Home » » Tibaijuka, Mwijage wajinadi kwa sufuria za wali Muleba

Tibaijuka, Mwijage wajinadi kwa sufuria za wali Muleba

WABUNGE wawili wa Muleba Kusini na Kaskazini, Profesa Anna Tibaijuka na Charles Mwijage, wote wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameibuka na mbinu mpya ya kupata wananchi kwa kupika na kugawa wali katika mikutano yao ya hadhara.
Aliyeanza ni Prof. Tibaijuka, ambaye tangu Oktoba mwaka jana alianza kutembea na sufuria za wali kama njia ya kushawishi wananchi kuhudhuria mikutano yake na kumsikiliza.
Mwijage ameanza kutumia mbinu hiyo mwaka huu kama njia ya kurejesha imani ya wananchi kwake na CCM, katika kujaribu kupiku nguvu za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho kinawanyima usingizi katika majimbo yao.
Kwa mara ya kwanza, Prof. Tibaijuka alizuka na sufuria za wali katika Kijiji cha Kiga, Kata ya Rulanda, akiwa na magari matatu yenye sufuria zipatazo sita za wali na kreti kadhaa za soda.
Jana, Mwijage alianza kutumia mbinu hiyo katika Kata ya Kamachumu ambapo alichinja ng’ombe mmoja na kupika wali kwa wingi kama njia ya kuvuta wananchi kuhudhuria mkutano kwa wingi.
Tibaijuka na Mwijage wanakabiliwa na upinzani mkubwa majimboni mwao kutokana na mwamko wa mabadiliko unaosimamiwa na makada na viongozi wa CHADEMA.
Mikutano yao imekuwa ikikosa mvuto, na watu wanahudhuria kwa uchache, jambo lililowalazimisha kubuni njia ya kuvuta wananchi kwa kupika na kugawa wali.
Hata hivyo, mbinu hii imeanza kuwaletea msukosuko katika jamii, kwani wananchi wanaona kama wabunge wao wanawadharau na kuwahonga chakula.
Wananchi wanataka wabunge hao watekeleze ahadi zao badala ya kugawa wali, kwani katika ilani ya uchaguzi waliyoinadi mwaka 2010, hakuna popote walipotangaza kugawa wali kwa wananchi.
Vile vile, baadhi ya wananchi wanadai kwamba kwa hatua hii, Mwijage na Tibaijuka wameanza kudhihirisha kwamba hawakubaliki kwa kiasi cha kutumia vivutio vya chakula kuita na kuteka watu.
Mmoja wa wakazi wa Kamachumu waliokerwa na ‘rushwa’ hii mpya, Justin Kingi, aliliambia gazeti hili jana kuwa: “Mwijage anatafuta watu wapya awadanganye kwa kutumia wali. Ni mbinu dhaifu ya CCM. Haitafanikiwa. Hawezi kupata watu wa maana, labda watoto wadogo na wachezaji mpira ambao watakuwa uwanjani.”
Mkazi mwingine wa Kamachumu, Sylvester Kaboko, alisema: “Amepika kilo 600 za wali na ng’ombe mmoja. Upo wali mwingine umebebwa kutoka Kagera Sugar, hatujui ni kiasi gani… Hiki ni kituko…. watu wanaendelea na shughuli zao.”
Habari zinasema aliwapatia waendesha pikipiki sh 1,000 kila mmoja ili waweke bendera za CCM kwenye pikipiki kupamba maandamano, wengi wakagoma wakisema hawawezi kujidhalilisha kwa shilingi elfu moja.
Muchunguzi Tibalikwenda, mkazi wa Kijiji Rwanda, akizungumza na gazeti hili kutoka Kamachumu, alisema: “Wawindaji wanapenda kwenda na wawindaji wenzao; wachungaji na wachungaji wenzao. Sisi tunataka maskini mwenzetu, atakayewasilisha maoni yetu kunakohusika. Waendelee na wali wao, na muziki wao, sisi tuna shughuli zetu za maendeleo.”
Alipotafutwa Mwijage kufafanua tuhuma hizo, aling’aka akidai amefanya mambo mengi ya maendeleo jimboni na hivyo, asiulizwe vitu vidogo vidogo kama hivyo
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa