Home » » Kodi ya Zimamoto yamuumiza kichwa Malima

Kodi ya Zimamoto yamuumiza kichwa Malima

Kodi ya Zimamoto yamuumiza kichwa MalimaNAIBU Waziri wa Fedha, Adam Malima, amesema suala la ukusanyaji wa kodi inayotozwa na Jeshi la Zimamoto linamuumiza kichwa kwa madai kuwa hawatoi huduma stahiki kwa wananchi wanaowatoza fedha.

Malima alitoa kauli hiyo mjini Bukoba jana alipozungumza na wafanyabiashara pamoja na wakulima kuhusu mashine za kieletroniki za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na tozo ya Zimamoto baada ya wananchi hao kumtaka kuondoa tozo hiyo.
Alisema kodi si tatizo isipokuwa huduma zinazotolewa na jeshi hilo hazifiki kwa wakati na si stahiki.
Awali mmoja wa wafanyabiashara, Julius Mwamba, alihoji katika kikao hicho kuwa wananchi watalipa kodi ngapi.
Mwamba alisema Tanzania kuna majeshi takribani sita wakiliruhusu jeshi hilo kuendelea kuwatoza kodi baada ya muda majeshi mengine nayo yatadai kulipwa kodi.
“Sijui suala la Jeshi la Zimamoto kukusanya kodi liliibuka kutoka wapi, Tanzania kuna majeshi mengi, kila jeshi likianza kudai kodi tutalipa kodi ngapi?” alihoji mfanyabiashara huyo.
Alisema kodi hiyo haina faida kwa wananchi kwa sababu hawajui matumizi ya fedha hiyo.
Akijibu hoja ya wafanyabiashara hao, Malima alisema jeshi hilo limekuwa likilalamikiwa mara nyingi na wakulima, viwanda, wafanyabiashara na wananchi wa kawaida kwa kutotimiza wajibu wake kwa wakati.
Alisema suala hilo linapaswa kuangaliwa upya huku akisema kuna tofauti kubwa ya kazi kati ya Jeshi la Zimamoto na polisi ambao wamekuwa wakifika kwenye migogoro ya wakulima kwa wakati huku mashamba yakiungua moto zimamoto hawafiki na kuteketea bila msaada licha ya kulipa kodi na wakati mwingine wakifika huwa hawana maji.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa