Home » » Diwani asomewa shtaka kitandani

Diwani asomewa shtaka kitandani

DIWANI wa Kata ya Magata Kalutanga, Geofrey Ezekiel (CCM), aliyekamatwa juzi na kuwekwa ndani kwa amri ya Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Limbris Kipuyo, jana alisomewa shtaka akiwa kitandani katika  Kituo cha Afya Kaigara.
Taarifa zilizolifikia gazeti hili kutoka wilayani humo, zilisema kuwa Ezekiel alisomewa shtaka hilo namba 11/ 2014 saa 4:30 asubuhi akidaiwa kutishia kumjeruhi mkuu wa wilaya kwa kummwagia tindikali.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu, mtoa taarifa wetu alisema kuwa diwani huyo alisomewa shtaka hilo na Kaimu Hakimu wa Mahakama ya wilaya aliyetambulika kwa jina moja la Ngonyani.
“Anadaiwa kutenda kosa hilo Januari 6, mwaka huu. Lakini mpaka sasa tunashughulikia dhamana maana alishutukizwa, hakuwa ameandaa wadhamini. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Febuari 3, mwaka huu,” alisema.
Ezekiel alikamatwa juzi akidaiwa kutishia kumuua mkuu wa wilaya na baada ya mahojiano na polisi alipekuliwa nyumbani kwake kisha kushikiliwa kituoni hadi saa 12:00 jioni afya yake ilipobadilika ghafla na kukimbizwa hospitali.
Chimbuko la mzozo huo ni baada ya diwani huyo kuandika barua ya kumshtaki mkuu huyo kwa uongozi wa CCM Wilaya ya Muleba kwa kile kilichoelezwa ni kutuhumiwa kula fedha za miradi.
Kipuyo anadaiwa kumtuhumu diwani huyo katika kikao cha Kamati ya Siasa ya Wilaya cha CCM cha Januari 5, mwaka huu, kuwa anatumia wadhifa wake wa uenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Ujenzi na Mazingira kufuja fedha za miradi akishirikiana na wahandisi wa halmashauri.
Pia alidai kuwa diwani huo anakwamisha miradi ya maendeleo kwa makusudi, tuhuma ambazo alizirudia mbele ya kikao cha Kamati Kuu ya Wilaya cha Januari 6, mwaka huu.
Baada ya Kipuyo kubaini ameshtakiwa kwa uongozi wa CCM, alitumia mamlaka yake kuagiza polisi wamkamate diwani huyo na kumchukulia hatua za kisheria, akidai ametishia kumuua kwa tindikali.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa