Home » » Kesi 82 zafutwa kwa kukosa ushahidi

Kesi 82 zafutwa kwa kukosa ushahidi

KESI 82 zilizokaa muda mrefu zimefutwa mkoani Kagera kwa kukosa ushahidi wa kutosha katika kipindi cha mwaka 2012/2013.
 Akizungumza wakati wa sherehe za Siku ya Sheria nchini, jana Mwanasheria Mfawidhi wa Serikali Kanda ya Bukoba, Sakina Sinda, alisema kesi zilizofutwa zilihusisha washitakiwa wa zamani.
 Sinda alisema tatizo la kesi hizo kukaa muda mrefu linatokana na sababu mbalimbali ikiwamo mashahidi kushindwa kufika mahakamani hasa kesi za jinai. 
Alisema ili kuhakikisha tatizo hilo linapungua wanajitahidi kutembelea magereza yote mkoani Kagera na kupitia majalada, lengo ni kubaini kesi zilizodumu muda mrefu bila kusikilizwa ili zitolewe maamuzi.
 “Tunajitahidi kukutana na mahabusu, kuwasikiliza na kubaini matatizo yao, baadaye tunatoa maelekezo ili kesi zao ziharakishwe,” alisema Sinda.
 Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, Gad Mjemmas, alisema suala la haki kutolewa kwa wakati linakabiliwa na changamoto ikiwemo sheria za uendeshaji wa mashauri huku akitolea mfano kifungu namba 225 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.
 Akizungumzia kifungu hicho, Jjaji Mjemmas alisema kinawataka upande wa mashtaka kukamilisha upelelezi  ndani ya siku 60 tangu mshtakiwa kufikishwa mahakamani lakini hakishughuliki na makosa ya kughushi na mauaji ya makusudi au ya bila kukusudia.
 Alisema hayo husababisha mshitakiwa kukaa mahabusu hata miaka 10 kwa kisingizio cha upelelezi kutokamilika, ambapo Mahakama hufungwa mikono kwa kutotoa unafuu kwa mshitakiwa kwa kuwa sheria haijaweka wazi ukomo wa muda wa upelelezi kwa baadhi ya makosa. 
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa