Home » » CHADEMA kususia Uchaguzi Mkuu 2015

CHADEMA kususia Uchaguzi Mkuu 2015

image

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetoa sharti ambalo kama halitatekelezwa chama hicho hakitashiriki Uchaguzi Mkuu wala hakitapiga kura ya kupitisha rasimu ya katiba.


Sharti hilo lilitolewa mjini Bukoba juzi na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, wakati akihutubia katika mkutano wa hadhara ikiwa ni mwendelezo mikutano ya Operesheni ya M4C Pamoja Daima uliofanyika katika Uwanja wa Mashujaa na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa watu.
Alisema chama hicho hakitashiriki uchaguzi iwapo Serikali haitaboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu na upigaji kura wa rasimu ya katiba.
Mbowe alisema kwa jins hali inavyoonesha Serikali haioneshi nia ya kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura wakati tunaelekea katika uchaguzi Mkuu mwakani.
Alisema katika utafiti wao wamebaini kuwepo kwa vijana zaidi ya milioni 5.3 ambao wamefikisha umri wa miaka 18 wanaotakiwa kushiriki kupiga kura mwakani kuchagua viongozi wao.
Alisema katika hilo nchi itasimama kwa vile kama tunahitaji mabadiliko hayawezi kufanyika bila kuboresha daftari la kura. Kuhusu Rasimu ya Katiba, Mbowe aliapa mbele ya mkutano huo kuwa mwaka huu ndio atang’olewa meno bungeni, kwani hawatakuwa tayari kuburuzwa wakati wa Bunge la Katiba lijalo .
Alisema:“Suala la katiba halina masihara ni maisha yenu, maisha ya watoto wenu, maisha ya vizazi na vizazi, ni maisha ya taifa letu kila Mtanzania mwenye umri wa miaka 18 wa kupiga kura lazima apige kura kukubali rasimu ya katiba mpya, nasi Bungeni hatutakubali kuburuzwa. ”
Alisema kutokana na hali hiyo, wananchi wanapaswa kujitokeza kwa wingi kujadili rasimu ya katiba mpya. Alisema bunge lijalo la katiba wao wanaenda kujadili rasimu ya Katiba Mpya ambayo tayari wameshaona .
“Tayari CCM wanampinga Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba kuhusiana na maoni ya wananchi kutaka serikali tatu, wakati wao haimo kwenye sera yao, hapa kuna tatizo, kwani sisi tunaenda kujadili maoni yawananchi wengi si kutetea sera za vyama vya siasa,” alisema.
Alisema katiba si suala la kidini, sera za vyama vya siasa wala la kikabila , bali ni ya watu wote kwa ajili ya mustakabali wa maisha na taifa kwa ujumla, hivyo hawaendi Dodoma kwa ajili ya kupinga Katiba hiyo, bali kupitisha maoni ya wananchi wanavyotaka.
Pamoja na mambo mengi, Mbowe aliwapongeza madiwani wa Manispaa hiyo bila kujali itikadi za vyama kuungana kupinga ufujaji wa kodi za wananchi maskini wa Manispaa uliokuwa ukifanyika ndani ya Manispaa hiyo.
“Mimi napenda kuwapongeza Madiwani wa Manispaa ya Bukoba pamoja na Mbunge wao, Balozi Kagasheki, ambao kwa pamoja walisimama kutetea maslahi ya wananchi wa Bukoba, ukweli tuuseme na mnyonge mnyongeni na haki yake mpeni,” alisema.
Wakati huo huo, Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA),Tundu Lissu, amewaonya baadhi ya wanasiasa wanaotumia makanisa na misikiti kuwashawishi wananchi ili wawachague kuwa viongozi katika uchaguzi wa mwaka huu 2014/15.
Lissu aliyasema hayo wakati alipokuwa akizungumza katika mikutano miwili iliyofanyika katika Kijiji cha Ilongero na Mjini Singida juzi wakati akiwa kwenye siku ya kwanza ya ziara ya ujumbe wa chama hicho ikiwa ni mwendelezo wa Operation M4C Pamoja Daima itakayofanyika nchi nzima.
Alisema kuwa pamekuwa na tabia ya baadhi ya wanasiasa Wakristo na Waislamu ambao hupita makanisani na misikitini na kutoa fedha kwalengo la kujijengea umaarufu jambo ambalo aliwataka wananchi wawe macho nao.
Alisema pamoja na wanasiasa hao kujiwekea mazingira ya kushawishi wananchi ili wawachague, Watanzania hawawakubali kwani hiyo inaweza kuleta tofauti za kidini.
“ Lazima tukumbuke mafundisho ya Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere ambayo yalisisitiza kuzingatia amani, upendo na mshikamano kwa kuepuka kugawanywa na watu hao,” alisema.
Kuhusu Katiba Rasimu ya Pili ya Katiba, alisema ni nzuri na kuzingatia vipengele vingi vilivyotolewa maoni kurekebishwa kazi ambayo ilifanywa na CHADEMA pamoja na wananchi wengine.
Alisema suala kubwa ni kuona kuwa Rasimu hiyo haichakachuliwi kwa manufaa ya chama cha siasa au viongozi kwa ajili ya maslahi yao.
“Tunasisitiza kuwepo kwa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga kura kuboreshwa ili wananchi wengi wakiwemo vijana waliofikia umri huo na wale waliopoteza shahada zao waweze kushiriki katika zoezi laku pigakura za maoni,”alisema.
Katika hatua zingine , Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa CHADEMA Taifa, John Henje, alisema chama hakitavumilia mtu yeyote anayetaka kukizamisha chama hicho. “Mtu yeyote akileta
 mchezo atafukuzwa, CHADEMA itaendelea kwani hakuna aliye mkubwa au maarufu kuliko wanachama,” alisema. Alieleza kuwa chama hicho kitaendelea kuwepo na kinachotakiwa sasa ni kuzungumzia mambo ya msingi yanayokijenga na kukiendeleza.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa