MKURUGENZI MULEBA AJIKAANGA

KITENDO cha Mkurugunzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, Joseph Mkude cha kuwafukuza waandishi wa habari na wananchi katika vikao vya Baraza la Madiwani, kimelaaniwa na Mkuu wa wilaya hiyo na madiwani.
Mkurugenzi huyo anadaiwa kukiuka kanuni ya kudumu namba 12 kifungu (1) na cha (2) inayowaruhusu wananchi kuhudhuria vikao hivyo vya wazi.
Mdiwani hao ambao walitishia kususia na kuhairishwa kwa kikao cha baraza cha Oktoba 31 mwaka huu, walimtaka mkurugenzi huyo, kurejea matangazo yake aliyoyabandika katika mbao za matangazo za halmashauri hiyo.
Tangazo hilo lilisomeka hivi; “Tangazo la mkutano wa Baraza la Madiwani. Napenda kuwatangazia wananchi wote  wa Wilaya ya Muleba kuwa mkutano wa Baraza la Madiwani utafanyika tarehe 30/10/ hadi 31/10/2014, kuanzia asubuhi katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri”.
Kwa mujibu wa tangazo hilo lenye kumb. namba KGR/HW/ML/.A.33/Vol.X/19, wananchi walikaribishwa kusikiliza kinachojadiliwa katika baraza hilo.
Hata hivyo, pamoja na tangazo lake hilo, Mkude aliingia ukumbini Okoba 30 mwaka huu, na kuwakuta wananchi pamoja na waandishi wa habari waliokuwa wamehudhuria kikao hicho, watoke nje, jambo lilipingwa vikali na madiwani.
Amri hiyo ya mkurugenzi, iliwafikisha waandishi kwa mkuu wa wilaya hiyo, Lembris Kipuyo na kumweleza yaliyojiri ambapo aliwataka kuwa wavumilivu wakati akiendelea kulishughulikia.
“Hata mimi sijapendezwa na kitendo hicho, kikao cha Baraza dogo ndio chenye habari nyingi na nzuri zinazohusu wananchi, unajua mimi huwa nawaambia viongozi wenzangu na watendaji wetu kuwa Muleba hii ina watu zaidi ya laki tano, sasa leo tukitaka wananchi wajue serikali yao imefanya mambo fulani lazima tutumie vyombo vya habari.
“Hata Rais Kikwete wakati tuko Dodoma katika semina elekezi mwaka 2006, alitueleza kuwa tukitaka mafanikio lazima tufanye kazi kwa karibu na vyombo vya habari, leo mkurugenzi amejisahau, nitamuita nimweleze,”alisema Kipuyo.
Alisema kuwa Muleba ikiharibikiwa pia naye ataharibikiwa kwa sababu kikao hicho kiko wazi, hivyo hakuna haja ya kuwafukuza waandishi kwani niwajibu wao kuchukua habari.
Chanzo:Tanzania Daima

WAINGIZAJI SUKARI YA MAGENDO KUSAKWA

SERIKALI imetangaza msako mkali kuwanasa waingizaji na wauzaji wa sukari ya magendo iliyoingizwa nchini na kuzagaa kwenye masoko.
Waingizaji sukari ya magendo kusakwa
Pia, maofisa wote wa Mamlaka ya Mapato na ushuru mwingine kwenye bandari kuu ya Dar es Salaam na watahojiwa.
Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, (Sera), Mwigulu Nchemba, aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya siku moja kwenye kiwanda cha kuzalisha sukari cha Kagera, (KSL), mwishoni mwa wiki, kutokana na taarifa ya kiwanda kwamba, sukari inayoingizwa nchini kimagendo na hailipiwi ushuru, imekuwa tishio kwa ustawi wa kiwanda hicho.
Akijibu kilio cha kiwanda hicho kilichoko wilayani Misenyi mkoani Kagera, Nchemba alisema; “Tutawasaka waingizaji, maofisa wetu wa TRA walioshughulika kupitisha sukari hiyo bandarini na wote wanaouza sukari hiyo.”
Nchemba, aliongeza kuwa msako huo utakuwa endelevu na wote watakaokamatwa watafikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
“Kiwanda hiki cha Kagera Sugar, ni mfano mzuri wa viwanda vilivyobinafsishwa na ambavyo vinafanya vizuri, kutokana na uwekezaji wake na uzalishaji, hatuwezi kukubali kiwanda hiki kife wakati kinachangia pakubwa katika jitihada za serikali kuwapatia watanzania zaidi ya 4,000 ajira na kodi,” alifafanua.
Awali, akitoa taarifa ya kiwanda hicho, Meneja Mkuu, Ashwin Rana, alisema sukari inayoingizwa kwa njia zisizo halali imetapakaa sokoni hapa nchini na matokeo yake, bei ya sukari imeshuka kwa kiwango kikubwa na hivyo kukifanya kiwanda hicho kuuza kwa bei isiyoendana na gharama za uzalishaji.
Waziri Nchemba, ambaye alipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ya uzalishaji ya kiwanda hicho pamoja na huduma za kijamii kama vile hospitali inayohudumia wafanyakazi na wanakijiji wanaozunguka kiwanda hicho, aliupongeza uongozi wa kwa mafanikio hayo makubwa ya uzalishaji sukari kwa njia ya kisasa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa KSL, Seif Ali Seif, alisema kiwanda chake hakiogopi ushindani ulio sawa, wanacholalamikia ni njama za kuua juhudi za kiwanda kuzalisha sukari ya kutosha na yenye kiwango cha juu kukidhi soko la humu nchini na je ya nchi.
Chanzo:Tanzania Daima

BAWACHA: WATUMISHI IBURUZENI SERIKALI MAHAKAMANI

MWENYEKITI wa Taifa wa Baraza la Wanawake CHADEMA (BAWACHA), Halima Mdee
MWENYEKITI wa Taifa wa Baraza la Wanawake CHADEMA (BAWACHA), Halima Mdee, amewataka watumishi wa umma kuiburuza Serikali mahakamani endapo watakatwa mishahara yao kwa ajili ya ujenzi wa maabara bila wao kuridhia kwa maandishi kama sheria ya kazi inavyotaka.
Aidha, amesema kuwa kama Rais Jakaya Kikwete ana dhamira ya dhati ya kuzijenga maabara hizo, basi akate sehemu ya bajeti yake ya kusafiri nje ya nchi ambayo kwa mwaka huu ametengewa sh bilioni 50 azipeleke kwenye ujenzi huo.
Pia, ametaka Serikali kuacha kutoa misamaha ya kodi kwa kampuni kubwa ambazo inakadiriwa kufikia kati sh trilioni 1.5 na 2 kwa mwaka, ili fedha hizo na kodi nyingine zinazokusanywa kwa wananchi zitumike kutekeleza mapango huo.
Mdee, aliyasema hayo juzi wakati akizungumza na umati mkubwa wa wananchi wa Bukoba kwenye uwanja wa mashujaa wa Mayunga, akiwa ameambatana na
Makamu wake, Hawa Mwaifunga, Katibu Grace Tendega na Naibu Katibu, Kunti Yusuph.

Alisema kuwa hawapingani na ujenzi wa maabara hizo ambazo zinasomesha watoto wengi wa wananchi maskini, ila wanachokataa ni utaratibu mbovu unaotumika kukusanya fedha kwa nguvu kwa kukamata mishahara ya watumishi wa umma.
Alisema kuwa taarifa ya msimamizi na mkaguzi mkuu wa serikali, (CAG), inaonyesha kuwa kwa mwaka wa fedha uliopita, kumefanyika ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma, ambako mishahara hewa ilikuwa trilioni 1.6, jambo alilohoji ni kwa nini serikali isizibe mianya hiyo ili fedha hizo zikatumika kujenga maabara hizo.
“Tusiwape mzigo walimu, tusiwape mzigo mapolisi, tusiwape mzigo manesi wala tusiwatese wananchi wetu kwa watendaji kuwakimbiza na fimbo wakiwadai michango ya ujenzi wa maabara, wakati fedha unazo wewe Rais (Kikwete), na serikali yako… zitoeni zitumike kufanya maendeleo ya nchi ….
“Mimi nilikuwa mtumishi wa Wizara ya Kazi na Ajira, sheria ya kazi namba 28 ya mwaka 2004 ya mahusiano makazini, inasema ni marufuku kwa mtu yeyote kumkata mtumishi wa umma mshahara wake mpaka pale mtumishi huyo atakaporidhia kwa maandishi… hivyo mapolisi, manesi, waalimu mkikatwa mishahara mnaweza kuishitaki serikali mahakamani,” alisema Mdee.
Tendega awataka wananchi kuwa majasiri
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa BAWACHA, Grace Tendega aliwataka wananchi hao kuwa majasiri kwa kuhakikisha wanafanya maamuzi sahihi ya kuwang’oa CCM madarakani kupitia sanduku la kura, zoezi wanalopaswa kulifanya kuanzia Desemba 14 mwaka huu kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa.
Alisema kuwa, njia rahisi ya kuwang’oa CCM ni kuanza kuwakataa kuanzia ngazi za chini ili iwe rahisi kuwatoa madarakani mwakani kwenye uchaguzi mkuu.
Tendega, aliwataka wagombea wa CHADEMA watakaosimama kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwenye uchaguzi huo, wahakikishe ni wale wenye umri wa miaka zaidi ya 21 kama sheria inavyoeleza ili waepuke kuondolewa kwa kukosa sifa, hivyo kufanya mgombea wa CCM apite bila kupingwa.
Mwaifunga: Wanawake msikubali kuwa madaraja
Makamu Mwenyekiti wa BAWACHA Taifa, Hawa Mwaifunga, aliwataka wanawake kukataa kutumika kama madaraja ya kuwaingiza madarakani viongozi wa CCM, ambao miaka yote wamekuwa wakiacha kuwatatulia matatizo yao.
Alisema kuwa, kila inapokaribia uchaguzi wanawake huonekana lulu kwa wawania uongozi wa CCM, ambao huwaendea na vijizawadi vidogo kama sukari, kanga na vilemba, ambavyo huwarubuni navyo ili wafikie malengo yao ya kuukwaa uongozi na baada ya hapo hawawakumbuki tena.
“Ifike mahali wanawake muwaambie CCM imetosha, wametufanya daraja kwa muda mrefu sana kuvuka, lakini hatuoni mafanikio wala mabadiliko yoyote, zaidi maisha yanazidi kuwa magumu huku kukiwa hakuna huduma muhimu za jamii, mahospitalini tunazalia chini, hivyo imetosha na msiwape kura chaguzi zote zinazokuja,” alisema Mwaifunga.
Kunti: Ni ajabu taifa tajiri wananchi wake maskini
Naye Naibu Katibu Mkuu wa BAWACHA Taifa, Kunti Yusuph, alisema kuwa hakuna Mtanzania maskini ambaye hajui maumivu ya kuiweka CCM madarakani, kwani wakati nchi ni tajiri kwa kuwa na rasilimali nyingi, lakini wananchi wake wengi ni maskini wa kutupwa wasioweza hata kumudu milo mitatu kwa siku.
Alisema kuwa ni aibu kwa Taifa hili tajiri kwa kuwa na gesi asili, uraniam, dhahabu, tanzanite na mbuga nzuri za wanyama viongozi wake kugeuka ombaomba kwa kuzunguka nchi mbalimbali wakiomba misaada, jambo alilodai kuwa linasababishwa na kuweka madarakani viongozi wabinafsi na wezi.
Chanzo:Tanzania Daima

MAMIA WAJITOKEZA KUMZIKA KWA HESHIMA KUBWA MKE WA JAJI JOHN RUHANGISA ALIYEFARIKI KWA AJALI YA GARI JIJINI ARUSHA

 Mke wa Jaji John Ruhangisa, Marehemu Laetitia 
Kokuhangisa Ruhangisa enzi za uhai wake.
 Jaji John Ruhangisa
 Jaji John Ruhangisa (wa pili kushoto), akiwa na watoto wake wakati wa ibada ya mazishi ya mke wake Laetitia Kokuhangisa Ruhangisa iliyofanyika nyumbani kwake katika Kijiji cha Ibwera mkoani Kagera leo jioni. Kutoka kulia ni mtoto wake wa kwanza Moreen, David na Fiona.
 Mapadre 30 wa Kanisa Katoliki wakiwa kwenye ibada 
hiyo ya mazishi.
 Viongozi mbalimbali , majaji, watawa na wananchi 
wakiwa kwenye ibada hiyo.
 Watawa wakiwa kwenye ibada hiyo.
 Waimbaji wa Kwaya ya Kanisa Katoliki Parokia ya Ibwera 
nao walikuwepo kutoa burudani.
 Watoto wa Kanisa Katoliki wanaoshiriki kuongoza ibada mbalimbali wakiwa kwenye ibada ibada hiyo.
 Watoto wa Kijiji cha Ibwera nao walijumuika katika 
mazishi ya mama yao Kokuhengesa.
 Jaji John Ruhangisa akimfariji mtoto wake David.
 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Bukoba, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Hery Mwaibambe akimpa pole  mtoto wa marehemu, David.
 Hii ndio nyumba ya milele ya  ya mpendwa wetu  mke wa Jaji John Ruhangisa, Marehemu Laetitia Kokuhangisa Ruhangisa. Bwana alitoa na bwana ametwaa jina lake libarikiwe.
 Waombolezaji wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa marehemu, Laetitia Kokuhangisa Ruhangisa wakielekea kaburini tayari kwa mazishi.
 Jeneza likishushwa kaburini.

 Jaji John Ruhangisa akiweka udongo kaburini wakati wa 
mazishi ya mke wake.
 Padre aliongoza ibada hiyo akiweka msalaba katika kaburi la Laetitia Kokuhangisa Ruhangisa.
 Jaji John Ruhangisa akifarijiana na watoto wake Moreen (kulia)
 na Fiona. Hakika inahuzunisha.
 Jaji John Ruhangisa na watoto wake wakiweka shada 
la maua kaburini.
 Mshauri wa Kimataifa wa Kujitegemea, Fr. James Rugemalira akisaini katika  kitabu cha maombelezo.
 Mdau Erick Kashasha naye alikuwa ni miongoni mwa waombolezaji waliosaini katika kitabu cha maombolezo.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba akisaini katika kitabu cha maombolezo.(Imeandaliwa na mtandao a www. habari za jamii.com)
MAMIA WAJITOKEZA KUMZIKA KWA HESHIMA KUBWA MKE WA JAJI JOHN RUHANGISA ALIYEFARIKI KWA AJALI YA GARI JIJINI ARUSHA
Dotto Mwaibale

SIMANZI na majonzi viligubika leo jioni  katika mazishi ya mke wa Jaji John Ruhangisa, Marehemu Laetitia Kokuhangisa Ruhangisa aliyefariki kwa ajali ya gari jijini Arusha.

Mazishi hayo yaliyofanyika katika Kijiji cha Ibwera katika mkoani Bukoba.

Viongozi  mbalimbali wa Serikali na vyama vya siasa, Majaji, dini na wageni waalikwa kutoka ndani na nje ya mkoa wa Bukoba walikuwa ni miongoni mwa watu waliohudhuria mazishi hayo.

Akizungumza katika mazishi hayo Rais wa Mahakama ya Afrika Mashariki, Dk. Emmanuel Ugirashebuja alisema kifo cha mke wa Jaji Ruhangisa kiliwashitua na kuwahunisha.

"Kifo cha mke wa mwenzetu kimetusikitisha sana kwani marehemu enzi za uhai wake tulikuwa tukijumuika naye kwa mambo mbalimbali kwa kweli tupepoteza mtu muhimu" alisema 

Ugirashebuja alisema mafanikio yote aliyoanyo Jaji John Ruhangisa yametokana na maisha ya upendo aliyokuwa mke wake kwake ndio maana alipata fursa ya kufanya kazi kwa bidii kwa kuwa hakuwa na matatizo nyumbani kwake.

Mazishi hayo yalihudhuriwa na majaji kadhaa akiwemo Rais aliyepita wa  Mahakama ya Afrika Mashariki, Jaji Nsekela, Jaji Rutakangwa aliye mwakilisha Jaji Mkuu wa Tanzania, Mwakilishi kutoka Halmshauri ya Meru

Mke wa Jaji Ruhangisa alipoteza maisha Oktoba 29 mwaka huu  Tengeru mkoani Arusha wakati akitoka kazini baada ya Hiace aliyokuwa amepanda kugongwa na lori la mafuta.

Katika ajali hiyo watu 12 walipoteza maisha wakiwemo maofisa elimu watatu wa Halmshauri ya Meru.(Imeandaliwa na mtandao a www. habari za jamii.com-simu namba 0712-727062)

MDEE: VIONGOZI WA DINI SIMAMENI KIDETE

Mdee: Viongozi wa dini simameni kidete
MWENYEKITI wa Taifa Baraza la Wanawake CHADEMA, (BAWACHA), Halima Mdee, amesema kuwa siasa za matamko ndizo zinazowapa jeuri watawala hivyo amewashauri viongozi wa dini wasimame kidete kupigania maslahi ya umma kwa vitendo.
Aidha, amesema kuwa Jeshi la polisi lilifikia hatua ya kuwapiga mabomu kutokana na Jeshi hilo kujitoa kwenye majukumu yake ya msingi na kuamua kufanya siasa kwa lengo la kukisaidia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambako lilishitushwa na mapokezi makubwa wanayoyapata kwa wananchi wa kanda ya Ziwa na ujumbe mzito wanaoufikisha, jambo ambalo hawakulitarajia.
Mdee, aliyasema hayo jana wilayani Karagwe, wakati alipokuwa akifanya mahojiano maalum na kituo cha redio jamii cha Fadeco, mara baada ya kumaliza ziara wilayani humo akiwa ameambatana na Makamu wake, Hawa Mwaifunga, Katibu Grace Tendega na Naibu Katibu, Kunti Yusuh.
Alisema kuwa viongozi wa dini wamekuwa wakitoa matamko mara kwa mara wakielezea misimamo yao juu ya mambo mbalimbali yanayoedelea nchini ikiwemo umuhimu wa kuheshimiwa kwa maoni ya wananchi kwenye mchakato wa Katiba, lakini watawala wamekuwa hawawasikilizi hivyo ni vema wakabadili njia ya kufikisha ujumbe.
Mbunge huyo wa Kawe, alisema kuwa suala la katiba ni la kila wananchi hivyo wabadilike waache kulalamika na badala yake wachukue hatua kwa kuhakikisha maoni yao  waliyotoa kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba yanaheshimiwa ikibidi kwa kufanya maandamano ya amani.
Alisema kuwa jukumu la kupigania katiba bora inayozingatia maoni ya wananchi lisiachiwe Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA ), kwani katiba ni kitu muhimu sana, ndiyo injini ya nchi na itasaidia kurekebisha mfumo wa nchi kwani kuna maeneo mengi yana utajiri mkubwa wa rasilimali lakini wananchi wake ni fukara wa kuindukia.
Chanzo:Tanzania Daima

WASHIKILIWA KWA TUHUMA ZA MAUAJI

WATU watatu wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Kagera kwa tuhuma mbalimbali zikiwemo za mauaji na uhalifu mwingine uliofanyika Oktoba mwaka huu, mkoani humo kwa nyakati tofauti.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Henry Mwaibambe alisema kuwa katika tukio la kwanza, waliwakatama watuhumiwa wiwili ambao walikuwa wakijihsusha na mauaji mabalimbali mkoani Kagera likiwemo la mwalimu wa sekondari.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Samitu Haruna (30) fundi pikipiki mwenyeji wa Kyaka wilayani Missenyi ambaye alikiri kuhusika na mauaji ya Ernest Kato (32) fundi ujenzi mkazi wa Kamizilente kata ya Rwamishenye yaliyotokea Oktoba 20, mwaka huu.
Alisema kuwa baada ya polisi kumhoji, alisema kuwa alitumwa na watu ambao polisi wamehifadhi majina yao akafanye uhalifu huo kwa ahadi ya kulipwa ujira wa sh. 450,000 huku akiwa amelipwa sh. 50,000 kama kianzio.
Mtuhumiwa mwingine ni Erick Mwombeki (27), aliyejihusisha na mauaji ya mwalimu Denis Ng’andu (35) wa shule ya Sekondari ya Kagemu mnamo Oktoba 6 mwaka huu, ambapo naye pia alikiri kuhusika na tukio hilo.
Kwa mujibu wa kamanda, polisi wanendelea kuusaka mtandao unaojihusisha na uhalifu huo wa mauji ndani ya Manispaa ya Bukoba ili wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria.
Wakati huo huo, jeshi hilo linamshikilia Wilfred Thomas (40) fundi wa kuchomelea mkazi wa wilayani Ngara kwa tuhuma za kukutwa na noti bandia zenye thamani ya sh. milioni1.1 kama zingekuwa fedha halali.
Kamnda alisema kuwa, Oktoba 26 mwaka huu, polisi wilayani Karagwe walipata taarifa kutoka kwa raia wema kuwa kuna mtu anafanya biashara ya kuuza noti bandia kwa kubadilishana sh. laki moja kwa sh. 40,000 fedha halali na hivyo kuwekewa mtego.
Alisema kuwa baada kupekuliwa alikutwa na noti 227 za sh. 5,000 za bandia na kwamba alipohojiwa alikiri kujihusisha na biashara hiyo na kutaja kuwa fedha hiyo aliipata nchi jirani ya Uganda.
Chanzo;Tanzania Daima

WASHIKILIWA KWA TUHUMA ZA MAUAJI

WATU watatu wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Kagera kwa tuhuma mbalimbali zikiwemo za mauaji na uhalifu mwingine uliofanyika Oktoba mwaka huu, mkoani humo kwa nyakati tofauti.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Henry Mwaibambe alisema kuwa katika tukio la kwanza, waliwakatama watuhumiwa wiwili ambao walikuwa wakijihsusha na mauaji mabalimbali mkoani Kagera likiwemo la mwalimu wa sekondari.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Samitu Haruna (30) fundi pikipiki mwenyeji wa Kyaka wilayani Missenyi ambaye alikiri kuhusika na mauaji ya Ernest Kato (32) fundi ujenzi mkazi wa Kamizilente kata ya Rwamishenye yaliyotokea Oktoba 20, mwaka huu.
Alisema kuwa baada ya polisi kumhoji, alisema kuwa alitumwa na watu ambao polisi wamehifadhi majina yao akafanye uhalifu huo kwa ahadi ya kulipwa ujira wa sh. 450,000 huku akiwa amelipwa sh. 50,000 kama kianzio.
Mtuhumiwa mwingine ni Erick Mwombeki (27), aliyejihusisha na mauaji ya mwalimu Denis Ng’andu (35) wa shule ya Sekondari ya Kagemu mnamo Oktoba 6 mwaka huu, ambapo naye pia alikiri kuhusika na tukio hilo.
Kwa mujibu wa kamanda, polisi wanendelea kuusaka mtandao unaojihusisha na uhalifu huo wa mauji ndani ya Manispaa ya Bukoba ili wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria.
Wakati huo huo, jeshi hilo linamshikilia Wilfred Thomas (40) fundi wa kuchomelea mkazi wa wilayani Ngara kwa tuhuma za kukutwa na noti bandia zenye thamani ya sh. milioni1.1 kama zingekuwa fedha halali.
Kamnda alisema kuwa, Oktoba 26 mwaka huu, polisi wilayani Karagwe walipata taarifa kutoka kwa raia wema kuwa kuna mtu anafanya biashara ya kuuza noti bandia kwa kubadilishana sh. laki moja kwa sh. 40,000 fedha halali na hivyo kuwekewa mtego.
Alisema kuwa baada kupekuliwa alikutwa na noti 227 za sh. 5,000 za bandia na kwamba alipohojiwa alikiri kujihusisha na biashara hiyo na kutaja kuwa fedha hiyo aliipata nchi jirani ya Uganda.
Chanzo:Tanzania Daima

BAWACHA: UWT ACHENI KUWAPUMBAZA WANAWAKE

BAWACHA: UWT acheni kuwapumbaza wanawake
BARAZA la Wanawake wa CHADEMA, (BAWACHA), limejipanga kuhakikishawanawake nchini wanaamka kudai haki zao huku likiuonya Umoja waWanawake wa CCM, (UWT), kuacha kuwapumbaza kwa kuwaimbisha nyimbo zisizo na tija huku ukishindwa kuwapatia ufumbuzi wa kero zao.
Aidha, limedai kuwa kwa sasa wanawake hawahitaji kufundishwa kupika auKuimba, wanataka kupatiwa fursa zao kiuchumi ili waweze kuzitumiakujiongezea kipato kitakachowawezesha kutunza familia zao.
Hayo yalisemwa juzi na Mwenyekiti wa BAWACHA mkoani Kagera, ConchestaRwamlaza, wakati akiwahutubia wananchi wa Biharamulo kwenye uwanja waSoko Jipya, ambako mkutano huo uliwashirikisha uongozi wa BAWACHATaifa.
Alisema kuwa wanawake nchini, wanahitaji huduma bora za afya wanapokwenda kwenye vituo vya afya na hospitali, wanahitaji watoto wao wapate elimu bora shuleni, wanahitaji kupatiwa fursa zao kwenye ardhi na  kiuchumi, waweze kushiriki shughuli za ujasiriamali na kupata kipato cha kutunza familia zao.
“Tunatangaza vita na UWT, waache kuwaimbisha wanawake ‘hiyena hiyena’
wanawake wa Tanzania kwa sasa hawahitaji mafunzo ya kupika… wameshaamka wanataka waelezwe namna watanufaika na rasilimali zilizo kwenye maeneo yao siyo kuwaimbisha nyimbo zisizo na faida,” alisema mbunge huyo wa viti maalum CHADEMA.
KUIZUIA KASI YA CHADEMA NI SAWA NA KUZUIA UPEPO JANGWANI
Kwa upande wake, Mbunge wa Biharamulo, Dk. Anthony Mbasa, alisema CCMhawataweza kuzuia kasi ya CHADEMA kutoa elimu ya uraia kwa wananchi,kwa kile alichodai kuwa atakayejaribu kufanya hilo hatafanikiwa.
“Kasi ya CHADEMA haizuiliki, tutahakikisha tunapita maeneo yote ya nchitutahamasisha wananchi kuikataa Katiba pendekezwa, imetupa maoni yetuwananchi ikahakikisha inalinda maslahi ya kikundi kidogo cha CCM natutahakikisha tunawang’oa na tunaanza kwenye uchaguzi huu wavitongoji, vijiji na mitaa…
“Kuizuia kasi ya CHADEMA ni kazi ngumu, sisi tunaahidi na tunatekeleza,hakuna wa kutuzuia na atakayejaribu ni sawa na kuzuia upepo jangwanijambo ambalo haliwezekani,” alisema Dk. Mbasa.
MIKATABA IKIWA WAZI CCM WANAHOFU KUSHINDWA KUPIGA ‘DILI’
Mwenyekiti wa Taifa BAWACHA, Halima Mdee, alisema wabunge waCCM wameondoa kipengele kinachotaka uwazi kwenye rasimu ya tume yamabadiliko ya Katiba, kwa hofu kuwa watashindwa kupiga dili.
Alisema kuwa Biharamulo kulikuwa na mgodi wa Tulawaka, ambao hivi sasawawekezaji wamemaliza kuchimba dhahabu wamerudisha mashimo kwaserikali, lakini yeye kama mwakilishi wa wananchi bungeni hajui mkatabaulikuwa unasemaje, kwani mikataba ni siri.
Mdee, alimpongeza mbunge wa jimbo hilo kwa kufanya vema kazi ya kuwawakilisha wananchi wake bungeni, kwani ameweza kufanikisha ujenzi wa barabara ya lami kwenye jimbo hilo, jambo ambalo lilishindikana kwa miaka 50 iliyopita
Chanzo:Tanzania Daima

YATIMA WAOMBA UFADHILI WA ELIMU

WATOTO yatima waliohitimu elimu ya awali katika shule ya Tegemeo Kagazi, wameiomba Serikali na taasisi mbalimbali kuwapatia ufadhili ili wajiunge na elimu ya msingi.
Meneja wa Kituo cha Tumaini letu, Kachocho Timanywa, alisema watoto hao wanakabiliwa na changamoto ya kukosa vifaa za shule ambavyo ni madaftari, kalamu, sare na mifuko   ya kubebea daftari.
Alizitaja changamoto nyingine ni msaada wa kadi za huduma ya jamii (CHIF), kutokana na mwaka huu kituo hicho   kumepoteza watoto saba waliofariki kutokana na ukosefu wa huduma za afya zinazosababishwa na kipato duni cha walezi.
Alisema kituo hicho kina upungufu wa fedha za mahitaji ya lishe, upungufu wa matundu ya choo, upungufu wa viti, meza za kusomea na zana za kufundishia kwa vitendo.
Timanywa alisema pia wanakabiliwa na changamoto ya kushindwa kuwahudumia watoto wenye ulemavu na gharama za kuendesha kambi.
Meneja Biashara Benki ya CRDB Tawi la Bukoba, Manase Mbaga, alisema jamii inatakiwa kuacha ukatili kwa watoto na badala yake kuwalea kwa moyo wa upendo ili wapate faraja.
Katika mahafali yaliyoambatana na harambee zaidi ya sh. milioni 2 zilipatikana huku ahadi zikiwa sh milioni 2.1.
Chanzo:Tanzania Daima

‘KAGERA INA WALEMAVU 150,000’

ASAS ya kiraia ya Karagwe Community Based Rehabilitation Program (KCBRT), imesema kuwa, mkoa wa Kagera una jumla ya walemavu 150,000, wanaokabiliwa na changamoto mblimbali.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mtendaji wa asasi hiyo, Agrey Mashanda wakati akisoma risala ya ujenzi wa kituo cha utengemavu kinachotarajiwa kujengwa katika eneo la Nyakanongo Kata ya Ndama kwa kufadhiliwa na shirika la Uholanzi la Lilian Foundation.
Mashanda alisema kuwa idadi hiyo ni sawa na asilimia 5.8 ya watu wote katika mkoa wa Kagera ambapo katika wilaya ya Karagwe, shirika linahudumia zaidi ya walemavu 10,000 katika kaya 31tangu mwaka 2004 hadi 2014.
Alisema kuwa, shirika hilo la Uholanzi limetoa kiasi cha sh. milioni 460, ambapo ujenzi kwa awamu ya kwanza utakamilika kwa kipindi cha miezi tisa kuanzia sasa kabla ya kuanza wa awamu ya pili na ya tatu.
Kwa mjibu wa katibu huyo, jengo hilo ambalo litahusika na shughuli za walemavu litakuwa na ukumbi wa mikutano, nyumba mbili za utumishi, matanki ya maji, vyumba vya walemavu kwa ajili ya mazoezi, jengo la taaluma, chumba cha upasuaji na mazoezi ya viungo.
Aliongeza kuwa ujenzi kwa awamu ya kwanza utagharimu sh.bilioni 150 na kwa awamu ya pili zitatumika sh. million 506 wakati awamu ya tatu itagharimu sh. million 367.
Chanzo;Tanzania Daima

ABIRIA WA MV VICTORIA WAFUNGA BARABARA

ABIRIA walisafiri kwa meli ya Mv Victoria wanaotokea Mkoani Kagera kuelekea jijini Mwanza wamefunga barabara kuu za mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani za Rwanda na Burundi baada ya kukwama katika Bandari ya Kemondo.
Wakizungumza na Tanzania Daima Jumapili kwa nyakati tofauti  baadhi ya abiria waliolala katika bandari hiyo walisema, waliondoka bandari ya Bukoba saa 3 usiku na kufika Kemondo saa 6 usiku jambo ambalo sio la kawaida.
Gervas Mugisha Alisema walilala bandari hapo bila kupewa maelekezo yoyote na kulipopambazuka wananchi waliokuwa safarini wakalazimika kufunga barabara kuu ya magari yaendayo mikoani na nchi jirani za Rwanda na Burundi.
“Abiria wengine wameamua kuondoka kwa sababu hawana mizigo mimi ni mfanyabiasha na nina mizigo hivyo siwezi kuondoka na kuacha mizigo yangu nina subiria utaratibu,” alisema.
Alisema, wakati wanaondoka bandari ya Bukoba baada ya mwendo wa saa 1 walishuhudia meli hiyo ikipoteza mwelekeo muda mfupi baadaye na kuzima na baada ya muda mfupi ili ilianza safari tena.
Mugisha alisema, kuwa kabla ya kufika Kemondo meli hiyo ilizima mara tatu hali  ambayo ilisababisha hofu kwa abiria ambao waliaanza kukimbilia maboya na kunyang’anyana hadi kufikia hatua ya kuyachana na ghafla meli hiyo ilianza safari tena.
Alisema cha kusikitisha walipofika Kemondo abiria waliowakuta hawakuelezwa jambo lolote na waliendelea na shughuli ya kupakia  mizigo ndani ya meli hiyo.
Salum  Sambaa, ambaye ni jamaa  wa  marehemu  aliyekuwa, akisafirisha mwili wa  marehemu kutoka Bukoba kuelekea Mkoani Morogoro kwa mazishi alisema, watumishi wa meli hiyo wameshindwa kuwa na lugha nzuri kwa abiria.
Alisema  muda wote meli hiyo ilipozima hawakutoa taarifa yoyote kwa abiria kwa muda wa zaidi ya saa nne.
Naye nahodha wa meli hiyo, Bembere Samson alisema, meli hiyo ilipata hitilafu katika mfumo wa umeme na kusababisha kupoteza mwelekeo kwa muda wa dakika kumi baada ya hapo hali ilirudi kama kawaida.
Alisema baada ya muda tatizo hilo lilijirudia na walipochunguza walibaini kuwa yanahitajika matengenezo ya kubadilisha kifaa ambacho kinasubiriwa kutoka jijini Mwanza.
Alisema, kuchelewa kufika kwa meli kumetokana na ukubwa wa mzigo uliobebwa ndani ya meli hiyo na sio ubovu kama wanavyodai baadhi ya wananchi.
Afisa mfawidhi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra ) Kapteni Alex Katama alisema, wamezungumza na uongozi wa kampuni hiyo juu ya tukio hilo.
Katama alisema, meli hiyo ipo salama tatizo lililotokea ni la kawaida ambalo limetokana na mfumo wa umeme ulioleta hitilafu.

AUAWA KWA KUCHARANGWA MAPANGA

WATU wasiojulikana wamevamia Kanisa la Pentekoste Assemblies of God ( PAG ) usiku wa kuamkia leo Tawi la Kagemu, Kata ya Kitendaguro Manispaa ya Bukoba na kumuua mwalimu ambaye ni muumini wa kanisa hilo kwa kumcharanga mapanga sehemu mbalimbali ya mwili.
Akizungumza na waandishi wa habari waliofika eneo la tukio na kushuhudia sehemu ya madhabahu ikiwa imetapakaa damu, Mchungaji wa kanisa hilo, Faustine Joseph alisema, wamekuwa na kawaida ya kuomba hadi saa 4 usiku.
Alisema kuwa siku hiyo waliondoka saa 5 usiku na kumuacha marehemu aliyemtaja kwa jina la Dionis Ng’wangu na mwenzake wakiendelea na mkesha wa maombi.
Joseph alisema, alipata taarifa za tukio hilo majira ya saa 8 usiku baada ya kupigiwa simu na majirani wanaoishi karibu na kanisa hilo na kufika eneo hilo huku akikuta polisi nao wakiwa wamefika.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi mkoa wa Kagera, Henry Mwaibambe alisema, kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa manane katika kata hiyo.
Kamanda Mwaibambe alisema mwili wa mwalimu huyo umehifadhiwa katika hospitali ya mkoa huo huku muumini aliyetambuliwa kwa jina la Themistocles ambaye ni fundi ujenzi anaendelea kupata matibabu katika hospitali hiyo.
Alisema waumini hao walivamiwa na kundi la watu wanne hadi sasa mtuhumiwa mmoja amekamatwa kuhusiana na tukio hilo na jina lake limehifadhiwa kwa ajili ya uchunguzi.

TRAFIKI WATATU WAFUKUZWA KAZI


JESHI la Polisi mkoani Kagera limewafukuza kazi askari wake watatu kwa kulifedhehesha jeshi hilo kutokana na kitendo cha kupiga picha inayowaonyesha wawili kati yao wakinyonyana ndimi wakiwa kazini.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Henry Mwaibambe, alisema kitendo kilichofanywa na askari hao kimeshusha hadhi ya jeshi.
Aliwataja askari hao waliofukuzwa ni F.7788 PC Mpaji Mwasumbi, G 2122 PC Fadhili Linga na WP.8898 Veronica Mdeme ambao wote ni wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Misenyi.
Alisema PC Mpaji na WP Veronica walipiga picha inayokwenda kinyume na maadili ya Jeshi la Polisi wakiwa kazini, huku PC Fadhili akiingia matatani kwa kuwapiga picha hiyo chafu askari wenzake na kuisambaza kwenye mitandao ya kijamii.
Kamanda Mwaibambe alisema picha hiyo ilianza kuonekana katika mitandao mbalimbali ya kijamii mapema wiki hii.
Alisema askari PC Fadhili alipiga picha hiyo mwaka 2012 kwa kutumia simu yake ya kiganjani na kuitunza, lakini wiki hii aliamua kuisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kitendo ambacho ni kinyume na kazi yake.
“Napenda kuthibitisha kuwa picha hii iliyoonekana kwenye mitandao ya kijamii ni picha halisi ambayo haijachakachuliwa kabisa.
“Maadili ya kijeshi yapo kisheria na askari wetu wanafundishwa namna ya kuishi katika maisha ya utumishi wa jeshi na si vinginevyo.
“Jeshi halikubaliani na vitendo hivi, ikitokea askari kwenda kinyume lazima achukuliwe hatua kali,” alisema Kamanda Mwaibambe.
Taarifa zaidi kutoka mkoani Kagera, zinaeleza baada ya kusambazwa kwa picha hiyo na kuonekana katika mitandao ya kijamii, WP Veronica alianguka ghafla na kupoteza fahamu kwa mshtuko wa tukio hilo.
Kutokana na hali hiyo, majirani waliokuwa karibu na nyumbani kwake walilazimika kumpatia msaada na kumkimbiza hospitali kwa matibabu, ambako aliruhusiwa juzi jioni kabla ya kutiwa mbaroni.
Chanzo:Mtanznia

TUKILINDANA MIGOGORO ARDHI HAITAKWISHA`

Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka.

Migogoro ya ardhi nchini haitamalizika iwapo viongozi wa serikali wataendelea kuwalinda watu wanaotumia fedha zao ‘kununua’ haki pasipo haki.

Akizungumza na NIPASHE, Mbunge wa Biharamulo (Chadema), Dk. Anthony Mbassa, alisema migogoro hiyo haitakuisha iwapo vitendo vya kulindana kwa baadhi ya viongozi wa serikali na wenye fedha havitaondolewa.

Alisema kulindana huko kunasababisha baadhi ya wananchi kujichukulia sheria mikononi baada ya kushindwa kuridhika na maamuzi yanayotolewa na vyombo vya serikali hususani mahakama.

"Iwapo vitendo vya kulindana miongoni mwa watumishi wa umma na kuwakumbatia watu wenye fedha hususani wafugaji wenye makundi makubwa ya mifugo havitaondolewa, italeta hatari kubwa ya kuendelea kutokea uvunjifu wa amani," alisema.

Alisema baadhi ya wenyeviti wa vijiji wamekuwa wakiuza ardhi yenye ukubwa wa zaidi ya ekari 50 kinyume cha sheria za ardhi kutokana na maslahi yao binafsi hali inayochangia ongezeko kubwa la migogoro hiyo.

Aidha, mbunge huyo alimtaka mkurugenzi wa halmashauri hiyo kutengeneza kikosi kazi kitakachoweza kuratibu kwa haraka migogoro yote inayojitokeza wilayani humo badala ya kuendelea kuwafumbia macho viongozi wasiowaaminifu.

Kwa upande wake, Diwani wa Viti Maalum kata ya Nyakahura (CCM), Ziyuni Hussein, aliwatupia lawama baadhi ya viongozi wa chama na serikali kuwa chanzo cha migogoro hiyo kutokana na kuwakumbatia watumishi wabovu, hatua inayosababisha madiwani hao kushindwa kuchukua hatua za kuwawajibisha kisheria.

Zayuni alisema kila wanapofuatilia kujua wahamiaji wamepata wapi ardhi, huambiwa wamepewa baraka zote kutoka ofisi ya mkuu wa wilaya, mkurugenzi mtendaji na uongozi wa CCM wilayani humo.

Akijibu malalamiko hayo, Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Nassib Mmbaga, licha ya kukiri uwapo wa migogoro ya ardhi alisema atafuatilia kwa ukaribu zaidi ili kuhakikisha hatua za haraka zinachukuliwa kabla ya kutokea uvunjifu wa amani.

Hata hivyo, alisema halmashauri yake inatarajiwa kumpeleka mwanasheria wa halmashauri hiyo kwenda vijijini kutoa elimu kwa mabaraza ya ardhi ya kata ikiwa ni mkakati wa kuwajengea uwezo wa kutatua migogoro hiyo kabla ya kufikia hatua mbaya.
 
CHANZO: NIPASHE

PINDA AVUNJA UKIMYA

WAZIRI Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Kagera, kuutafutia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa katika Manispaa ya Bukoba kwa manufaa ya wananchi.

Bw. Pinda alitoa wito huo juzi wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa Serikali mkoani humo baada ya kupokea taarifa ya Mkoa iliyowasilishwa kwake na Mkuu wa Mkoa huo, Kanali mstaafu Fabian Massawe.

Katika kikao hicho, Bw. Pinda alimuwakilisha Rais Jakaya Kikwete kwenye Maadhimisho ya Siku ya Walimu Duniani ambayo kitaifa yamefanyika jana mkoani humo.

“Naamini viongozi wa Mkoa huu, mtakaa kuzungumza ili muweze kukubaliana na kuondoa kesi iliyopo mahakamani, mkifanya hivyo kazi za kusaidia wananchi zitaendelea.

“Naumizwa na viongozi wa Mkoa huu, kukosa uchungu kwa kuwanyima wakazi wa Manispaa ya Bukoba, haki ya kupata maendeleo, kuna pesa zilizotolewa na Benki ya Dunia kiasi sh. bilioni 18 ambazo zinaweza kupotea kwa sababu ya maslahi binafsi ya watu wachache,” alisema.

Aliongeza kuwa, pesa za maendeleo zinapaswa kufanyiwa maamuzi katika vikao lakini watu wanashindwa kukutana kwa sababu ya mtu mmoja ambaye bila kujali maslahi mapana ya watu, anaenda mahakamani na kuzuia kila kitu kisifanyike hadi matakwa yake yatimizwe.

Akiwasilisha taarifa ya Mkoa huo, Kanali Massawe alisema tatizo la kisiasa katika Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba bado linaendelea ambapo hivi sasa kuna zuio la mahakama la kutofanyika vikao katika halmashauri hiyo ambalo limetolewa Agosti 25 mwaka huu hadi kesi namba 2/2014 itakapohitimishwa.

Alisema kesi hiyo ipo kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Bukoba na nyingine mbili zinaendelea baada ya mahakamani kutoa hukumu ya kesi ya kutaka madiwani sita wavuliwe udiwani Juni 25 mwaka huu.

“Kuna kesi ya rufaa namba 11/2014 katika Mahakama Kuu ya Tanzania hapa Bukoba inayomuhusu Yusufu Ngaiza na wenzake watano dhidi ya Chifu Adronicius Kalumuna na Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba, wakipinga uamuzi wa kuvuliwa udiwani.

“Rufaa hiyo ilipokelewa Julai 18 mwaka huu na imepangwa kusikilizwa Oktoba 13 mwaka huu...kesi ya pili namba 02/2014 ipo Mahakama ya Hakimu Mkazi Bukoba ikimuhusu Anatory Amani ambaye anataka Mkurugenzi wa Manispaa amtambue yeye ni Meya wa Manispaa hiyo na kumpatia haki na stahiki zake,” alisema.

Aliongeza kuwa, kesi hiyo ilifunguliwa Agosti 12 mwaka huu na imepangwa kuanza kusikilizwa Oktoba 6 mwaka huu ambapo Kanali Massawe alifafanua kuwa, kulikuwa na kesi nyingine namba 01/2014 katika Mahakama Kuu ya Anatory Amani dhidi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na mwanahseria Mkuu wa Serikali.

Alisema kesi hiyo ilifunguliwa Machi 7 mwaka huu ambapo mlalamikaji alitaka mambo kadhaa kuhusiana na taarifa ya ukaguzi maalumu ambayo ilitolewa Januari 17 mwaka huu yatenguliwe na mahakama.

“Aliiomba mahakama itengue taarifa hiyo akidai ni batili na isitambulike kisheria lakini mahakama imeiondoa kesi hiyo Septemba 25 mwaka huu kwa sababu ilipelekwa mahakamani hapo kwa kifungu kisicho sahihi.

TATIZO LA MICHE YA KAHAWA KUMALIZIKA

WAKULIMA wa kahawa nchini, wanatarajia kuondokana na kero ya upatikanaji wa miche ya zao hilo, ifikapo Aprili mwaka 2015,baada ya kituo cha uzalishaji wa miche kwa njia ya chupa (Tissue Culture) kuanza kuzalisha miche ya kahawa.

Kituo hicho kijulikanacho kwa jila la Crop Boiscience Solution kilichopo Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha, ambacho kinafanya kazi kwa kushirikiana kwa karibu na taasisi ya utafiti wa kahawa nchini TaCRI, kina uwezo wa kuzalisha miche ya kahawa zaidi ya milioni 10 kwa mwaka.

Akizungumza na waandishi wa habari mkurugenzi mtendaji wa kituo hicho, Bw. Wilfred Mushoboz, alisema uzalishaji huo wa miche ni moja ya njia ambazo zinaweza kuzalisha miche mingi ya kahawa na kuondoa kiu ya Watanzania ya uhitaji wa miche.

"Upungufu wa miche ni moja ya changamoto ambazo zimekuwa zikiwakabili wakulima wa kahawa nchini,lakini kwa sasa changamoto hiyo itaondoka, kwani kituo hiki kuna uwezo wa kuzalisha miche mingi hata zaidi ya milioni 10 kwa mwaka,kulingana na uhitaji wa wakulima;na sasa mchakato wa uzalishaji miche hiyo unaendelea na ifikapo Aprili mwaka 2015,tutaanza kusambaza miche hii," alisema Mushoboz.

Aidha, Mushoboz alisema uzalishaji wa miche hiyo ambao wamekuwa wakiufanya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Kilimo, wamekuwa wakifuata utaalamu waliopewa na Taasisi ya Utafiti wa Kahawa nchini (TaCRI), na kwamba miche wanayozalisha ni bora ambayo imefanyiwa utafiti na ina ukinzani wa magonjwa.

"Miche ya kahawa tunayoizalisha hapa kwa njia ya matawi au vishina, ni ya aina zote yaani Arabica na Rubusta; na ni miche bora ambayo imefanyiwa utafiti na TaCRI; na miche hii ina ukinzani na magonjwa kama chulebuni, kutu ya majani na mnyaoko funzari; na inazaa sana, kwa kweli ifikapo mwezi Aprili mwakani, kilio cha wananchi kuhusu miche ya kahawa ndo itakuwa mwisho," alisema.

Akizungumza mtafiti wa usambazaji teknolojia na mafunzo kutoka TaCRI, Bw. Jeremiah Magesa, alisema kazi yao kubwa ni kuhakikisha teknolojia zote zinazopatikana katika taasisi ya utafiti wa kahawa Tanzania,zinawafikia wakulima.

"Sisi tumekuwa tukizalisha miche bora ya kahawa, lakini kutokana na mahitaji kuwa makubwa tumekuwa tukishirikiana na wadau mbalimbali, kikiwemo kituo cha uzalishaji wa miche kwa njia ya chupa na tumeingia nao mkataba na kama alivyowaambia uzalishaji wake ni mkubwa, tatizo la upungufu wa miche litapungua kama si kwisha kabisa," alisema Magesa.

Wakizungumza baadhi ya wakulima wa kahawa mkoani Arusha walisema TaCRI, imekuwa ikiwapa utaalamu na kuwawezesha kuzalisha miche bora ya kahawa yenye ukinzani, kwa kuwapa vifaa na mbinu za uzalishaji wa miche bora

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa