Home » » RC awapa kibarua watendaji

RC awapa kibarua watendaji

MKUU wa Mkoa (RC) wa Kagera, Kanali mstaafu Fabian Massawe, amewataka watendaji wa vijiji na kata kuwafikisha mahakamani wazazi wanaowaozesha  watoto wao chini ya umri na wale wanaowapa ujauzito na kuwasababishia kutoendelea  na masomo.
Kanali mstaafu Massawe alitoa wito huo juzi wakati wa maadhimisho ya miaka 37 ya kuzaliwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) yaliyofanyika kimkoa wilayani Kyerwa.
Alisema watendaji wa vijiji na kata hawana budi kuwachukulia hatua watu wanaohusika kuwapa ujauzito wanafunzi na kuwaharibia  ndoto zao za kupata elimu na kuwasababishia  umaskini  na uduni wa maisha.
“Sitakaa kimya kwa hawa mafataki, nitabanana nao katika kipindi chote cha madaraka yangu, hata nikitoka madarakani sitawachoka, nitaendelea  kuwalaani kwani ni watu waharibifu kwa watoto wetu,” alisema mkuu huyo wa mkoa.
Alisema kuna baadhi ya wazazi ambao nao wanachangia kutowapeleka watoto wao shule kwa visingizio vya ugumu wa maisha, na wengine kuwaozesha kabla ya umri nao watafikishwa mahakamani watakapobainika kuhujumu haki za watoto wao.
Alisema serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya shule mbalimbali za msingi na sekondari kwa ajili ya watoto kupata elimu bora na kwamba watoto wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kuanza mwaka huu wataingia darasani bila matatizo, kwa kuwa  miundombinu ya kila shule, vyumba vya madarasa, madawati na walimu vinakidhi kiwango.
Chanzo;tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa