeacha maswali mengi, kinahusishwa na mambo ya siasa, lakini pia wapo wanaokihusisha na mambo binafsi.
Akizungumza na gazeti hili jana,  Diwani wa Kata ya Runazi, Constantine N’kwenge, alisema kuwa katibu huyo ameuawa usiku wa kuamkia Jumamosi Aprili 6, majira ya saa nne usiku baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana na kumshambulia kwa mapanga  akiwa nyumbani kwake.
Mume wa marehemu, Evodius Malembeka, aliliambia gazeti hili kuwa marehemu alikutwa na tukio hilo akiwa naye.
Alisema Oliva alivamiwa wakati akiingia chumbani mwake akitokea bafuni kuoga.
Msemaji wa familia hiyo, Raphael Sostenes Zitta, ameitaka serikali kupitia vyombo vya usalama kuimarisha ulinzi na kuongeza umakini katika uchunguzi wa matukio ya mauaji yanayofanyika na kuhatarisha usalama wa wananchi.
Jeshi la Polisi mkoani Kagera, limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba linawashikililia watu wawili wakati likiendelea kufanya uchunguzi zaidi kubaini wahusika wa mauaji hayo.
Wakati huo huo, watu wawili wamelazwa katika hospitali teule wilayani hapa baada ya kujeruhiwa katika matukio tofauti yaliyotokea mwishoni mwa wiki iliyopita.
Muuguzi wa zamu katika Hospitali hiyo, Haula Balikaho, amewataja waliojeruhiwa kuwa ni Frank Wera Mussa,  mkazi wa Runazi na Chola Rufungulo, mkazi wa Kisenga, Kata ya Nemba, wilayani humo.
Alisema Frank amejeruhiwa kichwani baada ya kupigwa na wananchi wenye hasira wakati Chola amejeruhiwa jicho la kulia baada ya kupigwa risasi na majambazi akitokea kwenye mnada wa ng’ombe.
Haula alisema hali za majeruhi  zinaendelea vizuri na wanaendelea kupata matibabu katika hospitali hiyo na mmoja wa majeruhi hao, Frank Mussa, anatibiwa chini ya uangalizi wa polisi.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa