Home » » Wakazi Missenyi wawahofia askari wa Uganda

Wakazi Missenyi wawahofia askari wa Uganda

WATANZANIA waishio mpakani mwa nchi za Tanzania na Uganda  eneo la Mtukula lililopo wilayani Missenyi, Kagera, wamesema  wamechoshwa na vitendo vinavyofanywa na askari wa Uganda kuingia upande wa Tanzania  kukamata wahalifu wakiwa na silaha bila kufuata  sheria.
Wakizungumza na waandishi wa habari kwa masharti ya kutotajwa majina, wananchi hao walisema juzi, saa 11 jioni askari wanne waliotokea Mbalala, Uganda walivuka mpaka kuwafuatilia wezi wa pikipiki waliokuwa upande wa Tanzania.
Walisema katika kurupushani za kuwakamata watuhumiwa  hao walikimbia  na kuingia ndani ya Kituo cha Polisi Mtukula kilichopo Tanzania.
Walisema wakati mtuhumiwa huyo akikimbilia katika kituo hicho, askari hao walianza kumfyatulia risasi ambazo hazikumpata mlengwa na badala yake kuwajeruhi  watu  wawili.
Walisema baada ya askari huyo kuingia katika kituo hicho cha polisi, alikamatwa na kunyang’anywa bunduki huku wenzake watatu walipoona mwenzao amekamatwa waliondoka na vijana wawili ambao ni Watanzania kuelekea nao Uganda.
Wananchi hao walisema imekuwa ni kawaida kwa askari wa Uganda kuingia  upande wa Tanzania na kuwakamata watu wanaowatuhumu na kuwapeleka Uganda  bila kufuata utaratibu wa mipaka.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kagera, George Mayunga, alipohojiwa kuhusiana na tukio hilo alisema hayuko tayari kulizungumzia suala hilo linalogusa nchi mbili.
Alisema tukio hilo linashughulikiwa na vyombo vya ulinzi na usalama, ili taarifa zitumwe Makao Makuu ya Jeshi la Polisi.
Chanzo ;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa