Home » » Mbowe apongeza kung’olewa Amani

Mbowe apongeza kung’olewa Amani

MWENYEKITI  wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe,  amewapongeza madiwani wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM ), CHADEMA na Mbunge wa Bukoba Mjini, Khamisi Kagasheki kwa kusimama  kidete kutetea masilahi ya wananchi wa Bukoba kuhusu  tuhuma za  ufisadi dhidi ya Meya wa Manispaa ya Bukoba, Dk. Anatory  Amani.
Mbowe alisema  hayo wakati akihutubia maelfu ya wakazi wa Bukoba waliojitokeza  katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa kumbukumbu  wa Mayunga (UHURU PLATFOM ), hali iliyosababisha vijana wa ulinzi wa chama hicho kuwazuia wananchi kuendelea kuingia ndani ya uwanja huo kutokana na idadi kubwa ya watu.
Alisema taarifa ya Mdhibiti na  Mkaguzi Mkuu  wa Hesabu za Serikali (CAG), ilibaini kuwa ubadhirifu uliosimamiwa na meya  ni zaidi ya sh bilioni mbili, ambazo ni fedha za wananchi zinazotokana na kodi.
Alisema mtu yeyote akifanya jambo jema lazima apongezwe bila kujali anatoka chama gani hata kama si wa chama chako.
Hata hivyo alifafanua kuwa CCM ina mng’ang’ania Meya Amani wakati kuna uchafu mwingi  unaofanywa  na viongozi  wa juu,  ukiwemo wizi  wa sh bilioni mbili, fedha zilizofujwa na Amani  ni fedha chache ukilinganisha na zinazoibwa na viongozi wa ngazi  ya juu na hawachukuliwi hatua yoyote.
Alisema sakata la Bukoba limewagawa watu katika misingi ya udini kwa waumini wa dini  anayoabudu meya huyo na kumtetea wakati amefanya ubadhirifu wa fedha za umma, kitu ambacho si sawa  na hata dini hazisemi hivyo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika, alisema viongozi wa serikali wanafanya ufisadi mkubwa  lakini hawachukuliwi hatua na matokeo yake wananchi wanaumizwa kwa kupandishiwa  gharama za maisha.
Mnyika alisema  mawaziri waliojiuzulu kwa kashfa za kifisadi  kwa kusaini mikataba mibovu ikiwamo ya Richmond wanaendelea kutamba  kwa fedha za wananchi wa Tanzania.
Aidha, alisema kujiuzulu kwa Kagasheki katika nafasi ya uwaziri haitoshi, kwani anapaswa kujiuzulu na ubunge kwa kushindwa kusimamia wizara yake na wananchi waliomtuma  kuwawakilisha  bungeni kwa  kupeleka kero zao ili zitatuliwe.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa