Home » » KAGERA YATANGAZA KUPAMBANA NA UGONJWA WA UNYANJAO

KAGERA YATANGAZA KUPAMBANA NA UGONJWA WA UNYANJAO

Mkoa wa Kagera umetangaza oparesheni maalum ya kutokomeza ugonjwa wa unyanjano unaoshambulia migomba kwa mwaka 2014, kwa lengo la kuhakikisha ifikapo mwishoni mwa mwaka huu ugonjwa huo uwe umekwisha kabisa.

Katibu tawala wa mkoa wa Kagera Nassor Mnambila amesema kuwa oparesheni hiyo iliyopewa jina la “oparesheni tokomeza unyanjano”, itafanyika katika wilaya zote za mkoa huo, kuanzia ngazi za vitongoji.

Mnambila amesema kuwa kuanzia Januari hadi Juni ni kipindi cha wananchi kung’oa na kuchoma moto migomba iliyoathirika kwa hiari na kuwa baada ya hapo kuanzia mwezi Julai kikosi kazi kitavamia mashamba yote yaliyoathirika na kung’oa migomba hiyo kwa nguvu.

Amesema kuwa wananchi na watendaji watakaobainika kukwamisha zoezi hilo watashtakiwa kwa sheria ndogo zilizotungwa na halmashauri kwa ajili ya kupambana na ugonjwa huo na sheria ya kilimo ya kudhibiti magonjwa.

Amesema wana mpango wa kutoa elimu kwa maafisa ugani ili waujue vizuri ugonjwa huo, ndipo wataweza kushiriki kikamilifu, na kuwa pia wananchi wataendelea kuelimishwa kuhusu njia bora za kupambana na ugonjwa huo kwa kushirikiana na kituo cha utafiti wa kilimo cha Maruku.

Akizungumzia oparesheni hiyo mkuu wa mkoa wa Kagera kanali mstaafu Fabian Massawe amesema kuwa tayari halmashauri zote zimekwishaandaa sheria ndogo kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa huo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kagera Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa